Misaada ya Kujifunza
Smith, Joseph, Mdogo


Smith, Joseph, Mdogo

Nabii aliyechaguliwa kurejesha Kanisa la kweli la Yesu Kristo duniani. Joseph Smith alizaliwa katika jimbo la Vermont katika Marekani na aliishi tangu mwaka 1805 hadi 1844.

Katika mwaka 1820, Mungu Baba na Yesu Kristo walimtokea Joseph, na alijifunza kwamba katika makanisa ya duniani hakuna hata moja lililokuwa la kweli (JS—H 1:1–20). Kisha baadaye alijiwa na malaika Moroni, aliyemfunulia mahali palipofichwa mabamba ya dhahabu ambayo yalikuwa na kumbu kumbu ya watu wa kale walioishi katika bara la Marekani (JS—H 1:29–54).

Joseph alitafsiri yale mabamba ya dhahabu na katika mwaka 1830 akayachapisha kama Kitabu cha Mormoni (JS—H 1:66–67, 75). Katika mwaka 1829, alipokea mamlaka ya ukuhani kutoka kwa Yohana Mbatizaji na Petro, Yakobo, na Yohana (M&M 13; 27:12; 128:20; JS—H 1:68–70).

Kama alivyoongozwa na Mungu, mnamo 6 Aprili 1830, Joseph na watu wengine kadhaa wakaanzisha Kanisa lililorejeshwa la Yesu Kristo (M&M 20:1–4). Chini ya uongozi wa Joseph, Kanisa lilikua katika Kanada, Uingereza, na sehemu za mashariki za Marekani, hususani katika Ohio, Missiouri, na Illinois. Mateso makali yaliwafuata Joseph na Watakatifu popote walipohamia. Mnamo 27 Juni 1844, Joseph na kaka yake Hyrum waliuawa katika kifo cha kishahidi katika Carthage, Illinois, katika Marekani.

Maandiko yaliyoletwa na Joseph Smith Nabii

Joseph alitafsiri sehemu ya yale mabamba ya dhahabu aliyopewa na malaika Moroni, tafsiri ambayo ilichapishwa katika mwaka 1830 kama Kitabu cha Mormoni. Pia alipokea mafunuo mengi kutoka kwa Bwana yakielezea mafundisho ya msingi na muundo wa Kanisa. Mengi ya mafunuo haya yalikusanywa katika kile ambacho sasa kinajulikana kama Mafundisho na Maagano. Pia alihusika katika kuleta Lulu ya Thamani Kuu, yenye tafsiri ya kuongozwa na Mungu ya baadhi ya maandiko ya Musa, Ibrahimu, na Mathayo, dondoo kutoka historia yake binafsi na ushuhuda, na kauli kumi na tatu za mafundisho na imani zinazoshikiliwa na Kanisa.