Miito ya Misheni
Sura ya 3: Somo la 1—Ujumbe wa Urejesho wa Injili ya Yesu Kristo


“Sura ya 3: Somo la 1—Ujumbe wa Urejesho wa Injili ya Yesu Kristo,” Hubiri Injili Yangu: Mwongozo wa Kushiriki Injili ya Yesu Kristo (2023)

“Sura ya 3: Somo la 1,” Hubiri Injili Yangu

Sura ya 3: Somo la 1

Ujumbe wa Urejesho wa Injili ya Yesu Kristo

Picha
Ono la Kwanza

Watu wanaweza kujiuliza

  • Je, Mungu yupo?

  • Ni kwa jinsi gani ninaweza kuhisi kuwa karibu na Mungu?

  • Je, ni kwa jinsi gani ninaweza kujifunza ukweli katika ulimwengu wenye kukanganya?

  • Je, ni kwa jinsi gani dini ingeweza kunisaidia mimi?

  • Je, ni kwa nini kuna makanisa mengi sana?

  • Je, ni kwa nini nina changamoto nyingi sana?

  • Je, ni kwa jinsi gani ninaweza kupata amani katika nyakati za ghasia?

  • Je, ni kwa jinsi gani ninaweza kuwa na furaha zaidi?

  • Je, ni kwa jinsi gani nabii angeweza kuusaidia ulimwengu leo?

Kutoka mwanzo wa ulimwengu, Mungu amefunua injili kwa watoto Wake kupitia manabii. Yeye amefanya hili kupitia Mwanaye, Yesu Kristo. Hapo kale, Yesu alifunua injili kwa manabii kama vile Adamu, Nuhu, Ibrahimu na Musa. Lakini watu wengi waliikataa.

Miaka elfu mbili iliyopita, Yesu Kristo Mwenyewe alifundisha injili Yake na kuanzisha Kanisa Lake. Watu hata hivyo walimkataa Yesu. Punde baada ya kifo Chake, kulikuwa na kukithiri kwa anguko kutoka kwenye ukweli na Kanisa la Bwana. Utimilifu wa injili na mamlaka ya ukuhani havikuwepo tena duniani.

Karne nyingi baadaye, Mungu alimwita nabii mwingine, Joseph Smith. Mungu alirejesha utimilifu wa injili kupitia kwake na kumuidhinisha yeye aanzishe Kanisa la Yesu Kristo tena.

Kuwa na utimilifu wa injili ya Yesu Kristo duniani ni mojawapo ya baraka kubwa ya siku yetu. Injili hutusaidia sisi tujibu maswali ya kuchunguza sana ya maisha. Manabii walio hai wanatuongoza kupitia nyakati za changamoto. Mamlaka ya ukuhani wa Mungu kwa mara nyingine tena yapo duniani kuwabariki watoto Wake.

Picha
wamisionari wakiifundisha familia

Mapendekezo kwa ajili ya Kufundisha

Sehemu hii hutoa sampuli ya muhtasari wa kukusaidia ujiandae kufundisha. Pia inajumuisha mifano ya maswali na mialiko unayoweza kutumia.

Unapojiandaa kufundisha, kwa sala fikiria hali na mahitaji ya kiroho ya kila mtu. Amua kile kitakachokuwa cha msaada sana kufundisha. Jiandae kuelezea maneno ambayo watu wanawezakuwa hawayaelewi. Panga kulingana na muda utakaokuwa nao, ukikumbuka kufanya masomo yawe mafupi.

Chagua maandiko ya kutumia unapofundisha. Kipengele cha “Msingi wa Mafundisho” hujumuisha maandiko mengi yenye msaada.

Fikiria ni maswali gani ya kuuliza wakati unapofundisha. Panga mialiko ya kutoa ambayo itamtia moyo mtu kutenda.

Sisitiza baraka zilizoahidiwa za Mungu, na shiriki ushuhuda wako wa kile unachofundisha.

Kile Ambacho Ungeweza Kuwafundisha Watu kwa dakika 15–25

Chagua moja au zaidi ya kanuni zifuatazo za kufundisha: Msingi wa mafundisho kwa kila kanuni umetolewa baada ya muhtasari huu.

Mungu ni Baba Yetu wa Mbinguni Mwenye Upendo

  • Mungu ni Baba yetu wa Mbinguni, na sisi ni watoto Wake. Yeye alituumba sisi kwa mfano Wake.

  • Mungu anatujua sisi binafsi na anatupenda.

  • Mungu ana mwili mkamilifu, mtukufu, wa nyama na mifupa.

  • Mungu anataka kutubariki kwa amani na utimilifu wa shangwe ambayo itadumu milele.

  • Kwa sababu Mungu anatupenda, Yeye alimtuma Mwanaye, Yesu Kristo, ili atukomboe kutokana na dhambi na kifo.

Mungu Hufunua Injili kupitia Manabii katika Kila Kipindi

  • Mungu huwaita manabii wawe wawakilishi Wake duniani.

  • Hapo kale, Mungu aliwaita manabii kama vile Adamu, Nuhu, Ibrahimu na Musa.

  • Nabii aliye hai hupokea ufunuo kutoka kwa Mungu ili kutufundisha na kutuongoza leo.

Huduma ya Duniani ya Yesu Kristo na Upatanisho

  • Yesu Kristo ni Mwana wa Mungu.

  • Wakati wa huduma Yake duniani, Yesu alifundisha injili Yake na kuanzisha Kanisa Lake.

  • Yesu aliwaita Mitume kumi na wawili na kuwapatia mamlaka ya kuongoza Kanisa Lake.

  • Mwisho wa maisha Yake, Yesu alilipa adhabu kwa ajili ya dhambi zetu kwa kuteseka kwake katika Bustani ya Gethsemane na wakati wa Kusulubiwa. Baada ya kifo cha Yesu, Yeye alifufuka.

  • Kwa sababu ya dhabihu yaYesu ya kulipia dhambi, sisi tunaweza kusamehewa na kutakaswa dhambi zetu pale tunapotubu. Hii hutuletea amani na kufanya iwezekane kwa sisi kurudi katika uwepo wa Mungu na kupokea utimilifu wa shangwe.

  • Kwa sababu ya Ufufuko wa Yesu, sisi sote tutafufuka baada ya kufa. Hii inamaanisha kwamba roho na mwili wa kila mtu vitaunganika tena na kuishi milele.

Ukengeufu

  • Baada ya Mitume wa Yesu kufa, kulikuwa na kukithiri kwa ukengeufu kutoka kwenye injili na Kanisa la Yesu Kristo.

  • Katika wakati huu, watu walibadilisha mafundisho mengi ya injili. Watu pia walibadili ibada za ukuhani, kama vile ubatizo. Mamlaka ya ukuhani na Kanisa ambalo Yesu alikuwa amelianzisha havikuwepo tena duniani.

Urejesho wa Injili ya Yesu Kristo kupitia Joseph Smith

  • Joseph alitaka kujua ni kanisa lipi lilikuwa kanisa la Mungu la kweli ili aweze kujiunga nalo. Baba wa Mbinguni na Yesu Kristo walimtokea Yeye mnamo mwaka 1820. Tukio hili linaitwa Ono la Kwanza.

  • Mungu alimwita Joseph Smith kuwa nabii, kama vile Yeye alivyokuwa amewaita manabii katika nyakati za kale.

  • Injili ya Yesu Kristo ilirejeshwa kupitia Nabii Joseph Smith.

  • Wajumbe wengine wa mbinguni walirejesha ukuhani, na Joseph aliidhinishwa kuratibu Kanisa la Yesu Kristo.

  • Yesu Kristo anaendelea kuongoza Kanisa Lake leo kupitia manabii na mitume walio hai.

Kitabu cha Mormoni: Ushuhuda Mwingine wa Yesu Kristo

  • Kitabu cha Mormoni ni juzuu ya maandiko iliyoandikwa nyakati za kale na manabii katika Amerika. Joseph Smith alikitafsiri kwa kipawa na uwezo wa Mungu.

  • Pamoja na Biblia, Kitabu cha Mormoni hutoa ushahidi wa huduma ya Yesu, mafundisho Yake, na misheni Yake kama Mwokozi wetu.

  • Tunaweza kusogea karibu na Mungu kwa kusoma Kitabu cha Mormoni na kuishi kwa maagizo yake.

  • Tunaweza kujua kwamba Kitabu cha Mormoni ni neno la Mungu kwa kukisoma, kukitafakari, na kusali kukihusu. Mchakato huu pia utatusaidia tujue kwamba Joseph Smith alikuwa nabii.

Sali ili Ujue Ukweli kupitia Roho Mtakatifu

  • Sala ni mawasiliano ya pande mbili kati ya Mungu na watoto Wake.

  • Kupitia sala ya dhati, tunaweza kujua kwamba ujumbe wa Urejesho wa Injili ya Yesu Kristo ni wa kweli.

  • Tunaposali, Roho Mtakatifu hutufundisha na kuthibitisha ukweli kwetu.

Picha
wamisionari wakiwafundisha wavulana

Maswali Ambayo Ungeweza Kuwauliza Watu

Maswali yafuatayo ni mifano ya kile ambacho ungeweza kuwauliza watu. Maswali haya yanaweza kukusaidia uwe na mazungumzo ya maana na uelewe mahitaji ya mtu na mtazamo wake.

  • Unaamini nini kuhusu Mungu?

  • Ni jinsi gani kuhisi kuwa karibu na Mungu kungeweza kukusaidia?

  • Unajua nini kuhusu Yesu Kristo? Jinsi gani maisha Yake na mafundisho Yake vimekushawishi?

  • Jinsi gani unapata majibu ya kuaminika katika ulimwengu wenye kukanganya?

  • Jinsi gani ingekuwa yenye kusaidia kujua kwamba kuna nabii aliye hai duniani leo?

  • Je, umewahi kusikia kuhusu Kitabu cha Mormoni? Tunaweza kushiriki kwa nini Kitabu cha Mormoni ni muhimu?

  • Je, ungeweza kushiriki imani yako kuhusu sala? Tunaweza kushiriki imani yetu kuhusu sala?

Mialiko Unayoweza Kuitoa

  • Je, utamuuliza Mungu katika sala ili kujua kwamba kile ambacho tumefundisha ni cha kweli? (Ona “Umaizi wa Kufundisha: Sala” katika sehemu ya mwisho ya somo hili.)

  • Je, utahudhuria kanisani Jumapili hii ili kujifunza zaidi kuhusu kile ambacho tumefundisha?

  • Je, utasoma Kitabu cha Mormoni na kusali ili ujue kwamba ni neno la Mungu? (Unaweza kupendekeza sura au mistari mahususi.)

  • Je, utafuata mfano wa Yesu kwa kubatizwa? (Ona “Mwaliko wa Kubatizwa na Kuthibitishwa,” ambao punde tu unafuatia somo hili.)

  • Je, tupange muda kwa ajili ya matembezi yetu yajayo?

Msingi wa Mafundisho

Sehemu hii inatoa mafundisho na maandiko kwa ajili yako kujifunza kuimarisha ufahamu wako na ushuhuda wako wa injili na kukusaidia ufundishe.

Picha
familia

Mungu ni Baba Yetu wa Mbinguni Mwenye Upendo

Mungu ni Baba yetu wa Mbinguni, na sisi ni watoto Wake. Alituumba sisi kwa mfano Wake. Yeye ana mwili uliotukuka, Mkamilifu “mwili wa nyama na mifupa wenye kushikika kama wa mwanadamu” (Mafundisho na Maagano 130: 22).

Mungu anatujua binafsi, na Yeye anatupenda sana kuliko tunavyoweza kuelewa. Yeye anaelewa majaribu yetu, huzuni, na udhaifu wetu, na Yeye hutoa msaada kupitia hayo. Yeye hufurahia maendeleo yetu na atatusaidia tufanye chaguzi sahihi. Yeye anataka kuwasiliana nasi, na tunaweza kuwasiliana Naye kupitia sala.

Mungu ametupatia sisi uzoefu huu katika dunia hii ili tuweze kujifunza na kukua, na kuwa zaidi kama Yeye. Kwa upendo kamili, Yeye anatutaka sisi turudi Kwake baada ya kufa. Hata hivyo, hatuwezi kufanya hivi sisi wenyewe. Kwa sababu Mungu anatupenda, Yeye alimtuma Mwanaye, Yesu Kristo, ili atukomboe. “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanaye wa pekee, … ili ulimwengu kupitia yeye uweze kuokolewa” (Yohana 3:16–17).

Mungu anataka kutubariki kwa amani na utimilifu wa shangwe ambayo itadumu milele. Yeye ametoa mpango ambao hutupatia sisi fursa ya kupokea baraka hizi. Mpango huu unaitwa mpango wa wokovu (ona somo la 2).

Kujifunza Maandiko

Jifunze Zaidi kuhusu Kanuni Hii

Picha
Musa na Mbao za Mawe, na Jerry Harston

Mungu Hufunua Injili kupitia Manabii katika Kila Kipindi

Manabii ni Wawakilishi wa Mungu Duniani

Njia moja muhimu ambayo Mungu huonesha upendo Wake kwetu ni kwa kuwaita manabii na kuwapa mamlaka ya ukuhani, na kuwavuvia wazungumze kwa niaba Yake. Manabii ni wawakilishi wa Mungu duniani. Nabii wa Agano la Kale Amosi aliandika kwamba, “Bwana Mungu hatafanya neno lolote, bila kuwafunulia watumishi wake manabii siri yake” (Amosi 3:7). Baadhi ya baraka tunazopokea kutoka kwa manabii walio hai zimeorodheshwa hapa chini.

Mashahidi wa Yesu Kristo. Manabii ni mashahidi maalum wa Yesu Kristo, wanaoshuhudia juu Yake kama Mwokozi na Mkombozi wetu.

Mafundisho. Manabii wanapokea maelekezo kutoka kwa Mungu ili kutusaidia tubainishe ukweli kutoka kwenye makosa. Wanatufundisha sisi kutii amri za Mungu na kutubu pale tunapokosea. Wanashutumu dhambi na kuonya juu ya matokeo yake.

Mafundisho ya manabii yanatuinua kumwelekea Mungu na yanatusaidia tupokee baraka Yeye anazotamani kwa ajili yetu. Usalama wetu mkuu upo katika kulifuata neno la Bwana lililotolewa kupitia manabii wake.

Mamlaka ya Ukuhani. Nabii wa sasa ndiye kiongozi msimamizi anaeshikilia ukuhani duniani. Ukuhani ni mamlaka na nguvu za Mungu. Nabii ana mamlaka ya kuzungumza na kutenda katika jina la Mungu kwa ajili ya wokovu wa watoto Wake.

Mwongozo wa Kanisa. Kanisa la Yesu Kristo limejengwa kwenye msingi wa manabii na mitume (ona Waefeso 2:19–20; 4:11–14).

Manabii katika Nyakati za Kale

Adamu alikuwa nabii wa kwanza hapa duniani. Mungu alifunua injili ya Yesu Kristo kwake na kumpatia yeye mamlaka ya ukuhani. Adamu na Hawa waliwafundisha watoto wao kweli hizi na kuwahimiza wakuze imani na kuishi injili.

Hatimaye uzao wa Adamu na Hawa uliasi na kugeuka mbali na injili. Hii ilisababisha hali inayoitwa ukengeufu, au kuanguka. Wakati ukengeufu uliokithiri unapojitokeza, Mungu huondoa mamlaka Yake ya Ukuhani, ambayo ni muhimu katika kufundisha na kutekeleza ibada za injili.

Kumbukumbu za Agano la Kale zina mifano mingi ya ukengeufu uliokithiri. Ili kuhitimisha vipindi hivi, Mungu aliwafikia watoto Wake kwa kumwita nabii mwingine. Yeye alifunua kweli za injili upya kwa manabii hawa na kuwapatia mamlaka ya ukuhani. Baadhi ya manabii hawa walikuwa ni Nuhu, Ibrahimu, na Musa. Cha kuhuzunisha, kwa mpangilio wa kujirudia baada ya muda, watu hatimaye waliwakataa manabii na wakaanguka.

Kujifunza Maandiko

Jifunze Zaidi kuhusu Kanuni Hii

  • Mwongozo wa Maandiko: “Nabii

  • Mada za Injili: “Manabii,” “Urejesho wa Kanisa

Picha
Ee Baba Yangu, na Simon Dewey

Huduma ya Yesu Kristo Duniani na Upatanisho

Yesu Kristo ni Mwana wa Mungu. Yesu na Upatanisho Wake ni kiini cha mpango wa Mungu kwa ajili yetu. Upatanisho Wake unajumuisha kuteseka Kwake katika Bustani ya Gethsemane na kuteseka Kwake na kifo kwenye msalaba, na Ufufuko Wake.

Tangu wakati wa Adamu na Hawa, watu walitegemea ujio wa Yesu Kristo kama Mwokozi na Mkombozi wetu. Baba wa Mbinguni alimtuma Yesu duniani zaidi ya miaka 2,000 iliyopita.

Yesu aliishi maisha ya ukamilfu bila dhambi. Yeye alifundisha injili Yake na kuanzisha Kanisa Lake. Yeye aliwaita Mitume kumi na wawili na akawapa mamlaka ya ukuhani ya kufundisha katika jina Lake na kufanya ibada takatifu, kama vile ubatizo. Yeye aliwapa mamlaka ya kuongoza Kanisa Lake.

Mwisho wa maisha Yake, Yesu alifanya upatanisho kwa ajili ya dhambi zetu kwa kuteseka Kwake Gethsemane na wakati wa Kusulubiwa Kwake. Kwa sababu ya upatanisho wa Yesu, tunaweza kusafishwa dhambi zetu pale tunapotubu. Hii hufanya iwezekane kwa sisi kurudi katika uwepo wa Mungu na kupokea utimilifu wa shangwe.

Baada ya Yesu kusulubiwa, Yeye alifufuka, akapata ushindi juu ya kifo kwa nguvu za Baba wa Mbinguni. Kwa sababu ya Ufufuko wa Yesu, sisi sote tutafufuka baada ya kufa. Hii inamaanisha kwamba roho na mwili wa kila mtu vitaunganika tena, na kila mmoja wetu ataishi milele katika mwili mkamilifu, uliofufuka. (Ona “(Upatanisho wa Yesu Kristo” katika somo la 2.)

Picha
Nabii Joseph Smith

Nabii Joseph Smith alifundisha, “Kanuni za msingi za dini yetu ni ushuhuda wa Mitume na Manabii, kuhusu Yesu Kristo, kwamba Alikufa, Akazikwa, na Akafufuka tena siku ya tatu, na kupaa mbinguni; na mambo yote mengine ambayo yanahusiana na dini yetu ni viambatisho vyake” (Teachings of Presidents of the Church: Joseph Smith [2007], 49).

Kujifunza Maandiko

Jifunze Zaidi kuhusu Kanuni Hii

Kuanguka

Baada ya kifo cha Yesu Kristo, Mitume Wake walitaka kuweka mafundisho ya Kristo yakiwa safi na kudumisha utaratibu katika Kanisa. Hata hivyo, waumini wengi wa Kanisa waliwaasi Mitume na kutoka kwenye mafundisho ambayo Yesu alikuwa ameyafundisha.

Baada ya Mitume kuuwawa, kulikuwa na kukithiri kwa kuanguka kutoka kwenye injili na Kanisa la Yesu Kristo. Kuanguka huku wakati mwingine kunajulikana kama Ukengeufu Mkuu. Kwa sababu ya ukengeufu, Mungu aliondoa mamlaka ya ukuhani kutoka duniani. Upotevu huu ulijumuisha mamlaka yaliyohitajika kuelekeza Kanisa. Kwa matokeo haya, Kanisa ambalo Yesu alikuwa amelianzisha halikuwapo tena duniani.

Katika wakati huu, watu walibadilisha mafundisho mengi ya injili. Wingi wa elimu kuhusu uhalisia wa kweli wa Baba wa Mbinguni, Yesu Kristo, na Roho Mtakatifu ulipotoshwa au kupotea. Watu pia walibadili ibada za ukuhani, kama vile ubatizo.

Karne nyingi baadaye, wanaume na wanawake wenye kutafuta ukweli walijaribu kurekebisha mafundisho na desturi ambazo zilikuwa zimebadilishwa. Walitafuta nuru kuu ya kiroho, na baadhi yao wakazungumza juu ya haja ya urejesho wa ukweli. Juhudi zao zilielekeza kwenye kuanzishwa kwa makanisa mengi.

Kipindi hiki kilileta ongezeko la msisitizo wa uhuru wa dini, ambao ulifungua njia ya urejesho wa ukweli na mamlaka kutoka kwa Mungu.

Manabii na Mitume walitabiri kuhusu ukengeufu (ona 2 Wathesalonike 2:1–3). Pia walikuwa wametabiri kwamba injili na Kanisa la Yesu Kristo vingerejeshwa duniani (ona Matendo ya Mitume 3:20–21). Kama kusingekuwepo na kuanguka, urejesho haungehitajika.

Kujifunza Maandiko

Jifunze Zaidi kuhusu Kanuni Hii

Urejesho wa Injili ya Yesu Kristo kupitia Joseph Smith.

Ono la Kwanza na Wito wa Joseph Smith kama Nabii

Wakati wa karne nyingi ambapo utimilifu wa injili ya Yesu Kristo haukuwepo duniani, Baba wa Mbinguni aliendelea kuwafikia watoto Wake. Baada ya muda, Yeye aliandaa njia ili waweze kubarikiwa tena kwa kuwa na utimilifu wa injili Yake. Wakati hali ilipokuwa sahihi, Yeye alimwita Joseph Smith kama nabii ambaye kupitia kwake injili na Kanisa la Yesu Kristo vingerejeshwa.

Joseph Smith aliishi katika Marekani ya mashariki wakati wa msisimko mkubwa wa kidini. Wanafamilia yake walikuwa washika dini sana na walitafuta ukweli. Makanisa mengi yalidai kuwa na ukweli, na Joseph alitamani kujua ni lipi lilikuwa sahihi (ona Joseph Smith—Historia ya 1:18). Biblia inafundisha kuwa kuna “Bwana mmoja, imani moja, ubatizo mmoja” (Waefeso 4:5). Joseph alihudhuria makanisa tofauti, lakini alibakia kukanganyikiwa kuhusu lipi ambalo angejiunga nalo. Yeye baadae alisema:

“Mchafuko na mzozo ulikuwa mkubwa miongoni mwa madhehebu mbalimbali, kiasi kwamba ilikuwa vigumu kwa mtu kijana mdogo kama mimi nilivyokuwa … kuweza kufikia uamuzi wa nani ni sahihi na nani si sahihi. …

“Katikati ya vita hivi vya maneno na makelele ya maoni, daima nilijisemea mimi mwenyewe: Ni nini cha kufanya? Nani kati yao hawa wote aliye sahihi; au, je, wote si sahihi? Kama yeyote kati yao yu sahihi, ni yupi, na nitajuaje?” (Joseph Smith—Historia ya 1:8, 10).

Kama vile watu wengi, Joseph Smith pia alikuwa na maswali kuhusu wokovu wa nafsi yake. Alitaka kusamehewa dhambi zake na kuwa msafi mbele ya Mungu. Alipokuwa akitafuta ukweli miongoni kwa makanisa tofauti, alisoma katika Biblia, “Lakini mtu wa kwenu akipungukiwa na hekima, na aombe dua kwa Mungu, awapaye wote kwa ukarimu, wala hakemei; naye atapewa” (Yakobo 1:5).

Kwa sababu ya maneno haya, Joseph aliamua kumuomba Mungu juu ya nini anapaswa kufanya. Katika majira ya kuchipua ya 1820 alienda kwenye kijisitu cha miti karibu na nyumbani kwao na akapiga magoti katika sala. Kuna simulizi nne za ono ambalo lilifuatia, zilizoandikwa na Joseph Smith au waandishi chini ya maelekezo yake (ona Insha za Mada za Injili, “Simulizi za Ono la Kwanza”). Katika simulizi zilizotambuliwa kama maandiko, yeye alielezea uzoefu wake kama ifuatavyo:

Picha
Ono la Kwanza, na Linda Christensen na Michael Malm

“Niliona nguzo ya mwanga juu ya kichwa changu, ambao ulikuwa ni mng’aro uliozidi mwangaza wa jua, ambao ulishuka taratibu hadi ukatua juu yangu. … Mwanga ulipotua juu yangu nikawaona Viumbe wawili, ambao mng’aro na utukufu wao wapita maelezo yote, wakiwa wamesimama juu yangu angani. Mmoja wao akaniambia, akiniita mimi kwa jina langu na kusema, huku akimwonyesha yule mwingine—Huyu ni Mwanangu Mpendwa. Msikilize Yeye!” (Joseph Smith—Historia ya 1:16–17).

Katika ono hili, Mungu Baba na Mwanaye, Yesu Kristo, walimtokea Joseph Smith. Mwokozi alimwambia asijiunge na lolote kati ya makanisa hayo.

Katika simulizi nyingine ya ono hili, Joseph alishiriki kwamba Mwokozi pia alimwambia: “Dhambi zako zimesamehewa. … Tazama, mimi ndimi Bwana wa utukufu. Nilisulubiwa kwa ajili ya ulimwengu ili kwamba wale wote wanaoamini katika jina langu waweze kupata uzima wa Milele.

Baada ya ono hili, Joseph alitafakari, “Nafsi yangu ilijawa na upendo, na kwa siku nyingi ningeweza kufurahi kwa shangwe kuu na Bwana alikuwa pamoja nami” (Joseph Smith—Historia ya, karibu na Msimu wa Joto, mwaka 1832, 3, josephsmithpapers.org; tahajia na vituo vya uandishi ni vya kisasa).

Kupitia ono hili, Joseph Smith alikuwa shahidi wa Yesu Kristo na alijifunza kweli muhimu kuhusu Uungu. Kwa mfano, alijifunza kwamba Baba wa Mbinguni na Yesu Kristo ni viumbe wawili tofauti. Wakati Walipomwita kwa jina, alijifunza kwamba Wao walimjua yeye binafsi. Wakati Joseph alipoambiwa kwamba amesamehewa, alijifunza kwamba Mungu ni mwenye huruma. Uzoefu huu ulimjaza furaha.

Kama vile Mungu alivyofanya kwa manabii wengi waliopita, Yeye alimwita Joseph Smith kuwa nabii ambaye kupitia kwake utimilifu wa injili ungerejeshwa duniani. Urejesho huu ungewasaidia watoto wa Mungu wapate furaha katika ulimwengu huu na uzima wa milele katika ulimwengu ujao—yote kupitia Yesu Kristo.

Urejesho wa Ukuhani na Funguo za Ukuhani

Picha
Juu Yenu Ninyi Watumishi Wenzangu, na Linda Curley Christensen na Michael Malm

Baada ya kutokea kwa Baba na Mwana, wajumbe wengine wa mbinguni walitumwa kwa Joseph Smith na mshirika wake Oliver Cowdery. Yohana Mbatizaji alitokea kama kiumbe aliyefufuka na kuwatunukia Ukuhani wa Haruni na funguo zake. Ukuhani wa Haruni unajumuisha mamlaka ya kubatiza.

Picha
Sauti ya Petro, Yakobo, na Yohana, na Linda Welden C. Andersen

Punde baadaye, Petro, Yakobo, na Yohana—watatu miongoni mwa Mitume halisi wa Kristo—walitokea kama viumbe waliofufuka na kutunukia Ukuhani wa Melkizedeki na funguo zake kwa Joseph Smith na Oliver Cowdery. Ukuhani huu ni ule ule ambao Kristo aliwapa Mitume Wake wa kale.

Picha
Image of Moses Elias and Elijah descending into the Kirtland temple and appearing to Joseph Smith.

Katika Hekalu la Kirtland, Musa, Elia, na Eliya walimtokea Joseph Smith na Oliver Cowdery na kuwakabidhi wao mamlaka zaidi na funguo za ukuhani zilizo muhimu kukamilisha kazi ya Mungu katika siku za mwisho. Musa alikabidhi funguo za kuikusanya Israeli. Elia alikabidhi kipindi cha injili cha Ibrahimu. Eliya alikabidhi funguo za kunganisha. (Ona Mafundisho na Maagano 110:11–16; ona pia Kitabu cha Maelezo ya Jumla, 3.1.)

Kuanzishwa kwa Kanisa

Joseph Smith alielekezwa kuanzisha tena Kanisa la Yesu Kristo ulimwenguni. Kupitia yeye, Yesu Kristo aliwaita Mitume kumi na wawili.

Manabii katika nyakati za biblia walirejelea kwenye wakati ambao sisi tunaishi au siku za mwisho. Ni wakati punde kabla ya Ujio wa Pili wa Yesu Kristo. Hiyo ndiyo sababu Kanisa linaitwa Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho (ona Mafundisho na Maagano 115: 3–4; ona pia 3 Nefi 27:3–8).

Manabii na Mitume Walio Hai Leo

Kama vile Yesu alivyowaita Mitume wakati wa huduma Yake duniani ili waongoze Kanisa Lake, Yeye amewaita Mitume waliongoze Kanisa Lake leo. Urais wa Kwanza na Akidi ya Mitume Kumi na Wawili ni manabii, waonaji na wafunuzi.

Ni mtume Mkubwa katika utume ndiye pekee anaitwa nabii kwa sababu yeye anaongoza Kanisa lote na kwa kipekee ameidhinishwa kuzungumza kwa niaba ya Bwana. Yeye ndiye mrithi aliyedhinishwa wa Joseph Smith. Yeye na Mitume wa sasa hufuatisha mstari wa mamlaka yao hadi kwa Yesu Kristo kwa mnyororo usiokatika wa kutawazwa kwao ambao ulianza wakati Joseph Smith alipotawazwa chini ya mikono ya wajumbe wa mbinguni.

Kujifunza Maandiko

Jifunze Zaidi kuhusu Kanuni Hii

Kitabu cha Mormoni: Ushuhuda Mwingine wa Yesu Kristo

Kitabu cha Mormoni ni juzuu ya kale ya maandiko matakatifu kama vile Biblia. Biblia ni ushahidi mmoja wa Yesu Kristo, na Kitabu cha Mormoni ni ushahidi wa pili wa huduma Yake, mafundisho Yake, na misheni Yake kama Mwokozi wetu.

Joseph Smith alielekezwa na mjumbe wa mbinguni anayeitwa Moroni kwenye kilima ambapo kumbukumbu za kale zilizikwa kwa karne nyingi. Kumbukumbu hii, ilichorwa kwenye mabamba ya dhahabu (mabamba membamba ya metali), yaliyokuwa na maandishi ya manabii kuhusu uhusiano wa Mungu na baadhi ya wakazi wa kale wa mabara ya Amerika. Joseph Smith alitafsiri kumbukumbu hii kwa kipawa na uwezo wa Mungu.

Manabii katika Kitabu cha Mormoni walijua kuhusu misheni ya Yesu Kristo na walifundisha injili Yake. Baada ya Yesu kufufuka, Yeye mwenyewe aliwatokea watu hawa na kuwahudumia. Yeye aliwafundisha na kuanzisha Kanisa Lake.

Kitabu cha Mormoni kinatusaidia tusonge karibu na Mungu kadiri tunavyojifunza, kuelewa, na kutumia mafundisho yake. Nabii Joseph Smith alisema kwamba “mwanamume [au mwanamke] angemkaribia zaidi Mungu kwa kufuata mafunzo yake, kuliko kitabu kingine chochote”(Mafundisho: Joseph Smith64).

Picha
mwanamume akisoma

Kujua kwamba Kitabu cha Mormoni ni neno la Mungu, tunahitaji kukisoma, kutafakari, na kusali kuhusu kitabu hiki. Nabii wa Kitabu cha Mormoni aliahidi kwamba Mungu angefunua ukweli wa kitabu kwetu pale tunaposali kwa moyo kwa dhati, kwa kusudi halisi, na kwa imani katika Kristo (ona Moroni 10:3–5). Kujifunza Kitabu cha Mormoni ni muhimu kwa ajili ya uongofu wa kudumu.

Tunaposoma Kitabu cha Mormoni na kusali kuhusu kitabu hiki, tutajifunza kweli kuhusu Yesu Kristo ambazo zitabariki maisha yetu. Pia tutakuja kujua kwamba Joseph Smith alikuwa nabii wa Mungu na kwamba injili na Kanisa la Yesu Kristo vimerejeshwa kupitia yeye.

Picha
Rais Russell M. Nelson

“Ninaahidi kwamba unapojifunza kwa sala Kitabu cha Mormoni kila siku, utafanya maamuzi mazuri zaidi—kila siku. Ninaahidi kwamba unapotafakari kile unachojifunza, madirisha ya mbinguni yatafunguka na utapokea majibu ya maswali yako na mwongozo kwa ajili ya maisha yako mwenyewe. Ninaahidi kwamba unapozama kila siku kwenye Kitabu cha Mormoni, unaweza kuepushwa dhidi ya maovu ya siku” (Russell M.Nelson, “Kitabu cha Mormoni: Je, Maisha Yako Yangekuwaje Bila Hicho?Liahona, Nov. 2017, 62–63).

Kujifunza Maandiko

Jifunze Zaidi kuhusu Kanuni Hii

Picha
mwanamke akisali

Sali ili Ujue Ukweli kupitia Roho Mtakatifu

Kwa sababu Mungu ni Baba yetu, Yeye atatusaidia tutambue ukweli. Tunaweza kujua kwamba ujumbe wa Urejesho wa Injili ya Yesu Kristo ni wa kweli tunaposoma Kitabu cha Mormoni na kusali kwa Mungu. Tunaposali kwa imani na kusudi halisi, Yeye atajibu maswali yetu na kuongoza maisha yetu.

Mungu kwa kawaida hujibu sala zetu kupitia Roho Mtakatifu. Tunaposali, Roho Mtakatifu hutufundisha na kuthibitisha ukweli. Mawasiliano kutoka kwa Roho Mtakatifu yana nguvu sana. Kwa kawaida yanakuja kama hakikisho tulivu kupitia hisia zetu, fikra zetu, na misukumo yetu (ona 1 Wafalme 19:11–12; Helamani 5:30; Mafundisho na Maagano 8:2).

Mafunzo thabiti ya maandiko (hasa Kitabu cha Mormoni), mahudhurio ya mkutano wa sakramenti kila wiki, na sala za dhati vinatusaidia tuhisi nguvu za Roho Mtakatifu na tugundue ukweli.

Kujifunza Maandiko

Jifunze Zaidi kuhusu Kanuni Hii

  • Mwongozo wa Maandiko: “Sala

  • Kamusi ya Biblia: “Sala

  • Mada za Injili: “Sala

Muhtasari Mfupi hadi wa Wastani wa Somo

Muhtasari ufuatao ni sampuli ya kile ambacho ungemfundisha mtu kama una muda mfupi tu. Unapotumia muhtasari huu, chagua kanuni moja au zaidi za kufundisha. Msingi wa mafundisho kwa kila kanuni ulitolewa mapema katika somo hili.

Unapofundisha, uliza maswali na usikilize. Toa mwaliko ambao utawasaidia watu wajifunze jinsi ya kusonga karibu na Mungu. Mwaliko mmoja muhimu ni kwa ajili ya mtu kukutana nanyi tena. Urefu wa somo utategemea maswali unayouliza na usikilizaji unaoufanya.

Picha
wamisionari wakizungumza na mtu

Unachoweza Kuwafundisha Watu kwa Dakika 3–10

  • Mungu ni Baba yetu wa Mbinguni, na Yeye alituumba kwa mfano Wake. Yeye anatujua binafsi na anatupenda. Yeye anataka kutubariki kwa amani na utimilifu wa furaha ambayo itadumu milele.

  • Yesu Kristo ni Mwana wa Mungu. Misheni Yake ilifanya iwezekane kwetu kutakaswa dhambi zetu, kushinda kifo na kupokea uzima wa milele.

  • Mungu huwaita manabii kuwa wawakilishi Wake duniani. Hapo kale, Yeye aliwaita manabii kama vile Adamu, Nuhu, Ibrahimu na Musa. Nabii aliye hai hupokea ufunuo kutoka kwa Mungu ili kutufundisha na kutuongoza leo.

  • Wakati wa huduma Yake duniani, Yeye alianzisha Kanisa Lake. Baada ya Mitume wa Yesu kufa, kulikuwa na kukithiri kwa ukengeufu kutoka kwenye injili na Kanisa la Yesu Kristo. Watu pia walibadili mafundisho mengi ya injili na ibada za ukuhani, kama vile ubatizo.

  • Mungu alimwita Joseph Smith kuwa nabii, kama vile Yeye alivyokuwa amewaita manabii katika nyakati za kale. Baba wa Mbinguni na Yesu walimtokea yeye. Injili ya Yesu Kristo ilirejeshwa kupitia yeye.

  • Kitabu cha Mormoni ni juzuu ya maandiko. Kama vile Biblia, ni ushuhuda mwingine wa Yesu Kristo na hutusaidia tusonge karibu na Mungu pale tunapokisoma na kutumia mafundisho Yake. Joseph Smith alikitafsiri kwa kipawa na uwezo wa Mungu.

  • Kupitia sala ya dhati, tunaweza kuwasiliana na Mungu. Tunaweza kujua kwamba ujumbe wa Urejesho wa Injili ya Yesu Kristo ni wa kweli.