2018
Sala: Ufunguo wa Ushuhuda na Urejesho
April 2018


Sala :Ufunguo wa Ushuhuda na Urejesho

Kutoka katika hotuba ya mkutano mkuu wa Oktoba 2003.

Fuata mfano wa Joseph Smith na mpangilio wa Urejesho. Geukia maandiko. Piga magoti usali. Omba kwa imani. Msikilize Roho Mtakatifu.

Picha
clasped hands

Picha kutoka Getty Images

Kama viongozi wa Kanisa, mara nyingi tunaulizwa, “Je, ni kwa jinsi gani ninapokea ushuhuda wa injili ya urejesho ya Yesu Kristo?

Kupata ushuhuda na kuongoka huanza kwa kujifunza na sala, kisha kuishi injili kwa uvumilivu na jitihada na kumualika na kumsubiri Roho. Maisha ya Joseph Smith na mpangilio wa Urejesho ni mifano mizuri ya mchakato huu. Wakati [Nina shiriki nanyi] … matukio ya Urejesho, tafuta hatua zinazotupeleka kwenye ushuhuda.

Mkanganyiko Mkubwa

Joseph Smith alizaliwa mnamo Desemba 23, 1805, huko Sharon, Vermont, Marekani. Alikuja kwenye familia ambayo ilisali na kujifunza Biblia. Katika ujana wake, alivutiwa na dini na kugundua “mkanganyiko mkubwa” juu ya mafundisho ya Kristo, pamoja na “kuhani akibishana dhidi ya kuhani, na muongofu dhidi ya muongofu” (Joseph Smith—Historia 1:6).

Mkanganyiko huu … ulianza karne kadhaa kabla katika kile kilichokuwa kimeitwa Ukengeufu Mkuu. Siku ya Bwana “haiji,” alisema Mtume Paulo, “usipokuja kwanza ule ukengeufu” (2 Wathesalonike 2:3).

Miongo michache baada ya Ufufuko wa Kristo, Mitume Wake waliuawa, mafundisho Yake yalichafuliwa, na ukuhani uliondolewa duniani. Lakini Paulo, akiona siku yetu, alitoa unabii “kwamba kipindi cha mwongozo wa Mungu cha utimilifu wa nyakati [Mungu ange] vijumlisha vitu vyote katika Kristo” (Waefeso 1:10). Angerejesha tena Kanisa la kweli la Kristo duniani. …

Joseph Anapata Jibu

Joseph … , katika umri wa miaka 14, alijikuta akinaswa katika “mkanganyiko wa maoni ya [kidini].” Mara nyingi alijiuliza mwenyewe, “Kama lolote kati ya [makanisa haya] ni sahihi, ni lipi, na nitajuaje?” Joseph Smith—Historia ya 1:10.

Joseph aligeukia Biblia kupata majibu. “Lakini mtu wa kwenu akipungukiwa na hekima,” alisoma katika waraka wa Yakobo, “na aombe dua kwa Mungu, awapaye wote, kwa ukarimu, wala hakemei; naye atapewa” (Yakobo 1:5).

Picha
joseph praying

Utondoti wa kina kutoka Matamanio ya Moyo Wangu II na Walter Rane

Kufuatia maelekezo ya Yakobo, Joseph alienda kwenye kijisitu karibu na nyumbani kwao na alisali. Alipokuwa akimlilia Mungu, “nguzo ya mwanga … ilitokea,” yenye mng’aro kuliko jua la mchana, na “Viumbe wawili” walitokea. “Mmoja wao aliongea … , akimwita [Joseph] kwa jina na kusema, huku akimwonyesha yule mwingine—Huyu ni Mwanangu Mpendwa. Msikilize Yeye!” (Joseph Smith—Historia ya 1:16–17).

Mungu Baba na Mwanawe, Yesu Kristo, waliongea na Joseph. Walijibu swali lake. Walimfundisha kwamba Kanisa la kweli la Kristo lilikuwa limetoweka duniani. Joseph alijifunza kwamba hawa washirika wa Uungu walikuwa ni viumbe tofauti na dhahiri, Walimjua yeye kwa jina, na Walikuwa tayari kujibu sala zake. Mbingu zilifunguka, giza la ukengeufu lilikuwa limetoweka, na nuru ya injili ilianza kung’ara.

Sawa na Joseph, wengi wetu hujikuta tukitafuta nuru ya ukweli. … Sawa na Joseph, lazima tusome maandiko, kusali, … [kuwa] wanyenyekevu, na [kujifunza] kuonyesha imani.

Moroni na Mabamba ya Dhahabu

Wakati wa miaka mitatu kufuatia Ono lake la Kwanza, Joseph [alisema mara nyingi alihisi kukata tamaa kwa sababu ya udhaifu na mapungufu yake]. Lakini hakupoteza imani au kusahau nguvu ya sala.

Mnamo Septemba 21, 1823, katika umri wa miaka 17, [Joseph] alipiga magoti kuomba “kwa ajili ya msamaha wa dhambi [zake] zote” … na [kujua] hali ya msimamo wake mbele za [Mungu]” (ona Joseph Smith—Historia ya 1:29). Aliposali, mwangaza … ulitokea, ukiongezeka, “mpaka chumba kilipokuwa na mwanga mkali zaidi ya jua la saa sita” (mstari wa 30). Katika mwanga ule alisimama kiumbe aliyevalia joho lenye “weupe mzuri sana” (mstari wa 31). Alimuita Joseph kwa jina na kujitambulisha kama Moroni. Alisema “kwamba Mungu ana kazi kwa ajili ya [Joseph] kufanya” na kumuambia kuhusu kumbukumbu ya kale “iliyoandikwa juu ya mabamba ya dhahabu,” ambayo, yalipotafsiriwa yakawa Kitabu cha Mormoni. Kitabu kilikuwa na kumbukumbu ya utimilifu wa injili. (Ona mstari 33–34.)… Joseph alielekezwa kwenye … kumbukumbu ile, iliyozikwa … [chini ya] Mlima uliokuwa jirani … Kumora.

Siku iliyofuata Joseph aliyapata yale mabamba, lakini muda ulikuwa haujafika wa kuyatoa. Moroni alimpa maelekezo Joseph kukutana naye pale siku kama ile kila mwaka kwa miaka minne iliyofuata (ona mstari 52–53). Joseph alitii. Kila mwaka alikwenda kwenye kilima ambapo Moroni alimpa “maelekezo” (mstari wa 54) kuhusu Urejesho wa Kanisa la Kristo. …

Joseph alipokea yale mabamba mnamo Septemba 22, 1827, katika umri wa miaka 21. Pia alipokea kifaa cha kale kwa ajili ya kutafsiri, kilichoitwa Urimu na Thumimu. Kwa kutumia kitafsiri hiki kitakatifu, pamoja na Roho Mtakatifu, Joseph alianza kazi ya kutafsiri. …

Urejesho Unafunuka

Katika umri wa miaka 23 Joseph alikuwa akitafsiri yale mabamba wakati yeye na [mwandishi wake], Oliver [Cowdery,] walifika kwenye kifungu kinachohusu ubatizo kwa ajili ya ondoleo la dhambi. Walitaka kujua zaidi. Joseph alijua nini cha kufanya.

Mnamo Mei 15,1829, [Joseph na Oliver] walikwenda msituni kumwomba Bwana. Walipokuwa wakisali, Yohana Mbatizaji alitokea “katika wingu la mwanga” (Joseph Smith—Historia 1:68). Yeye … alikuwa amembatiza Mwokozi katika uhai, [na] alishikilia funguo muhimu za ukuhani za kufanya ibada hiyo kwa mamlaka ya Mungu.

… Yohana … aliweka mikono yake juu ya [kichwa cha Joseph na kisha cha Oliver] na kumtunukia Ukuhani wa Haruni juu ya [kila] mmoja wao (ona M&M 13; Joseph Smith—Historia 1:68–69). … Mwishoni mwa Mei au mapema Juni 1829, Ukuhani wa Melkizedeki, au Ukuhani wa juu, ulitolewa kwa Joseph na Oliver na Mitume Petro, Yakobo na Yohana.

Picha
conferring the Aaronic Priesthood

Urejesho wa Ukuhani wa Melkizediki, na Walter Rane

Tafsiri ya Kitabu cha Mormoni pia ilikuwa imemalizika Juni ile, na kitabu kilichapishwa mnamo Machi 26, 1830. … Siku kadhaa baadaye, mnamo Aprili 6, kanisa lilianzishwa rasmi. … Kama ilivyotolewa unabii na Paulo, Kanisa la kale la Kristo, lilikuwa limeanzishwa tena duniani.

Lakini kazi ya Urejesho haikuwa imekwisha. … [Hekalu la Kirtland, hekalu la kwanza kujengwa katika kipindi hiki cha mwongozo wa Mungu,] liliwekwa wakfu … mnamo Machi 27, 1836. Wiki moja baadaye, mnamo Aprili 3, mkutano ulifanywa huko. Kufuatia sala ya dhati na ya kimya, … Bwana Yesu Kristo [aliwatokea Joseph na Oliver.] … Musa, Elia, na Eliya pia walitokea [ndani ya Hekalu la Kirtland] na [kukabidhi funguo za ukuhani] kwa Joseph (ona M&M 110).

Picha
in the Kirtland Temple

Utondoti wa kina kutoka Yesu Kristo anawatokea Nabii Joseph Smith na Oliver Cowdery, na Walter Rane

Mpangilio kwa ajili Yetu Sisi Kuufuata

Wakina kaka na wakina dada, je, tunauona mpangilio huu? Kila tukio kuu la Urejesho—Ono la Kwanza, kutokea kwa Moroni na ujio wa Kitabu cha Mormoni, urejesho wa ukuhani, na kutokea kwa Yesu Kristo [ndani ya] hekalu Lake takatifu—vilitanguliwa na sala. …

[Mara nyingi] nimeusikia ushahidi usiopingika wa Roho wa Mungu, kama moto ukiwaka ndani ya moyo wangu, kwamba injili ya urejesho ni ya kweli. … [Kama hujui vitu hivi mwenyewe,] naomba nipendekeze kuukubali mwaliko uliotolewa na Moroni ndani ya Kitabu cha Mormoni: “Na mtakapopokea vitu hivi, ningewashauri kwamba mngemwuliza Mungu, Baba wa Milele, katika jina la Kristo, ikiwa vitu hivi si vya kweli; na ikiwa mtauliza na moyo wa kweli, na kusudi halisi, mkiwa na imani katika Kristo, ataonyesha ukweli wake kwenu, kwa uwezo wa Roho Mtakatifu. “Na kwa uwezo wa Roho Mtakatifu mtajua ukweli wa vitu vyote.” (Moroni 10:4–5). …

… Fuata mfano wa Joseph Smith na mpangilio wa Urejesho. Geukia maandiko. Piga magoti usali. Omba kwa imani. Msikilize Roho Mtakatifu. … Na katika jina la Yesu Kristo, Ninaahidi, “Kama mta … mwomba [Baba wa Mbinguni] kwa imani, mkiamini kwamba mtapokea, kwa bidii katika kutii amri za [Bwana], kwa kweli vitu hivi vitafanywa vijulikane kwenu” (1 Nefi 15:11).