Maandiko Matakatifu
Mafundisho na Maagano 39


Sehemu ya 39

Ufunuo uliotolewa kupitia Joseph Smith Nabii kwa James Covel, huko Fayette, New York, 5 Januari 1831. James Covel ambaye alikuwa mchungaji wa Kimethodisti kwa karibu miaka arobaini, aliagana na Bwana kuwa atatii amri yoyote ambayo Bwana atampa kupitia Joseph Nabii.

1–4, Watakatifu wanao uwezo wa kuwa wana wa Mungu; 5–6, Kuipokea injili ni kumpokea Kristo; 7–14, James Covel anaamriwa kubatizwa na kufanya kazi katika shamba la mizabibu la Bwana; 15–21, Watumishi wa Bwana wataihubiri injili kabla ya Ujio wa Pili; 22–24, Wale ambao huipokea injili watakusanyika wakati huu na hata milele.

1 Sikiliza na sikia sauti yake yeye aliye wa kutoka milele hadi milele yote; Mimi Ndimi Mkuu, hata Yesu Kristo—

2 Nuru na uzima wa ulimwengu; nuru ingʼaayo gizani na hata giza haikuitambua;

3 Yeye yule ambaye alikuja wakati wa meridiani alikuja kwa walio wangu, na walio wangu hawakunipokea;

4 Bali wote walionipokea, niliwapa uwezo wa kufanyika wana wangu; na vivyo hivyo nitawapa wale wote wanipokeao Mimi, uwezo wa kufanyika wana wangu.

5 Na amini, amini ninakuambia, yeye aipokeaye injili yangu anipokea Mimi, na yeye asiyeipokea injili yangu hanipokei Mimi.

6 Na hii ni injili yangu—toba na ubatizo wa maji, na halafu huja ubatizo wa moto na Roho Mtakatifu, hata Mfariji, aonyeshaye mambo yote, na afundishaye mambo ya amani yaliyo ya ufalme.

7 Na sasa, tazama, ninakuambia, mtumishi wangu James, nimeziangalia kazi zako na ninakujua wewe.

8 Na amini, ninakuambia, moyo wako sasa ni mnyoofu mbele zangu kwa wakati huu; na, tazama, nimeweka baraka kubwa juu ya kichwa chako;

9 Hata hivyo, wewe umeona huzuni kuu, kwa kuwa umenikataa mimi mara nyingi kwa sababu ya kiburi na shughuli za ulimwengu.

10 Lakini, tazama, siku za ukombozi wako zimefika, kama utaisikiliza sauti yangu, ambayo yasema kwako wewe: Simama na ubatizwe, na ukaoshe dhambi zako, ukilingana jina langu, nawe utampokea Roho wangu, na baraka kubwa namna hii ambayo kamwe hujazijua.

11 Na kama wewe utafanya haya, nimekutayarisha kwa ajili ya kazi kuu. Wewe utahubiri utimilifu wa injili yangu, ambayo nimeileta katika siku hizi za mwisho, agano ambalo nimelileta ili kuwarejesha watu wangu, ambao ni wa nyumba ya Israeli.

12 Na itakuwa kwamba uwezo utakuwa juu yako; utakuwa na imani kubwa, na Mimi nitakuwa pamoja na wewe na nitatangulia mbele ya uso wako.

13 Na umeitwa kufanya kazi katika shamba langu la mizabibu, na kulijenga kanisa langu, na kuistawisha Sayuni, ili kwamba iweze kufurahi juu ya vilima na kustawi.

14 Tazama, amini, amini, ninakuambia, hujaitwa kwenda katika nchi za mashariki, bali umeitwa kwenda Ohio.

15 Na kadiri watu wangu watakavyokusanyika wenyewe kule Ohio, nimeweka katika ghala baraka ambayo haijapata kujulikana miongoni mwa wanadamu, nayo itamiminwa juu ya vichwa vyao. Na kutokea huko watu watakwenda katika mataifa yote.

16 Tazama, amini, amini, ninakuambia, kwamba watu huko Ohio wananilingana katika imani kubwa, wakifikiria kuwa nitauzuia mkono wangu katika hukumu juu ya mataifa, lakini siwezi kulikana neno langu.

17 Kwa hiyo anza kazi kwa nguvu zako zote na waite wafanyakazi waaminifu katika shamba langu la mizabibu, ili liweze kupogolewa kwa mara ya mwisho.

18 Na kadiri watakavyotubu na kupokea utimilifu wa injili yangu, na kutakaswa, nitauzuia mkono wangu katika hukumu.

19 Kwa hivyo, nenda, ukipaza sauti kubwa, ukisema: Ufalme wa mbingu u karibu; paza sauti, ukisema: Hosana! libarikiwe jina la Mungu Aliye Juu Sana.

20 Nenda na ukabatize kwa maji, ukiitengeneza njia mbele ya uso wangu kwa ajili ya wakati wa ujio wangu;

21 Kwani wakati umekaribia; siku wala saa hakuna ajuaye; bali hakika yaja.

22 Na yeye ayapokeaye mambo haya anipokea Mimi; na watakusanyika kwangu sasa na hata milele.

23 Na tena, na itakuwa kwamba juu ya wote utakaowabatiza kwa maji, utawawekea mikono yako, na watapokea kipawa cha Roho Mtakatifu, na watatazamia ishara za ujio wangu, na watanijua.

24 Tazama, naja haraka. Hivyo ndivyo. Amina.