Maandiko Matakatifu
Mafundisho na Maagano 38


Sehemu ya 38

Ufunuo uliotolewa kupitia Joseph Smith Nabii, huko Fayette, New York, 2 Januari 1831. Tukio lilikuwa ni mkutano wa Kanisa.

1–6, Kristo aliviumba vitu vyote; 7–8, Yeye yupo katikati ya Watakatifu Wake, ambao hivi karibuni Watamwona; 9–12, Wenye mwili wote wameharibika mbele Zake; 13–22, Ameihifadhi nchi ya ahadi kwa ajili ya Watakatifu Wake sasa na hata milele; 23–27, Watakatifu wameamuriwa kuwa na umoja na wachukuliane kama vile ni ndugu; 28–29, Vita vyatabiriwa; 30–33, Watakatifu watapewa uwezo kutoka juu nao watakwenda miongoni mwa mataifa yote; 34–42, Kanisa limeamriwa kuwajali maskini na wenye shida na kuutafuta utajiri wa milele.

1 Hivyo ndivyo asemavyo Bwana Mungu wenu, hata Yesu Kristo, Mimi Ndimi Mkuu, Alfa na Omega, mwanzo na mwisho, yule yule ambaye aliangalia uwazi mpana wa milele, na majeshi yote ya maserafi wa mbinguni, kabla ya ulimwengu kufanyika;

2 Yeye yule ajuaye vitu vyote, kwani vitu vyote vipo mbele ya macho yangu;

3 Mimi ni yeye yule ambaye alinena, na ulimwengu ukafanyika, na vitu vyote vilikuja kwa njia yangu Mimi.

4 Mimi ni yeye yule niliyechukua Sayuni ya Enoki kifuani mwangu mwenyewe; na amini, ninasema, wengi wameamini katika jina langu, kwani Mimi ndiye Kristo, na katika jina langu mwenyewe, na kwa nguvu za damu yangu ambayo nilimwaga, nimewatetea mbele za Baba.

5 Lakini tazama, mabaki ya uovu nimeyaweka katika minyororo ya giza hadi siku ile kuu ya hukumu, ambayo itakuja mwisho wa dunia;

6 Na hivyo ndivyo nitakavyo acha wafungwe, ili kwamba wasiweze kuisikia sauti yangu ila wataishupaza mioyo yao, ole, ole, ole, hayo ndiyo maangamizi yao.

7 Lakini tazama, amini, amini, ninawaambia kuwa macho yangu yanawaangalia. Mimi nipo katikati yenu nanyi hamuwezi kuniona;

8 Lakini siku i karibu kuja ambayo mtaniona, na kujua kuwa Mimi ndimi; kwa kuwa utaji wa giza karibu utaondolewa, na yule ambaye hakutakaswa hataweza kukaa siku hiyo.

9 Kwa hiyo, fungeni viuno vyenu na kuwa tayari. Tazameni, ufalme ni wenu, na wala adui hatawashinda.

10 Amini, ninawaambia, ninyi ni safi, lakini siyo wote; na hapana mwingine ninayependezwa naye;

11 Kwani wenye mwili wote wameharibika mbele zangu; na nguvu za giza zimetapakaa juu ya dunia, miongoni mwa wanadamu, katika uwepo wa majeshi yote ya mbinguni—

12 Ambao husababisha ukimya kutawala, na mbingu yote yaumia, na malaika wanasubiri amri kuu ya kuangamiza dunia, kukusanya magugu ili wapate kuyachoma moto; na, tazama, adui amejikusanya.

13 Na sasa ninawaonyesha siri, kitu ambacho kilikuwa sirini, ambacho kingeleta angamizo lenu katika wakati wake, na ninyi hamkujua hilo;

14 Lakini sasa ninawaambia ninyi, na mmebarikiwa ninyi, siyo kwa sababu ya uovu wenu, wala siyo kwa sababu ya mioyo yenu isiyoamini; kwani hakika baadhi yenu mna hatia mbele zangu, lakini nitawasamehe udhaifu wenu.

15 Kwa sababu hiyo, kuweni imara tangu sasa; msiogope, kwani ufalme ni wenu.

16 Na kwa ajili ya wokovu wenu ninatoa amri hii kwenu, kwani nimesikia sala zenu, na maskini wamelalamika mbele zangu, na matajiri nimewaumba, na viumbe vyote ni vyangu, na mimi sina upendeleo.

17 Na nimeifanya dunia kuwa tajiri, na tazama nayo ni mahali pangu pa kuweka miguu, kwa sababu hiyo, tena nitasimama juu yake.

18 Na Mimi ninatoa na ninataka kuwapa ninyi utajiri mkubwa, hata ile nchi ya ahadi, nchi itiririkayo maziwa na asali, nchi ambayo haitakuwa na laana wakati Bwana ajapo;

19 Nami nitaitoa kwenu kuwa nchi ya urithi wenu, kama mtaitafuta kwa mioyo yenu yote.

20 Na hili litakuwa agano langu na ninyi, mtaipata kama nchi yenu ya urithi, na kwa urithi wa watoto wenu milele, kadiri ya dunia itakavyoendelea kuwepo, na ninyi mtaimiliki tena milele yote, wala siyo ya kupita tena.

21 Lakini, amini ninawaambia kwa wakati hamtakuwa na mfalme wala mtawala, kwa kuwa Mimi nitakuwa mfalme wenu na kuwalinda.

22 Kwa hiyo, isikieni sauti yangu na mnifuate, na mtakuwa watu huru, hamtakuwa na sheria bali sheria zangu wakati nitakapokuja, kwa kuwa Mimi ni mtoaji sheria wenu, na ni kipi kitakachouzuia mkono wangu?

23 Lakini, amini ninawaambia, fundishaneni kulingana na ofisi ambayo nimewateua;

24 Na kila mtu na ampende ndugu yake kama vile ajipendavyo mwenyewe, na kutenda wema na utakatifu mbele zangu.

25 Na tena ninakuambia, kila mtu na ampende ndugu yake kama vile ajipendavyo yeye mwenyewe.

26 Kwani ni mtu gani miongoni mwenu mwenye watoto kumi na wawili, na asiye na upendeleo, na watoto wote wanamtumikia kwa utiifu, na amwambie mmoja wao: Vaa majoho na ukae hapa; na kwa mwingine: Kavae matambara na ukakae pale—naye awaangalie watoto wake na kujisemea kuwa mimi ni mtu wa haki?

27 Tazama, hili nimelitoa kwenu kama mfano, na hivyo ndivyo nilivyo. Ninawaambia, muwe na umoja; na kama hamna umoja ninyi siyo wangu.

28 Na tena, ninawaambia kuwa adui katika vyumba vya siri ayatafuta maisha yenu.

29 Mnasikia juu ya vita katika nchi za mbali, na mnasema kwamba karibu kutakuwa na vita vikali katika nchi za mbali, lakini hamjui mioyo ya watu wa nchi yenu yenyewe.

30 Ninawaambia ninyi haya kwa sababu ya sala zenu; kwa hiyo, ihifadhini hekima katika vifua vyenu, wasije watu waovu wakayafunua mambo haya kwenu kwa uovu wao, katika namna ambayo itasema kwa sauti kubwa masikioni mwenu kuliko ile ambayo itaitikisa dunia; lakini kama mmejitayarisha hamtaogopa.

31 Na hivyo muweze kuiepuka nguvu ya adui, na kukusanyika kwangu watu wenye haki, pasipo mawaa na aibu—

32 Kwa hivyo, kwa sababu hii, niliwapa amri kuwa yawapasa kwenda mto Ohio; na huko nitawapa sheria yangu; na huko mtajaliwa uwezo kutoka juu;

33 Tokea wakati huo, yeyote nitakayemhitaji atakwenda miongoni mwa mataifa yote, nao wataambiwa nini cha kufanya; kwani ninayo kazi kubwa inayosubiriwa, kwani Israeli itaokolewa, na Mimi nitawaongoza kokote nitakako, na hakuna nguvu itakayozuia mkono wangu.

34 Na sasa, ninatoa amri kwa kanisa katika sehemu hizi, kuwa watu fulani miongoni mwao watateuliwa, na wateuliwa kwa sauti ya kanisa;

35 Na watawaangalia maskini na wenye shida, na kuwapatia msaada ili kwamba wasiteseke; na kuwapeleka mahali ambapo nimewaamuru wao;

36 Na hii ndiyo itakuwa kazi yao, kusimamia mambo yahusuyo mali za kanisa hili.

37 Na wale wenye mashamba ambayo hayawezekani kuuzwa, na yaachwe au yakodishwe kama vile wao wanavyoona inafaa.

38 Hakikisheni kwamba vitu hivi vyote vinahifadhiwa; na wakati watu watakapojaliwa uwezo kutoka juu na kutumiwa, vitu hivi vyote vikusanywe kwenye kifua cha kanisa.

39 Na endapo mtatafuta utajiri ambao ni mapenzi ya Baba kuwapeni ninyi, mtakuwa matajiri kuliko watu wote, kwa kuwa mtakuwa na utajiri wa milele; na ni kweli kwamba utajiri wa ulimwengu ni wangu na mimi huutoa; lakini jihadharini na majivuno, msije mkawa kama Wanefi wa kale.

40 Na tena, ninawaambia, amri ninawapa, kwamba kila mtu, mzee, kuhani, mwalimu, na pia muumini, aende kwa nguvu zake, kwa kazi za mikono yake, kutayarisha na kutimiliza mambo ambayo nimeyaamuru.

41 Na mahubiri yenu yawe sauti ya kuonya, kila mtu kwa jirani yake, katika upole na unyenyekevu.

42 Na tokeni huko miongoni mwa waovu. Jiokoeni wenyewe. Kuweni safi ninyi mnaochukua vyombo vya Bwana. Hivyo ndivyo. Amina.