Misaada ya Kujifunza
Biblia


Biblia

Mkusanyiko wa maandiko ya Kiebrania na Kikristo ambayo yana mafunuo matakatifu. Neno biblia maana yake “vitabu.” Biblia ni kazi ya manabii wengi na waandishi wengine waliokuwa wakiandika chini ya maongozi ya Roho Mtakatifu (2 Pet. 1:21).

Biblia ya Kikristo ina pande mbili, hujulikana kama Agano la Kale na Jipya. Agano la Kale linajumuisha vitabu vya maandiko yaliyotumika miongoni mwa Wayahudi wa Filisti wakati wa huduma ya Bwana hapa duniani. Agano Jipya lina maandiko yaliyoandikwa nyakati za Kitume na huheshimika kama yana utakatifu na mamlaka sawa sawa na yale maandiko ya Kiyahudi. Vitabu vya Agano la Kale vimechukuliwa kutoka vitabu vya maandiko mbali mbali ya kitaifa yaliyoendelezwa kwa karne nyingi nayo yalikuwa kwa ujumla yameandikwa katika Kiebrania, wakati vile vitabu vya Agano Jipya ni kazi ya kizazi kimoja tu, nayo kwa kiwango kikubwa yalikuwa yameandikwa katika Kiyunani.

Katika Agano la Kale neno ushuhuda liliwakilisha neno la Kiebrania lenye maana ya “agano.” Agano la Kale ni torati iliyotolewa kwa Musa wakati Israeli walipokataa utimilifu wa injili iliyokuwa na watu wa Mungu kutoka mwanzo wa uhai. Agano Jipya ni injili kama ilivyofundishwa na Yesu Kristo.

Katika Biblia ya Kiebrania (Agano la Kale) vitabu hivi viligawanywa katika makundi matatu: Sheria, Manabii, na Maandiko. Biblia iliyotumiwa na ulimwengu wa Wakristo imeweka vitabu hivi katika madaraja kulingana na mada, kama vile vya kihistoria, vya kishairi, na vya kinabii.

Vitabu vya Agano Jipya kwa ujumla viko katika mpangilio huu: Injili nne na Matendo ya Mitume; nyaraka za Paulo; nyaraka kwa watu wote za Yakobo, Petro, Yohana, na Yuda; na Ufunuo wa Yohana.

Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho linatukuza na kuheshimu sana Biblia na linasisitiza pia kwamba Bwana anaendelea kutoa ufunuo wa nyongeza kupitia manabii Wake katika siku hizi za mwisho ufunuo ambao unaunga mkono na kuthibitisha yaliyoandikwa katika biblia juu ya matendo ya Mungu kwa wanadamu.