Miito ya Misheni
Sura ya 10: Fundisha Kujenga Imani katika Yesu Kristo


“Sura ya 10: Fundisha Kujenga Imani katika Yesu Kristo,” Hubiri Injili Yangu: Mwongozo wa Kushiriki Injili ya Yesu Kristo (2023)

“Sura ya 10,” Hubiri Injili Yangu

Picha
Mahubiri ya Mlimani, na Harry Anderson

Sura ya 10

Fundisha Kujenga Imani katika Yesu Kristo

Zingatia Hili

  • Ni jinsi gani ninaweza kufundisha kwa njia ya Roho.

  • Ni jinsi gani ninaweza kufundisha kutoka kwenye maandiko?

  • Ni jinsi gani ninapaswa kushiriki ushuhuda wangu wakati ninapofundisha?

  • Ni jinsi gani ninaweza kupanga na kurekebisha ufundishaji wangu ili kukidhi mahitaji ya watu?

  • Ni jinsi gani ninaweza kuuliza maswali mazuri na kuwa msikilizaji mzuri?

  • Ni jinsi gani ninaweza kuwasaidia watu wapate majibu ya maswali yao na wapokee mwongozo na nguvu?

Wewe umeitwa kufundisha injili ya urejesho ya Yesu Kristo kwa watu wengi kadiri watakavyokupokea. Kufundisha ni kiini cha kila kitu unachofanya. Unapomtegemea Bwana kwa ajili ya msaada, Yeye ameahidi:

“Na yeyote awapokeaye ninyi, hapo nitakuwepo pia, kwani nitakwenda mbele ya uso wenu. Nitakuwa mkono wenu wa kuume na wa kushoto, na Roho wangu atakuwa mioyoni mwenu, na malaika zangu watawazingira, ili kuwabeba juu” (Mafundisho na Maagano 84:88).

Sali, jifunze, na fanya mazoezi ili kuboresha uwezo wako wa kufundisha. Tumia kanuni zilizo katika sura hii na katika sura zingine za kitabu hiki. Kwa dhati tafuta kipawa cha kufundisha ili uweze kuwabariki wengine na kumtukuza Mungu. Bwana atakusaidia ufundishe kwa nguvu na mamlaka kadiri unapomtafuta Yeye na kujifunza neno Lake kwa bidii.

Tafuta Kufundisha kama Mwokozi Alivyofundisha.

Wakati wa huduma Yake duniani, Yesu “alikuwa akizunguka … akifundisha … , akihubiri … , na kuponya” (Mathayo 4:23). Yeye alifundisha katika mazingira anuai—katika masinagogi, nyumbani, na barabarani. Alifundisha katika mikusanyiko mikubwa na katika mazungumzo ya faragha. Baadhi ya michangamano Yake yenye nguvu zaidi ilikuwa ya muda mfupi sana au katika mazingira yasiyo ya kawaida. Yeye alifundisha kupitia matendo Yake vile vile kwa maneno Yake.

Mwokozi alimfundisha kila mtu kulingana na mahitaji yake ya kipekee. Kwa mfano, wakati akimhudumia mtu aliyepooza, Yeye alimsamehe dhambi zake na kumponya (ona Marko 2:1–12). Alipokuwa akimhudumia mwanamke ambaye alikuwa amefanya uzinzi, Yeye alimlinda na kumwalika asitendee dhambi tena (ona Yohana 8:2–11). Wakati akizungumza na mtu tajiri ambaye alitamani uzima wa milele, Yeye “alimpenda” licha ya kijana kukataa kupokea mwaliko Wake wa kumfuata (Marko 10:21; ona mstari wa 17–21).

Unaweza kuboresha ufundishaji wako kwa kujifunza jinsi Mwokozi alivyofundisha. Kwa mfano, Yeye alimpenda Baba na wale ambao aliwafundisha. Yeye alikuwa mwenye kusali sana. Yeye alifundisha kutoka kwenye maandiko. Yeye alijiandaa kiroho. Yeye aliuliza maswali yenye mwongozo wa kiungu. Yeye aliwaalika watu watende kwa imani. Yeye alilinganisha kanuni za injili na maisha ya kila siku.

Kutafuta kufundisha kama Mwokozi alivyofundisha ni harakati za maisha yote. Itakuja kwako mstari juu ya mstari kadiri unavyomfuata Yeye (ona 2 Nefi 28:30; Etheri 12:41).

“Tafuta Kulipata Neno Langu”

Ili kufundisha injili ya Yesu Kristo, unahitaji kujua mafundisho na kanuni za msingi. Pia unahitaji ufahamu wa kiroho na uthibitisho wa kweli za injili. Bwana alisema, “Usitafute kulitangaza neno langu, bali kwanza tafuta kulipata neno langu.”

“Kupata” neno la Bwana humaanisha kujifunza na kuliacha lizame kwa kina katika moyo wako. Unapofanya juhudi hii, Yeye aliahidi, “Kisha ulimi wako utalegezwa; halafu, kama unataka, utapata Roho wangu na neno langu, ndiyo, nguvu ya Mungu kwa kuwashawishi wanadamu” (Mafundisho na Maagano 11:21).

Picha
mtu akiweka alama kwenye maandiko

Bwana pia alisema, “yahifadhini katika akili zenu daima maneno ya uzima” (Mafundisho na Maagano 84:85). Kuyahifadhi maneno ya Bwana kutaongeza ufahamu wako na kuimarisha ushuhuda wako. Tamanio lako na uwezo wako wa kufundisha injili pia vitaongezeka. (Ona Yakobo 4:6–7; Alma 32:27–42; 36:26; 37:8–9.)

Kwa maombi yapate na uyahifadhi maneno ya Bwana kwa kujifunza maandiko, maneno ya manabii walio hai, na masomo katika sura ya 3.

Fundisha kwa Roho

Injili ya Yesu Kristo ni “uweza wa Mungu uletao wokovu, kwa kila aaminiye” (Warumi 1:16). Kwa sababu hiyo, ujumbe wa Urejesho wa injili unahitaji kufundishwa kwa nguvu takatifu—uwezo wa Roho Mtakatifu.

Ni muhimu kwamba wewe ukuze ujuzi wa kufundisha. Pia ni muhimu kwamba ujifunze mafundisho na kanuni unazozifundisha. Hata hivyo, unapofundisha kweli za kiroho, hauhitaji kutegemea kimsingi juu ya uwezo na elimu yako mwenyewe.

Kweli za kiroho hufundishwa kwa uwezo wa Roho Mtakatifu. Bwana alisema, “Na Roho atatolewa kwenu kwa sala ya imani; na msipompokea roho msifundishe” (Mafundisho na Maagano 42:14; ona pia Mafundisho na Maagano 50:13–14, 17–22).

Kile Inachomaanisha Kufundisha kwa Roho

Unapofundisha kwa Roho, unasali ili kuwa na nguvu ya Roho Mtakatifu katika ufundishaji wako. Pia unasali ili kwamba watu wapokee kweli hizo kwa Roho. Watu wanaweza kushawishika na baadhi ya kweli hizi, lakini ili kuongolewa, wanahitaji kupata uzoefu wa Roho (ona Mafundisho na Maagano 8:2–3).

Jiandae kuwa chombo ambacho kupitia kwako Roho anaweza kufundisha. Mfikirie Roho Mtakatifu kama mwenza wako katika ufundishaji.

Mtegemee Roho ili akusaidie ujue nini cha kusema. Yeye ataleta mafundisho uliyojifunza katika kumbukumbuku yako. Yeye atakusaidia kupanga na kurekebisha kile unachofundisha kilingane na mahitaji ya watu.

Unapofundisha kwa Roho, Yeye atabeba ujumbe wako hadi mioyoni mwa watu. Yeye atathibitisha ujumbe wako wakati unapotoa ushuhuda wako. Wewe na wale ambao wanapokea kile wewe unachofundisha kwa Roho mtaadilishwa, mtaelewana, na mtafurahi pamoja. (Ona 2 Nefi 33:1; Mafundisho na Maagano 50:13–22).

Picha
Rais Ezra Taft Benson

“Roho ndiyo kitu kimoja muhimu zaidi katika kazi hii. Roho akiwa anakuza wito wako, unaweza kufanya miujiza kwa ajili ya Bwana katika eneo la misheni. Bila Roho, kamwe hautafanikiwa licha ya kipaji na uwezo wako” (Ezra Taft Benson, seminar for new mission presidents, June 25, 1986).

Ahadi ya Wito Wako

Umeitwa na kutawazwa “kuihubiri injili Yangu kwa Roho, hata Mfariji ambaye alitumwa kufundisha ukweli” (Mafundisho na Maagano 50:14). Wakati mwingine unaweza kuhisi kuwa na wasiwasi au kupungukiwa. Pengine una wasiwasi ya kwamba haujui vya kutosha au kwamba hauna uzoefu wa kutosha.

Baba yako wa Mbinguni, ambaye anakujua kikamilifu, alikuita kwa sababu ya kile unachoweza kushiriki kama mfuasi wa kujitolea wa Yesu Kristo. Yeye hatakuacha. Tumaini kwamba Roho atapanua uwezo wako na kukufundisha ukweli huo kwa wale wanaoukubali.

Picha
Mzee Neil L. Andersen

Mzee Neil L. Andersen alisema: “Nilipotafakari changamoto ya misheni, nilihisi kutostahili na sikuwa nimejiandaa. Ninakumbuka nikiomba, ‘Baba wa Mbinguni, ninawezaje kutumikia misheni wakati najua machache tu?” Niliamini katika Kanisa, lakini nilihisi ufahamu wangu wa kiroho ulikuwa mdogo sana. Nilipokuwa nikisali, hisia ilikuja: “Wewe hujui kila kitu, lakini unajua vya kutosha!’ Hakikisho hilo lilinipa ujasiri wa kupiga hatua inayofuata katika eneo la misheni” (“Unajua vya Kutosha,” Liahona, Nov. 2008, 13).

Mwalike Roho Unapoanza Kufundisha

Dakika chache za mwanzo ukiwa na watu ni muhimu sana. Kuwa muwazi na mwenye heshima. Onesha utashi na upendo wa dhati. Tafuta kupata kuaminiwa nao. Njia mojawapo ya kupata kuaminiwa ni wakati watu wanapohisi uwepo wa Roho wanapokuwa pamoja na wewe.

Uliza maswali machache rahisi ili kukusaidia uelewe asili yao na matarajio yao kuhusu matembezi yako. Sikiliza kwa makini.

Kabla hujaanza, waalike wale ambao wapo wajiunge katika somo. Wahimize waondoe vivuruga mawazo ili Roho wa Bwana aweze kuhisiwa.

Eleza kwamba ungependa kuanza na kumaliza kila somo kwa sala. Jitolee kutoa sala ya kufungua. Sali kwa urahisi na kwa dhati kwamba Mungu awabariki watu unaowafundisha katika kila nyanja ya maisha yao. Sali kwamba waweze kuhisi ukweli wa kile utakachofundisha. Kumbuka kwamba “kuomba kwa [mtu] mwenye haki kwafaa sana” (Yakobo 5:16).

Kuwa na imani katika nguvu za kuongoa za Roho Mtakatifu. Kama utakavyoongozwa na Roho, unaweza kuelezea mawazo kama yafuatayo wakati unapoanza kufundisha:

  • Mungu ni Baba yetu wa Mbinguni mwenye upendo. Sisi sote ni kaka na dada. Yeye anatutaka sisi tupate shangwe.

  • Sisi sote tunazo changamoto na mapambano. Bila kujali kile unachokabiliana nacho, Yesu Kristo na mafundisho Yake yanaweza kukusaidia. Yeye anaweza kukusaidia upate amani, tumaini, uponyaji, na furaha. Yesu anaweza kukusaidia uwe na nguvu nyingi kwa ajili ya changamoto za maisha.

  • Sisi sote tunafanya makosa, ambayo yanaweza kuleta hisia za hatia, aibu, na kujuta. Hisia hizi zitaondoka tu tunapotubu na kutafuta msamaha wa Mungu. Ni kupitia Upatanisho wa Yesu Kristo pekee tunaweza kuponywa kikamilifu kutokana na dhambi zetu.

  • Sisi tutakuwa wenye kukuongoza ili uweze kujifunza ukweli wa ujumbe wetu kwa ajili yako mwenyewe. Tutakualika ufanye mambo fulani, kama vile kusoma, kusali, na kuhudhuria kanisani. Wajibu wetu ni kukusaidia utende juu ya mialiko hii na kuelezea baraka unazoweza kupokea. Tafadhali uliza maswali.

  • Tumeitwa na nabii wa Mungu ili kushiriki kile tunachojua. Tunajua kwamba ujumbe wetu ni wa kweli.

  • Tutakufundisha ujue jinsi ya kufanya maagano, au ahadi maalum, na Mungu. Maagano haya yatakuunganisha na Mungu na kukuruhusu upokee shangwe, nguvu, na ahadi maalum kutoka Kwake.

  • Utajifunza jinsi ya kufanya mabadiliko katika maisha yako na kumfuata Yesu Kristo na mafundisho Yake. Fundisho moja muhimu la Yesu Kristo, na agano la kwanza tunalofanya, ni kufuata mfano Wake kwa kubatizwa kwa mamlaka sahihi (ona Yohana 3:5; Mafundisho na Maagano 22).

Picha
wamisionari wakisali

Kabla ya kufundisha somo, toa muhtasari rahisi wa kile utakachofundisha. Wasaidie watu waone jinsi linavyowahusu. Kwa mfano, ungeweza kusema, “Tuko hapa kushiriki ujumbe kwamba Yesu Kristo ameanzisha Kanisa Lake hapa duniani leo na amewaita manabii walio hai kutuongoza.” Au ungeweza kusema, “Tuko hapa ili kukusaidia ujue kwamba Mungu anakupenda na ana mpango kwa ajili ya furaha yako.”

Watu wote watafaidika wanapokubali na kuishi injili ya Yesu Kristo. Baba wa Mbinguni anaweza kuwa aliwabariki watu unaowapata kwa maandalizi ya kiroho ya thamani (ona Alma 16:16–17).

Kumwalika Roho na kushiriki ukweli katika mkutano wa kwanza kutawasaidia watu wawatambue ninyi kama watumishi wa Bwana.

Kujifunza Binafsi au na Mwenza

Tumia mapendekezo yaliyopo katika sehemu hii ili kufanya mazoezi katika njia tofauti za kuanza somo.

Tumia maandiko

Vitabu vikuu vya Kanisa ni nyenzo zako za msingi kwa ajili ya kufundisha injili ya urejesho ya Yesu Kristo. Kuna sababu nyingi kwa nini ni muhimu kutumia maandiko kama msingi wa ufundishaji wako. Kwa mfano:

Kwa kutumia maandiko katika ufundishaji wako, unaweza kuwasaidia wengine waanze kujifunza maandiko wao wenyewe. Upendo wako wa maandiko unapokuwa dhahiri, watahamasika kujifunza. Onesha jinsi kujifunza maandiko kutakavyowasaidia wao wajifunze injili na wahisi upendo wa Mungu. Toa mifano ya jinsi gani maandiko yanavyoweza kuwasaidia wapate majibu ya maswali yao na wapokee mwongozo na nguvu.

Jitolee kujifunza maandiko ili uweze kufundisha kutoka kwenye maandiko hayo kwa ufanisi (ona sura ya 2). Uwezo wako wa kufundisha kutoka kwenye maandiko utaboreka unapojifunza kila siku, vyote binafsi na pamoja na mwenza wako.

Wasaidie watu wakuze imani katika Yesu Kristo kupitia kujifunza maandiko, hasa Kitabu cha Mormoni. Mapendekezo yafuatayo yanaweza kusaidia.

Picha
kundi likisoma maandiko

Tambulisha Maandiko

Kwa ufupi eleza historia ya kifungu hicho. Mifano ifuatayo inaonesha baadhi ya njia za kutambulisha maandiko.

  • “Katika historia ya Joseph Smith, Joseph anatuambia kwa maneno yake mwenyewe kile kilichotoke wakati alipokwenda ndani ya kijisitu kusali. Alisema, ‘Niliona nguzo ya mwanga …’”

  • “Katika kifungu hiki, nabii Alma alikuwa akiwafundisha watu ambao walikuwa masikini jinsi ya kufanyia kazi imani yao katika neno la Mungu. Analinganisha neno la Mungu na mbegu ambayo inaweza kupandwa katika mioyo yetu? Je, utaanza kusoma mstari … ?”

Soma Kifungu hicho

Soma aya kwa sauti au muombe mtu unayemfundisha asome kwa sauti. Kuwa msikivu kwa wale ambao wanasumbuka kusoma. Kama kifungu ni kigumu kwao kuelewa, soma pamoja nao na uelezee kama inavyohitajika. Elezea maneno au vishazi vyovyote vigumu. Au wape kifungu kidogo rahisi wasome. Waalike watafute vipengele maalum kwenye kifungu.

Tumia Maandiko

Nefi alisema, “Nililinganisha maandiko yote na sisi, ili yaweze kuwa kwa ajili yamanufaa yetu na kujifunza” (1 Nefi 19:23). “Kulinganisha” humaanisha kutumia maandiko katika maisha yako.

Linganisha maandiko na wale unao wafundisha kwa kuonesha jinsi gani hadithi na kanuni zinavyohusiana nao binafsi. Kwa mfano:

  • “Kama ninyi, watu wa Alma walikuwa na mizigo mizito, karibia zaidi ya vile ambavyo wangehimili. Lakini walipoonesha imani na kusali, Mungu aliwaimarisha ili waweze kuvumilia changamoto. Kisha aliwakomboa kutokana na majaribu yao. Kama vile Yeye alivyofanya kwa watu hawa, najua Mungu atakusaidia katika majaribu yako unapo …” (ona Mosia 24.)

  • “Mafundisho ya Alma kwa watu katika Maji ya Mormoni yanatumika hata kwetu leo. John, uko tayari … ?” (Ona Mosia 18.)

Wafundishe watu jinsi ya “kulinganisha” maandiko peke yao. Kugundua matumizi binafsi kutawasaidia watumie na wapate uzoefu wa nguvu za neno la Mungu.

Waalike na Wasaidie Watu Wasome Maandiko Peke Yao

Watu unaowafundisha wanahitaji kusoma maandiko, hasa Kitabu cha Mormoni, ili kupata ushuhuda wa ukweli. Kwa kutumia maandiko kwa mafanikio katika kufundisha kwako unaweza kuwasaidia watu waanze kujifunza maandiko peke yao.

Baada ya kila matembezi, pendekeza sura au mistari mahususi kwa ajili ya wao kusoma. Pendekeza maswali kwa ajili ya wao kufikiria wakati wanaposoma. Wahimize wajifunze maandiko kila siku peke yao na pamoja na familia zao. Ungeweza pia kuwaomba waumini wasome pamoja nao kati ya masomo.

Kabla ya kuanza somo linalofuata, fuatilia kwa kujadili kile ulichowaalika watu wasome. Kadiri inavyohitajika, wasaidie waelewe na “walinganishe” maandiko haya. Wahimize waandike fikra zao na maswali yao.

Unapowasaidia watu wasome, waelewe, na watumie maandiko—hususani Kitabu cha Mormoni—watakuwa na uzoefu wa kiroho na neno la Mungu. Watakuwa na uwezekano mkubwa wa kusoma peke yao na kufanya maandiko kuwa sehemu muhimu ya maisha yao.

Picha
wamisionari wakiifundisha familia

Wasaidie Watu Wapate Maandiko

Maandiko na maneno ya manabii walio hai yanapatikana katika njia nyingi na lugha nyingi kuliko hapo awali. Jifunze ni chapisho lipi na chaguzi za kidijitali zinapatikana kwa watu unaowafundisha. Wasaidie watu wapate maandiko katika njia zinazoendana na mahitaji yao na mapendeleo yao. Zingatia yafuatayo:

  • Waulize watu ni kwa lugha ipi wangependa kusoma au kusikiliza maandiko.

  • Wale ambao wanapata shida kusoma, au wanapata shida kuelewa kile wanachosoma, wanaweza kufaidika kutokana na kusoma kwa sauti au kusikiliza rekodi za sauti. Hizi zinapatikana kupitia app na tovuti za bila malipo za Kanisa.

  • Kama mtu ana chombo cha kidigitali, msaidie apate maandiko, hasa Kitabu cha Mormoni. App ya Kitabu cha Mormoni na Maktaba ya Injili havina malipo na ni rahisi kushiriki.

  • Kama unatumia maandishi, chati, au barua pepe, tuma viungo au picha za maandiko. Wakati unapofundisha katika chati ya video, fikiria kushiriki skrini yako ili muweze kusoma mistari pamoja.

  • Wasaidie watu wapate maneno ya manabii walio hai.

Kujifunza Binafsi au na Mwenza

Hakikisha wewe na mwenza wako mna nyenzo ya maandiko iliyosasishwa kwenye simu yenu, ikijumuisha app ya Kitabu cha Mormoni na Maktaba ya Injili.

Chagua mojawapo ya vifungu vya maandiko vifuatavyo: ukurasa wa jina wa Kitabu cha Mormoni; 3 Nefi 11; Moroni 10:3–8; Yohana 17:3; Warumi 8:16–17; 1 Wakorintho 15:29; Yakobo 1:5; 1 Petro 3:19–20; Amosi 3:7.

Amua jinsi ambavyo:

  • Ungetambulisha kifungu.

  • Ungetoa historia na muktadha.

  • Ungesoma kifungu na uelezee maana yake.

  • Ungefafanua maneno magumu.

  • Wasaidie wale unaowafundisha watumie maandiko katika maisha yao.

Kujifunza Maandiko

Kwa nini ni muhimu kufundisha kutoka katika maandiko?

Shiriki Ushuhuda Wako.

Ushuhuda ni ushahidi wa kiroho unaotolewa na Roho Mtakatifu. Kushiriki ushuhuda wako ni kutoa tamko rahisi la moja kwa moja la ufahamu au imani kuhusu ukweli wa injili. Kushiriki ushuhuda wako huongeza ushahidi wako binafsi kwenye kweli ulizofundisha kutoka kwenye maandiko.

Kushiriki ushuhuda wako ni njia yenye nguvu ya kumwalika Roho na kuwasaidia wengine wahisi ushawishi Wake. Mojawapo ya misheni za Roho Mtakatifu ni kushuhudia juu ya Baba wa Mbinguni na Yesu Kristo. Yeye kila mara hutimiza hili katika wenza na wewe wakati unapotoa ushuhuda.

Ushuhuda wenye nguvu hautegemei ufasaha au ukubwa wa sauti yako—bali kusadiki na udhati wa moyo wako. Kuwa makini usiharakishe au kutia chumvi ushuhuda wako. Wape watu nafasi ya kumhisi Roho Mtakatifu akitoa ushahidi kwao kwamba kile ulichofundisha ni cha kweli.

Ushuhuda wako unaweza kuwa rahisi kama vile “Yesu Kristo ni Mwokozi na Mkombozi wetu” au “Mimi nimejifunza mwenyewe kwamba Kitabu cha Mormoni ni cha kweli. Ungeweza pia kushiriki uzoefu mfupi kuhusu jinsi ulivyopata ushuhuda huu.

Unapofundisha, shiriki ushuhuda wako kadiri unavyohisi msukumo siyo tu mwishoni. Wakati mwenza wako anafundisha, shiriki ushuhuda wako kutoa ushahidi wa pili ya juu ya kile ambacho yeye amefundisha.

Shiriki ushuhuda wako kwamba kanuni unayoifundisha itabariki maisha ya mtu yule kama ataifuata. Eleza jinsi gani kuishi kanuni hiyo kulivyoyabariki maisha yako. Ushuhuda wako wa dhati utasaidia kujenga mazingira kwa ajili ya watu kumhisi Roho Mtakatifu akithibitisha ukweli.

Kujifunza Binafsi

Vifungu vya maandiko vifuatavyo ni mifano ya kutoa ushuhuda. Fikiria maswali pale unaposoma kila andiko. Andika majibu yako katika shajara yako ya kujifunzia.

Kujifunza Maandiko

Ni kipi maandiko yafuatayo yanafundisha kuhusu kanuni na ahadi za kutoa ushuhuda?

Panga na Rekebisha Ufundishaji Wako ili Kukidhi Mahitaji

Kila mtu unayemfundisha ni wa pekee. Tafuta kuelewa utashi wa kiroho, mahitaji, na wasiwasi wake. Uliza maswali na sikiliza kwa makini. Ingawa unaweza usielewe kikamilifu mahitaji ya mtu, kumbuka kwamba Baba wa Mbinguni anaelewa. Yeye atakuongoza kupitia Roho Mtakatifu.

Picha
wamisionari wakiwafundisha wanandoa

Mruhusu Roho Aongoze Utaratibu wa Masomo

Mruhusu Roho aongoze utaratibu ambao unafundisha masomo. Una uhuru wa kufundisha masomo katika utaratibu ambao ni bora kwa ajili ya mahitaji, maswali, na hali za wale unaowafundisha.

Mara kwa mara ungeweza kuunganisha kanuni kutoka kwenye masomo tofauti ili kushughulikia mahitaji na mapendeleo wa mtu. Ona mifano mitatu ifuatayo.

Yuki alikupata mtandaoni na anauliza kwa nini rafiki zake katika kanisa hawavuti sigara au kunywa pombe. Ungeweza kumfundisha kuhusu baraka za amri kwa kutumia sehemu zifuatazo kutoka sura ya 3:

Samuel hahisi kama amejumuishwa popote. Ungeweza kumfundisha kuhusu utambulisho wake na mahali pake katika familia ya Mungu kwa kutumia sehemu zifuatazo kutoka kwenye sura ya 3:

Tatyana amejifunza kuhusu dini nyingi na anataka kujua nini hufanya Kanisa hili liwe tofauti. Ungeweza kumfundisha kuhusu Urejesho wa injili ya Yesu Kristo kwa kutumia sehemu zifuatazo kutoka katika sura ya 3:

Baba wa Mbinguni anawajua watoto Wake, kwa hiyo tafuta mwongozo ili kufanya maamuzi haya wakati unapojiandaa kufundisha. Sali kwa ajili ya kipawa cha utambuzi pale unapoamua nini cha kufundisha. Kuwa makini juu ya mawazo na hisia ambazo zinakujia.

Picha
familia ikisoma maandiko

Ruhusu Muda kwa ajili ya Watu Kutumia Kile Wanachojifunza

Unapofundisha, ruhusu muda kwa ajili ya watu kutumia kile wanachojifunza (ona 3 Nefi 17:2). Tafuta njia sahihi za kuwasaidia katika kutimiza ahadi zao. Fokasi kwenye kuwasaidia kwa vitendo ambavyo vitajenga msingi wa Imani, kama vile kusali, kusoma, na kuhudhuria kanisani. Hii itawawezesha wao kutimiza ahadi za zaida.

Unapopanga na kufundisha, kuwa makini kuhusu ni taarifa kiasi gani unashiriki. Lengo la msingi la ufundishaji wako ni kumsaidia mtu ajenge imani katika Yesu Kristo ili iongoze kwenye toba. Lngo lako si kuona ni kiasi gani cha taarifa unaweza kukitoa.

Fundisha kwa kasi ambayo ni sahihi kwa mtu huyo. Uliza maswali na sikiliza kwa makini ili uelewe ni vizuri kiasi gani anajifunza na kutumia kile unachofundisha.

Kweli unazozifundisha, zikiungwa mkono na nguvu ya Roho Mtakatifu, zinaweza kuwashawishi watu watumie haki yao ya kujiamulia katika njia ambazo zinajenga imani yao katika Kristo. Wanapotumia imani katika Bwana kwa kutumia kile wanachojifunza, watakuja kujua kwa njia ya Roho kwamba injili ni ya kweli.

Tumia Fursa Tofauti Tofauti za Kufundisha

Fursa za kufundisha huja kwa aina nyingi, kama vile kwenye matembezi binafsi, chati za video, simu, ujumbe wa maandishi, na mitandao ya kijamii.

Heshimu Muda wa Watu

Fanya ufundishaji wako kuwa rahisi na mfupi. Watu wana uwezekano mkubwa wa kukutana na wewe kama unaheshimu muda wao na maombi yao. Uliza ni muda kiasi gani wanao kwa aili ya kuwatembelea. Anza na maliza mazungumzo yoyote katika muda mliokubaliana, iwe unamfundisha mtu ana kwa ana au mtandaoni. Fahamu kwamba sehemu zingine, simu au chati ya video inaweza kuwa ghali.

Utahitaji mikutano mingi ili kufundisha kanuni zilizopo katika somo moja. Kwa kawaida matembezi ya kufundisha hayapaswi kuzidi dakika 30, na unaweza kumfundisha mtu katika dakika chache kama vile dakika 5 tu. Rekebisha ufundishaji wako kulingana na muda wa watu.

Tumia Teknolojia kwa Busara

Una nafasi nyingi za kuwafundisha watu ukitumia teknolojia. Watu wengine wanapendelea urahisi au ufaragha wa kuchangamana kupitia njia za kieletroniki. Hata watu unaowatembelea ana kwa ana wanaweza kufaidika kutokana na msaada wa ziada kupitia teknolojia. Jadilini nyenzo zinazopatikana za kuwasiliana. Kisha fuatilia na ubaki umeunganika. Ruhusu mapendeleo ya kila mtu yaongoze mchangamano wenu.

Teknolojia kama vile simu za video inaweza kuwa msaada hasa kwa kuwafundisha watu ambao wana shughuli nyingi au wanaishi mbali. Wakati mwingine ni rahisi kwa waumini kushiriki katika somo kwa njia ya teknolojia.

Wasaidie Wanafunzi Wadogo

Wakati wa huduma ya Mwokozi, Yeye aliwaambia wafuasi Wake: ‘Waacheni watoto wadogo waje kwangu, na msiwazuie: kwa maana watoto kama hawa ufalme wa Mungu ni wao” (Marko 10:14). Unapowafundisha watoto, rekebisha mbinu na ujumbe wako ili kukidhi mahitaji yao. Wasaidie wajifunze injili kwa kujadili mambo ambayo yanafahamika kwao. Hakikisha kwamba wanaelewa kile unachokifundisha.

Kujifunza Maandiko

Soma Mafundisho na Maagano 84:85. Inamaanisha nini kupewa “sehemu ile ambayo itakakusudiwa kwa kila mtu”? Ni kwa jinsi gani unaweza kutumia hili katika ufundishaji wako?

Ni nini Bwana amewaahidi wamisionari waaminifu kuhusu kujua nini cha kusema?

Fundisha pamoja na Mwenza Wako kwa Umoja

Bwana alisema, “Nanyi mtaenenda katika nguvu ya Roho wangu, mkihubiri injili yangu, wawili wawili” (Mafundisho na Maagano 42:6). Yeye pia anawaamuru wewe na mwenza wako “muwe na umoja” (Mafundisho na Maagano 38: 27). Ufundishaji wako utakuwa wenye nguvu zaidi na wa kupendeza kama wewe na mwenza wako mtafanya kazi umoja. Pokezaneni kutoa sehemu fupi fupi za masomo.

Wakati wa kujifunza na mwenza, jadilini na mfanye mazoezi ya jinsi mtakavyofundisha ili muweze kuwa na umoja. Andaeni jinsi mtakavyofanya kazi pamoja wakati mnapowafundisha watu mtandaoni. Fuata ulinzi kwa ajili ya kutumia teknolojia, ulioainishwa katika sura ya 2.

Picha
wamisionari wakimfundisha mwanamume

Wakati mwenza wako anafundisha, sali, sikiliza, na mtazame yeye. Msaidie mwenza wako kwa kutoa ushahidi wa pili kwenye kweli ambazo \amezifundisha (ona Alma 12:1). Fuata misukumo yako wakati Roho anapokushawishi useme kitu.

Kuwa mwenye kuvutiwa kwa dhati na watu unaowafundisha. Wasikilize Dumisha kuwaangalia machoni wakati wanapozungumza au wewe unapozungumza. Kwa makini chunguza majibu yao, na usikilize misukumo ya kiroho.

Waalike Waumini Washiriki

Waalike waumini wakusaidie kufundisha na wawasaidie watu unaofanya nao kazi. Hii inaweza kutokea ana kwa ana au kimtandao. Wakati wa mkutano wa kila wiki wa uratibu, shauriana na viongozi wa kata kuhusu nani angeweza kusaidia.

Wakati waumini wanaposhiriki katika kufundisha na kuwa marafiki, wanaweza kuongeza umaizi na kutengeneza miunganiko kama marafiki. Watahisi shangwe ya kazi ya umisionari.

Waalike Waumini Wakusaidie Kufundisha

Kabla ya masomo, panga na waumini jinsi ya kufanya kazi pamoja. Ungeweza kutumia ujumbe wa maandishi au kupiga simu ili kuthibitisha kile utakachokuwa ukifundisha, nani atasali, nani ataongoza mazungumzo, na maelezo mengine.

Wajibu wa msingi wa muumini katika masomo ni kutoa ushuhuda wa dhati, kushiriki uzoefu mfupi wbinafsi, na kukuza uhusiano na watu unaowafundisha. Ungeweza kuwaomba waumini washiriki jinsi ambavyo wameweza kujifunza, kukubali, na kuishi kanuni maalum katika somo. Kama wao ni waongofu, waalike kushiriki jinsi walivyofikia uamuzi wa kujiunga na Kanisa.

Wakati waumini wanapowapa mtu wa kumfundisha, waombe washiriki katika ufundishaji. Waumini wanaweza kuhusishwa zaidi katika hali hizi. Shauriana nao kuhusu jinsi gani wangependa kushiriki.

Fikiria jinsi gani kutumia teknolojia kufundisha pamoja na waumini kungekuwa sahihi. Teknolojia huwaruhusu waumini wajiunge nawe bila sharti la muda ambalo matembezi ya ana kwa ana yanahitaji.

Katika mkutano wa kila wiki wa uratibu, panga na viongozi wa kata kuwa na muumini akishiriki katika masomo mengi iwezekanavyo (ona sura ya 13). Fikiria kuwaomba waumini wapya wakusaidie kufundisha.

Kujifunza Binafsi au na Mwenza

Fikiria kwamba una miadi ya kufundisha somo kwa familia katika nyumba ya muumini. Jadili jinsi ambavyo ungeweza kumhusisha kila mmoja wa waumini wafuatao katika kukusaidia kufundisha:

  • Mmisionari wa kata ambaye karibuni amerudi kutoka misheni

  • Kuhani

  • Muumini mpya

  • Rais wa akidi ya wazee, au Muungano wa Usaidizi

Waalike Waumini Watoe Msaada

Waumini wanaweza pia kutoa msaada wenye thamani kwa watu kati ya matembezi ya ufundishaji. Wanaweza kutuma ujumbe wa maandishi, kusoma maandiko pamoja, kuwaalika watu kwenye nyumba zao au kwenye shughuli, au kuwaalika wakae pamoja nao kanisani. Wanaweza kujibu maswali na kuonesha vile maisha yao yalivyo wakiwa kama waumini wa Kanisa. Uzoefu wa maisha yao na mtazamo wao unaweza kuwasaidia wao kujumuika na watu katika njia ambazo wakati mwingine ni tofauti sana na jinsi wamisionari wanavyojumuika.

Shauriana na waumini kuhusu jinsi mnavyoweza kufanya kazi pamoja ili kuwasaidia watu nje ya matembezi ya ufundishaji.

Fundisha kwa ajili ya Uelewa

Fundisha injili ya Yesu Kristo ili watu waielewe. Jifunze maandiko na masomo ili uweze kufundisha kwa uwazi kutoka kwenye maandiko hayo. Kadiri unavyofundisha kwa uwazi zaidi, ndivyo itakavyokuwa fursa bora kwa ajili ya Roho Mtakatifu kushuhudia ukweli.

Uliza maswali ili kuwasaidia watu wafikirie kuhusu kile ulichofundisha. Kisha sikiliza ili kuona kama wanakielewa na kukikubali.

Sehemu ya kufundisha kwa ajili ya uelewa ni kuelezea maneno, virai, na mawazo. Unaweza kuboresha uwezo wako wa kufundisha injili kwa:

  • Kuelewa maneno unayotumia.

  • Kufafanua maneno ambayo wengine wanaweza kuwa hawayaelewi.

  • Kuwauliza watu maswali kama vile “Je, ungeweza kushiriki nasi uelewa wako wa kile tulichofafanua?” au “Je, ungependa kufanya muhtasari wa kile ambacho tumekizungumzia?

Unapofundisha mafundisho katika sura ya 3, andika maneno, virai na mawazo yoyote ambayo watu wangeweza kuwa hawakuyaelewa. Fafanua haya kwa kutumia nyenzo katika Maktaba ya Injili, kama vile Mwongozo wa Maandiko, Kamusi ya Biblia, na Mada za Injili.

Fanya ufundishaji wako uwe rahisi na mfupi. Ufanye ufokasi juu ya injili ya Yesu Kristo, ujenge uelewa wa mafundisho na kanuni za msingi. Wasaidie watu watafute uelewa ambao huja kutoka kwa Roho Mtakatifu. Wanapopata uelewa huu, watakuja kuamini ujumbe wa injili.

Kujifunza Maandiko

Kwa nini tunapaswa kufafanua mafundisho kwa makini?

Je, tunajifunzaje? Kwa nini ni muhimu kufundisha maelezo taratibu?

Kwa nini uwazi ni muhimu?

Je, unaweza kujifunza nini kutoka kwenye mistari ifuatayo kuhusu jinsi gani Mungu huwasiliana na watoto Wake?

Uliza Maswali

Mwokozi aliuliza maswali yaliyowaalika watu wafikirie na wahisi kwa kina kuhusu kweli ambazo Yeye alizifundisha. Maswali Yake yalichochea kuichunguza nafsi na kuweka ahadi.

Maswali mazuri pia ni muhimu katika ufundishaji wako. Yatakusaidia uelewe matamanio, wasiwasi na maswali ya watu. Maswali mazuri yanaweza kumwalika Roho na kuwasaidia watu wajifunze.

Uliza Maswali Yenye Maongozi ya Kiungu

Tafuta mwongozo wa Roho katika kuuliza maswali mazuri. Maswali sahihi katika wakati sahihi yanaweza kuwasaidia watu wajifunze injili na wamhisi Roho.

Maswali yenye mwongozo wa kiungu na kusikiliza kwa dhati kutawasaidia watu wawe huru kuzungumza kwa uwazi na kushiriki hisia zao. Hii inaweza kuwasaidia wagundue ushuhuda unaokua. Pia watakuwa huru zaidi kukuuliza maswali wakati wanapokuwa hawaelewi kitu fulani au wana wasiwasi.

Jedwali lifuatalo linaonesha baadhi ya kanuni za kuuliza maswali yenye mwongozo, pamoja na baadhi ya mifano.

Kanuni na Mifano ya Maswali Yenye Mwongozo wa Kiungu

Kanuni

Mifano

Uliza maswali ambayo yanawasaidia watu wamhisi Roho.

  • Je, unaweza kushiriki uzoefu ambapo ulihisi ushawishi wa Mungu katika maisha yako?

  • Ni kwa jinsi gani ulihisi upendo wa Mungu kwa ajili yako?

Uliza maswali ambayo ni wazi na rahisi kueleweka.

  • Je, umejifunza nini kuhusu Yesu Kristo kutoka kwenye andiko hili?

Uliza maswali ambayo yanawasaidia watu wafikirie kuhusu kile unachofundisha.

  • Ni kwa jinsi gani hii ni sawa na kile ambacho tayari unakiamini? Ni kwa jinsi gani hii ni tofauti?

Uliza maswali ambayo yanakusaidia ujue watu wanaelewa vizuri kiasi gani kile unachokifundisha.

  • Je, una maswali yapi kuhusu kile ambacho tumefundisha leo?

  • Ni kwa jinsi gani utafanya muhtasari wa mazungumzo yetu ya leo?

Uliza maswali ambayo yanawasaidia watu kushiriki kile wanachohisi.

  • Ni kwa jinsi gani Yesu Kristo amekusaidia katika maisha yako?

  • Kitu gani kilikuwa muhimu zaidi kwako kutokana na kile tulichozungumza juu yake leo?

Uliza maswali ambayo yanaonesha upendo na shauku.

  • Ni kwa jinsi gani tunaweza kukusaidia?

Uliza maswali ambayo yatawasaidia watu watumie kile wanachojifunza.

  • Tunaweza kujifunza nini kutoka katika maandiko haya?

  • Ni kwa jinsi gani maandiko haya yanakusaidia katika maisha yako?

  • Kama tulivyozungumza, ni kipi umehisi kusukumwa kufanya kutokana na kile ulichojifunza?

Kujifunza na Mmisionari Mwenza

Pitieni tena mpango wenu wa somo kutoka kwenye somo mlilofundisha karibuni. Andikeni swali moja kwa kila kanuni kuu zilizoainishwa katika mpango wenu.

Rejeleeni maswali yenu ili kuona kama yanakubaliana na kanuni katika sehemu hii.

Kisha, jibuni kila swali kama vile ninyi ni watu mnaofundishwa.

Shiriki maswali yako na mwenza wako. Kwa pamoja, fanyeni tathimini na boresheni maswali yenu.

Kujifunza Binafsi au na Mwenza

Watu unaowafundisha wangeweza kukutana na uzoefu ufuatao:

  • Wanakuwa na uzoefu wa kiroho wakati wakisoma Kitabu cha Mormoni.

  • Wafanya kazi wenza kila mara wanadhihaki mambo ya kiroho.

  • Wanafamilia ni waumini thabiti wa kanisa lingine.

  • Marafiki wanaamini kwamba “Wamormoni” si Wakristo.

Fikiria juu ya swali ambalo wewe ungeuliza ili kujifunza zaidi kuhusu kila moja ya hali hizi. Andika maswali haya katika shajara yako ya kujifunzia. Jadiliana na mwenza wako jinsi ambavyo mngeweza kuboresha maswali mliyoyaandika.

Epukana na Maswali Yasiyofaa au Mengi Kupita Kiasi

Jaribu usiulize maswali ambayo:

  • Yana majibu dhahiri.

  • Yanaweza kumuaibisha mtu kama hajui jibu.

  • Yanajumuisha zaidi ya wazo moja.

  • Yanahuhusu mafundisho ambayo hujayafundisha.

  • Hayana dhumuni lililo wazi.

  • Ni mengi mno

  • Ya kupeleleza au yangeweza kuwakasirisha na kuudhi watu.

Ifuatayo ni mifano ya maswali ambayo hayafai:

  • Ni nani alikuwa nabii wa kwanza? (Mtu anaweza kuwa hajui jibu.)

  • Ni kwa jinsi gani kuiweka miili yetu kuwa safi kunatusaidia tuwe na Roho na tuoneshe kwamba tuko tayari kumfuata nabii wa Mungu? (Kuna wazo zaidi ya moja.)

  • Je, ni muhimu kujua kuhusu amri za Mungu? (Hili ni swali la ndiyo-hapana, na jibu ni dhahiri.)

  • Ni kitu gani kimoja tunaweza kufanya kila siku ambacho kitatusaidia tuhisi kuwa karibu na Mungu? (Hili ni swali lisilo dhahiri la kutafuta jibu mahususi: sali.)

  • Ni nani alikuwa nabii aliyefuata baada ya Nuhu? (Mtu anaweza kuwa hajui jibu, na swali hili si muhimu kwa ajili ya ujumbe wako.)

  • Je, unaelewa kile ninachosema? (Mtu angeweza kuhisi unamdharau.)

Kujifunza Binafsi au na Mwenza

Fikiria mahitaji ya mtu unayemfundisha. Jadilini jinsi ambavyo angeweza kujibu maswali yako. Panga baadhi ya maswali ya kuuliza ambayo yanafuata mwongozo katika sehemu hii. Jadilini jinsi ambavyo ambavyo maswali haya yangemwalika Roho na kumsaidia mtu ajifunze injili.

Sikiliza

Unapowasikiliza wengine kwa makini, utawaelewa vyema. Wanapojua kwamba mawazo na hisia zao ni muhimu kwako, watakuwa na uwezekano mkubwa wa kupokea mafundisho yako, kushiriki uzoefu binafsi, na kuweka ahadi.

Unaposikiliza, unaweza kupata umaizi wa jinsi ya kutohoa ufundishaji wako kwa mahitaji yao na mapendeleo yao. Unaweza kuwa na uelewa mzuri wa kweli zipi za injili zingekuwa na manufaa kwao.

Sikiliza hasa minong’ono ya Roho. Wakati wengine wanaposhiriki hisia zao, Roho Mtakatifu anaweza kukupa msukumo kwa fikra au mawazo. Roho anaweza pia kukusaidia uelewe kile wengine wanachojaribu kueleza.

Picha
wamisionari wakizungumza na familia

Sikiliza kwa Kujali kwa Dhati

Kusikiliza huhitaji juhudi na kujali kwa dhati. Wakati wengine wanapozungumza, hakikisha unazingatia juu ya kile wanachokisema. Epukana na tabia ya kupanga kitu ambacho utakisema.

Mzee Jeffrey R. Holland alifundisha: “Pengine kilicho muhimu zaidi ya kuzungumza ni kusikiliza. Watu hawa siyo vitu visivyo na uhai vilivyofichwa kama takwimu za ubatizo. … Waulize marafiki hawa ni kipi kilicho na maana sana kwao. Ni kipi wao wanakipenda sana, na ni kipi wao wanakithamini sana? Na kisha sikiliza. Kama mazingira ni sahihi unaweza kuwauliza hofu yao ni nini, ni kipi wanatamani, au ni kipi wanahisi kinakosekana kwenye maisha yao. Ninaahidi kwamba kitu fulani katika kile wanachosema daima kitaangazia ukweli wa injili ambao juu ya huo unaweza kutoa ushuhuda na ambao juu ya huo unaweza kisha kutoa zaidi. … Kama tukisikiliza kwa upendo, hatutakuwa na haja ya kujiuliza nini cha kusema. Kitatolewa kwetu—na Roho na rafiki zetu” (“Mashahidi Wangu,” Ensign, Mei 2001, 15).

Chunguza Jumbe Zisizozungumzwa

Watu pia wanawasiliana kupitia lugha yao ya mwili. Tazama vile wanavyoketi, maonyesho ya nyuso zao, kile wanachofanya kwa mikono yao, tuni ta sauti zao, na wapi wanaangalia. Kuchunguza jumbe hizi zisizozungumzwa kunaweza kukusaidia uelewe hisia za wale unaowafundisha.

Kuwa makini pia na lugha yako mwenyewe ya mwili. Tuma ujumbe wa kuvutiwa na shauku kwa kusikiliza kwa dhati.

Wape Watu Muda wa Kufikiria na Kujibu

Mwokozi kila mara aliuliza maswali ambayo yalihitaji muda kwa ajili ya kujibu. Wakati unauliza swali, tulia kidogo ili kumpa mtu nafasi ya kufikiria na kujibu. Usiogope ukimya. Watu mara nyingi wanahitaji muda kufikiri kuhusu kitu na kujibu maswalii au kueleza jinsi wanavyohisi.

Ungeweza kutulia kidogo baada ya kuuliza swali, baada ya kushiriki uzoefu wa kiroho, au wakati watu wanapopata ugumu kujieleza. Hakikisha unawapa muda wa kukamilisha mawazo yao kabla ya wewe kujibu. Usiwakatize wakati wanapozungumza.

Jibu kwa Kuonesha Huruma

Wakati mtu anajibu swali, anza majibu yako kwa kuonesha huruma ikiwa inafaa. Hurumahuonesha kwamba wewe unajali kwa dhati. Epuka kurukia hitimisho, kutoa masuluhisho haraka au kuonekana una majibu yote.

Thibitisha Kwamba Unaelewa Kile Watu Wanachosema

Wakati unatafuta kuelewa kile mtu anachosema, uliza ili kuhakikisha unaelewa. Kwa mfano, unaweza kuuliza, “Kwa hiyo kile unachosema ni . Je, hivyo ndivyo? au “Kama ninakuelewa vizuri, unahisi kwamba .” Wakati huna hakika ikiwa unaelewa, mwombe mtu afafanue.

Fanyia Utafiti Michangamano yenye Changamoto

Utawasaidia watu sana kwa kuwafundisha injili ya Yesu Kristo. Baadhi ya watu wanaweza kutaka wao wazungumze sana. Wakati mwingine watu wanahitaji tu mtu wa kusikiliza kwa upole masumbuko yao na hisia zao. Watu wengine wanaweza kutafuta kutawala au kubishana.

Jifunze kusimamia hali kama hizi kwa busara na kwa upendo. Unaweza kutohoa ufundishaji wako ili kushughulikia kitu fulani mtu alichoshiriki. Au unaweza kuhitaji kusema kwa upole kwamba ungependa kujadili wasiwasi wao wakati mwingine. Roho anaweza kukusaidia ujue jinsi ambavyo utajibu katika hali zenye changamoto.

Wasaidie Watu Wahisi Faraja Kushiriki Hisia za Kweli

Ili kuepukana na aibu, baadhi ya watu watajibu maswali kwa njia ambayo wanadhani unawataka wajibu badala ya kushiriki hisia zao za kweli. Tafuta kukuza uhusiano ambao unawaruhusu wawe huru kushiriki nawe hisia zao za kweli.

Kuwaelewa na kuunganika na watu kutakuruhusu uwasaidie, wakidhi matamanio yao na mahitaji yao, na kuonesha upendo wa Mwokozi kwao. Jenga uhusiano wa kutumainika kwa kuwa mkweli kwao, kudumisha uhusiano wa umisionari unaofaa, na kuonesha heshima.

Kujifunza Binafsi au na Mwenza

Tafakari ni vyema jinsi gani unawasikiliza wengine. Andika majibu yako katika shajara yako ya kujifunzia kwa maswali hapo chini. Au yajadili na mwenza wako.

A=Kamwe si kweli kwangu, B=Wakati mwingine ni kweli kwangu, C=Mara Nyingi ni kweli kwangu, D=Daima ni kweli kwangu

  • Wakati wengine wanapozungumza na mimi, ninafikiria uzoefu unaofanana ninaoweza kuushiriki badala ya kusikiliza kwa makini.

  • Wakati wengine wananiambia kuhusu hisia zao, ninajaribu kujiweka katika nafasi yao ili kuona jinsi ambavyo ningehisi.

  • Wakati ninawafundisha watu, ninafikiria kuhusu kile ninachokwenda kusema au kufundisha.

  • Ninachukia wakati watu wanapozungumza sana.

  • Ninajitahidi kufuata au kuelewa kile wengine wanachojaribu kuniambia.

  • Akili yangu mara nyingi haitulii wakati mwenzangu anapofundisha.

  • Ninakasirika kama mtu anazungumza na mimi na wengine wanaingilia au wanavuruga usikivu wangu.

  • Ninapokea misukumo ya kiroho ya kusema au kufanya kitu, lakini ninapuuzia.

Wasaidie Watu Wapate Majibu kwa Maswali yao na Wasiwasi Wao

Fanya juhudi za dhati kushughulikia maswali ya watu na uwasaidie watatue wasiwasi wao. Hata hivyo, siyo jukumu lako kujibu kila swali. Hatimaye, watu lazima watatue maswali yao na wasiwasi wao wenyewe.

Tambua kwamba siyo wasiwasi na maswali yote yanaweza kujibiwa kikamilifu. Baadhi ya majibu huwa wazi zaidi baada ya muda. Mengine bado hayajafunuliwa. Fokasi kwenye kujenga msingi thabiti wa kweli za msingi, muhimu za injili. Msingi huu utakusaidia wewe na wale unaowafundisha msonge mbele kwa subira na imani wakati kukiwa maswali ambayo hayakujibiwa au magumu.

Baadhi ya kanuni kwa ajili ya kujibu maswali zimeainishwa katika sehemu hii.

Picha
Yesu na Mwanamke Msamaria Kisimani

Elewa Wasiwasi

Baadhi ya kile unachowafundisha watu kinaweza kuonekana kuwa kigumu au kisichokuwa cha kawaida kwao. Kama watu wana maswali au wasiwasi, kwanza tafuta kuwaelewa kwa uwazi. Wakati mwingine wasiwasi wa watu ni kama siwa barafu. Ni sehemu ndogo tu inaonekana juu ya uso wa maji. Wasiwasi huu unaweza kuwa changamani. Sali kwa ajili ya kipawa cha utambuzi na mfuate Roho katika jinsi unavyojibu. Baba wa Mbinguni anajua mioyo na uzoefu wa watu wote (siwa barafu yote). Yeye atakusaidia ujue kile kilicho bora kwa kila mtu.

Kila mara wasiwasi ni wa kijamii kuliko kimafundisho. Kwa mfano, baadhi ya watu wanaweza kuogopa upinzani kutoka kwa wanafamilia ikiwawatajiunga na Kanisa. Au wanaweza kuogopa kukataliwa na marafiki kazini.

Tafuta kuelewa chanzo cha wasiwasi kwa kuuliza maswali na kusikiliza. Je, wasiwasi uliibuka kwa sababu mtu hana uthibitisho wa kiroho wa ukweli wa Urejesho? Je, uliibuka kwa sababu mtu hataki kuweka ahadi ya kuishi kanuni ya injili? Kujua chanzo cha wasiwasi wao kutakusaidia wewe ujue ikiwa utafokasi kwenye ushuhuda au ahadi.

Tumia Maandiko, Hususani Kitabu cha Mormoni, Kusaidia Kujibu Maswali

Waoneshe watu jinsi kweli katika maandiko zinavyoweza kusaidia kujibu maswali yao na kutatua wasiwasi wao. (Ona “(Kitabu cha Mormoni Hujibu Maswali ya Nafsi” katika sura ya 5.) Wakati watu wanatafuta mwongozo kwa kujifunza na kutumia maandiko, wataongeza uwezo wao wa kumsikia na kumfuata Bwana. Imani yao katika Yeye itaongezeka. Kwa imani iliyoongezeka kutakuja ushuhuda, toba, na ibada ya ubatizo.

Picha
Rais Henry B. Eyring

“Wakati mwingine ninaenda kwenye maandiko kwa ajili ya mafundisho. Wakati mwingine ninaenda kwenye maandiko kwa ajili ya maelekezo. Ninaenda na swali, na kawaida swali ni ‘Ni kipi Mungu anataka nifanye?’ au ‘Ni kipi Yeye anataka nihisi?’ Kila mara, ninapata mawazo mapya, fikra ambazo kamwe sikuwa nazo hapo awali, na ninapokea mwongozo na maelekezo na majibu ya maswali yangu” (Henry B. Eyring, katika “A Discussion on Scripture Study,” Ensign, July 2005, 22).

Inaweza kuwa msaada kueleza kwamba wingi wa uelewa wetu wa injili ya Yesu Kristo huja kutokana na kile kilichofunuliwa kwa Nabii Joseph Smith na wale ambao walimrithi. Maswali kuhusu ukweli wa injili yanaweza kutatuliwa kwa kupata ushuhuda kwamba Joseph Smith alikuwa nabii wa Mungu. Kusoma na kusali kuhusu Kitabu cha Mormoni ni njia muhimu ya kupata ushuhuda huu.

Wasaidie watu wafokasi kwenye kuimarisha imani yao katika Yesu Kristo. Kusoma na kusali kuhusu Kitabu cha Mormoni ni njia muhimu ya kuimarisha ushuhuda wao?

Waalike Watu Watende kwa Imani

Kadiri watu wanavyopiga hatua na kuimarisha ushuhuda wao wa injili ya urejesho, wataweza kutatua maswali yao na wasiwasi kutoka kwenye msingi wa imani. Wanapotenda kwa imani juu ya kweli wanazoziamini, wataweza kupata shuhuda zingine za kweli za injili.

Baadhi ya njia za kutenda kwa imani hujumuisha:

  • Kusali kila mara kwa kusudi halisi kwa ajili ya uvuvio na mwongozo.

  • Kujifunza maandiko, hasa Kitabu cha Mormoni.

  • Kuhudhuria kanisani

Kujifunza na Mmisionari Mwenza

Chagueni mwaliko mmoja kwa kutoa wakati mnapofundisha somo. Kisha bainisheni wasiwasi ambao ungeweza kumzuia mtu kukuubali mwaliko au kuweka ahadi. Jadilini na mfanye mazoezi jinsi mnavyoweza kuwasaidia watu kushughulikia kutatua wasiwasi wao.

Kujifunza Binafsi au na Mwenza

Katika shajara yako ya kujifunzia, andika jinsi ambavyo ungemrejelea Joseph Smith na Kitabu cha Mormoni ili kujibu wasiwasi ufuatao:

  • “Siamini kwamba Mungu huzungumza na watu tena.”

  • “Ninaamini kwamba ninaweza kumwabudu Mungu katika njia yangu mwenyewe badala ya kupitia dini iliyopangiliwa.

  • “Kwa nini niache kunywa divai kwenye milo yangu kama nitajiunga na kanisa lenu?”

  • “Kwa nini ninahitaji dini?”

Acha Kitu cha Kujifunza na Kusali Kukihusu

Mwisho wa kila matembezi ya kufundisha, wape watu kitu cha kujifunza, kutafakari, kusali kukihusu ili kujiandaa kwa ajili ya mkutano unaofuata. Kusoma, kusali, kutafakari kati ya matembezi ya kufundisha hualika ushawishi wa Roho Mtakatifu katika maisha yao.

Ungeweza kuwaalika watu wasome sura mahususi katika Kitabu cha Mormoni. Au ungeweza kuwahimiza watumie nyenzo za Kanisa, kama vile Maktaba ya Injili, ili kupata majibu ya maswali, kujifunza kuhusu mada, au kutazama video. Hii inaweza kuwa mada ya kuanzisha mjadala wakati ujao mnapokutana.

Picha
mtu akisoma maandiko

Epukana na kuwapa watu mambo mengi ya kufanya, hususani kama una mikutano mifupi, ya kila mara na wao.

Kujifunza Binafsi au na Mwenza

Mzingatie kila mtu mliyepanga kumfundisha wiki hii. Ni sura zipi katika Kitabu cha Mormoni zitakuwa na msaada sana kwao? Ni nyenzo zipi zingine zingewanufaisha? Andika kile unachodhamiria kutoa kwa kila mtu. Pia andika kile ambacho ungeweza kufanya ili kufuatilia wakati wa matembezi yako yajayo.

Kufundisha Watu wenye Uraibu

Unaweza kuwasaidia watu ambao wanapambana kushinda uraibu kwa kujadili mapambano yao kwa upendo, kuwasaidia, na kuwaunganisha na nyenzo. Unaweza kuwahimiza wahudhurie mojawapo ya vikundi vya Kanisa vya kusaidia kupata ahuweni ya uraibu. Vikundi hivi vinaweza kukutana ana kwa ana au mtandaoni. (Ona AddictionRecovery.ChurchofJesusChrist.org.) Wahimize watumie nyenzo katika kipengele cha “Uraibu” cha Msaada wa Maisha katika Maktaba ya Injili.

Viongozi wa Kanisa na waumini wenyeji wanaweza pia kutoa msaada. Baadhi ya watu walio na uraibu wanaweza kuhitaji tiba ya kitabibu na afya ya akili.

Hapa kuna mapendekezo machache kwa ajili ya jinsi unaweza kuwasaidia watu wanaopambana kushinda uraibu:

  • Imarisha juhudi zao za kuja kwa Kristo. Wasaidie waone kwamba juhudi zao ili kupata nafuu na kupona zinatambulika na kuthaminiwa kwa Baba yao wa Mbinguni na Yesu Kristo. Wafundishe kwamba wanaweza kuimarishwa kupitia Mwokozi na Upatanisho Wake. Yeye anatambua kikamilifu kusudi la moyo wao la kutenda mema.

  • Waombee katika sala zako binafsi na sali pamoja nao. Kadiri inavyofaa, wahimize watafute baraka kutoka kwa viongozi wenyeji wenye ukuhani.

  • Endelea kuwafundisha injili ya Yesu Kristo. Wafundishe kwamba Baba yako wa Mbinguni, Mwokozi, na Roho Mtakatifu wanawapenda na wanataka mafanikio yao.

  • Wahimize wahudhurie kanisani kila mara na wakuze urafiki na waumini.

  • Kuwa chanya na mwenye msaada—hasa kama watarudi nyuma.

Picha
Yesu akimfikia mwanamke

Uraibu ni mgumu kuushinda, na kurudi nyuma kunaweza kutokea. Viongozi wa Kanisa na waumini hawapaswi kushangazwa na hilo. Wanapaswa kuonesha upendo, wala si hukumu.

Muumini mpya ambaye anaacha kuhudhuria kanisa anaweza kurudia uraibu wa awali na anaweza kujihisi kuwa hastahili na kukata tamaa. Matembezi ya haraka ya kutoa faraja na msaada yanaweza kusaidia. Waumini wanapaswa kuonesha kwa maneno na matendo kwamba Kanisa ni mahali ambapo upendo wa Kristo unaweza kupatikana (ona 3 Nefi 18:32).

Kujifunza Binafsi au na Mwenza

Fikiria juu mtu unayemfundisha au mtu mpya au muumini anayerejea ambaye anajaribu kushinda uraibu. Pitia upya “Imani katika Yesu Kristo” na “toba” kutoka kwenye somo la “Injili ya Yesu Kristo” katika sura ya 3.

  • Nini ungeweza kumfundisha mtu huyu kutoka kwenye somo hilo na kutoka kwenye sura hii ambacho kingemsaidia?

  • Tengeneza mpango wa somo ili kumsaidia mtu huyu.

Kuwafundisha Watu Ambao Hawana Asili ya Ukristo

Baadhi ya watu unaowafundisha wanaweza kuwa hawana asili ya Ukristo au hawaamini katika Baba wa Mbinguni na Yesu Kristo. Hata hivyo, wengi wa watu hawa wana imani, desturi, na mahali wanapopachulia kwa utakatifu. Ni muhimu kwamba uoneshe heshima kwa ajili ya imani zao za kidini na desturi.

Wasaidie Waelewe Mungu Ni Nani

Unaweza kujiuliza jinsi ya kurekebisha ufundishaji wako kwa ajili ya watu ambao hawana asili ya Ukristo. Kanuni ambazo humsaidia mtu kujenga imani ni zile zile katika tamaduni zote. Wasaidie watu wapate uelewa sahihi wa Mungu na misheni takatifu ya Yesu Kristo. Njia nzuri zaidi kwa ajili yao ili wajifunze kweli hizi ni kwa kuwa na uzoefu binafsi wa kiroho. Baadhi ya njia unazoweza kuwasaidia wawe na uzoefu huu zimeainishwa hapo chini:

  • Fundisha kwamba Mungu ni Baba yetu wa Mbinguni na Yeye anatupenda. Sisi ni watoto Wake. Waalike watafute ushahidi huo kwa ajili yao wenyewe.

  • Fundisha kuhusu mpango wa wokovu.

  • Fundisha kwamba Mungu Baba na Yesu Kristo walimtokea Nabii Joseph Smith.

  • Toa ushuhuda wa dhati wa injili, ikijumuisha jinsi unavyohisi upendo wa Baba wa Mbinguni na kwa nini unachagua kumfuata Yesu Kristo.

  • Waalike watoe sala rahisi, za moyoni—wakiwa na wewe na wakiwa peke yao.

  • Waalike wasome Kitabu cha Mormoni kila siku—wakiwa na wewe na wakiwa peke yao.

  • Waalike wahudhurie kanisani.

  • Watambulishe kwa waumini wa Kanisa ambao wanaweza kueleza jinsi walivyofikia kuamini katika Baba wa Mbinguni na Yesu Kristo.

  • Waalike wazishike amri.

Watu wengi wanatamani kuwa na muunganiko mkubwa na Mungu na kupata dhumuni na maana katika maisha. Wasaidie waone jinsi ambavyo wao ni watoto wa Baba wa Mbinguni mwenye upendo na jinsi Yeye alivyo na mpango kwa ajili yao. Kwa mfano, ungeweza kuanza kwa sema kitu kama kifuatacho:

Mungu ni Baba yetu aliye Mbinguni, na Yeye anatupenda. Sisi ni watoto Wake. Tuliishi na Mungu kabla hatujazaliwa. Kwa sababu sisi ni watoto Wake, sote ni kaka na dada. Yeye anataka turejee Kwake. Kwa sababu ya upendo Wake kwa ajili yetu, Yeye ametoa mpango kwa ajili yetu kurudi Kwake kupitia Mwanaye, Yesu Kristo.

Tohoa Ufundishaji Wako kama Inavyohitajika

Waongofu wengi kutoka kwenye asili isiyo ya Ukristo wanasema kwamba hawakuelewa mengi ya kile wamisionari walichokuwa wakifundisha. Hata hivyo, walimhisi Roho na walitaka kufanya kile wamisionari walichowataka wafanye. Fanya yote uwezayo kuwasaidia watu waelewe mafundisho ya injili. Kuwa na subira na usikate tamaa. Inaweza kuchukua muda kwa watu kujifunza kutambua na kuonesha hisia zao. Unaweza kuhitaji kurekebisha kasi na kina cha ufundishaji wako ili uwasaidie.

Mapendekezo yafuatayo yanaweza kusaidia pale unapojiandaa kuwafundisha watu ambao hawana asili ya Ukristo:

  • Elewa ni hitaji gani la kiroho au pendeleo huwasukuma wakutane na wewe.

  • Toa muhtasari rahisi na pitia tena kila somo.

  • Waombe wakuambie kile wanachoelewa na kile ambacho wamepitia.

  • Fafanua maneno na kanuni ngumu. Watu wanaweza kuwa hawafahamu mengi ya maneno unayoyatumia wakati unapofundisha.

  • Rudi kwenye somo ulilofundisha awali ili kufundisha mafundisho kwa uwazi kabisa. Hii inaweza kuwa muhimu muda wowote wakati wa mchakato wa ufundishaji.

  • Tambua mialiko ambayo ungeweza kuitoa ili uwasaidie watu wapate baraka za injili.

Zilizoorodheshwa hapo chini ni baadhi ya nyenzo katika Maktaba ya Injili ambazo ungeweza kutumia ili uwasaidie wale wasio wa asili ya Ukristo.

  • Mungu ni Nani?

  • Yesu Kristo ni Nani?

  • Yesu Kristo, Mwana wa Mungu

  • Nini cha Kutarajia Unapozungumza na Wamisionari wa Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho

  • Waislamu na Watakatifu wa Siku za Mwisho: Imani, Maadili, na Mitindo ya Maisha

Kujifunza Binafsi au na Mwenza

Kama inawezekana, mbainishe muongofu ambaye hakuwa wa asili ya Ukristo kabla ya kukutana na wamisionari. Panga kukutana naye na umuulize kuhusu uzoefu wake wa uongofu. Kwa mfano, unaweza kumuuliza mtu huyo kuhusu:

  • Je! ni kipi kilikufanya uamini katika Baba wa Mbinguni na Yesu Kristo.

  • Uzoefu wa kusali kwa mara ya kwanza ulikuwa namna gani.

  • Ilikuwaje mara ya kwanza yeye kuhisi jibu la sala.

  • Wajibu wa maandiko katika uongofu wake.

  • Ilikuwaje kuhudhuria kanisani.

Andika kile unachojifundisha katika shajara yako ya kujifunzia.

Fikiria kumwalika mtu akusaidie kumfundisha mtu ambaye hana asili ya Ukristo.


Mawazo kwa ajili ya Kujifunza na Kutumia

Kujifunza Binafsi

  • Fikiria umewekwa katika hali zifuatazo: Ni kwa jinsi gani ungeweza kutumia kanuni na ujuzi katika sura hii kuwasaidia watu wapige hatua? Panga jinsi utakavyozitumia katika kila hali.

    • Mtu ambaye amekuwa akijiandaa kwa ajili ya ubatizo anakuambia hataki tena kukutana na wewe.

    • Unakutana kwa mara ya saba na mtu ambaye ameshafunzwa na wamisionari kadhaa kwa kipindi cha zaidi ya miaka miwili. Kumekuwa na dalili chache za maendeleo.

  • Chagua mojawapo ya masomo ya mmisionari. Bainisha kifungu kimoja au viwili vya maandiko kutoka kwenye kila kanuni muhimu. Fanya mazoezi ya kufundisha kutoka kwenye vifungu hivi kama vilivyoainishwa katika sehemu ya “Tumia Maandiko” ya sura hii.

Kujifunza pamoja na Mwenza na Kubadilishana Mwenza

  • Someni hadithi ya Amoni na Mfalme Lamoni katika Alma 18–19 na hadithi ya Haruni katika Alma 22:4–18. Mnaposoma, tambueni na mbainishe jinsi Amoni na Haruni:

    • Walivyomfuata Roho na kufunza kwa upendo.

    • Walivyoanza kufundisha.

    • Walivyotohoa ufundishaji wao ili kukidhi mahitaji.

    • Walivyotoa ushuhuda.

    • Walivyotumia maandiko.

    • Walivyouliza maswali, walivyosikiliza, na walivyowasaidia wale waliowafunza watatue wasiwasi wao.

    • Walivyowahimiza wale waliowafundisha waweke ahadi.

    Jadilini jinsi huduma yao na ufundishaji wao ulivyomwathiri Mfalme Lamoni, baba yake, na Abishi.

Baraza la Wilaya, Mikutano ya Kanda na Baraza la Uongozi la Misheni

  • Waalike waumini au wale wanaofundishwa sasa kwenye mkutano wenu. Eleza kwa kila kundi kwamba wewe unataka wamisionari waboreshe uwezo wao wa kushiriki ujumbe wao muhimu. Chagua somo na ujuzi. Waruhusu wamisionari wamfundishe mtu au watu somo ulilolichagua kwa dakika 20, wakifokasi juu ya ujuzi ulioubainisha. Waruhusu wabadilishane wale wanaowafundisha baada ya dakika 20. Baada ya wamisionari kufundisha, yaunganishe makundi pamoja. Mruhusu mtu au watu wawaambie wamisionari kile kilichoenda vizuri na kile ambacho wanapaswa kuboresha.

  • Onesha mifano ya video ya wamisionari wakifundisha au wakitafuta watu wa kuwafundisha. Chagua ujuzi na ujadili ni vyema kiasi gani wamisionari walitumia kanuni kwa ajili ya ujuzi huo.

  • Chagua ujuzi, na bainisha mafundisho au vifungu vya maandiko ambavyo vinauunga mkono. Fundisha msingi wa mafundisho wa ujuzi huo kwa wamisionari.

Viongozi wa Misheni na Washauri wa Misheni

  • Mara kwa mara andamana na wamisionari wanapofundisha. Panga jinsi unavyoweza kushiriki katika kufundisha.

  • Wahimize viongozi wenyeji washiriki pamoja na wamisionari katika matembezi yao ya ufundishaji.

  • Onesha kwa mfano na wasaidie wamisionari wafanyie mazoezi mojawapo ya ujuzi wa kufundisha ulioelezwa katika sura hii, kama vile kuuliza maswali mazuri na kusikiliza.

  • Onesha kwa mfano utumiaji mzuri wa maandiko yanavyofaa wakati unapowafundisha wamisionari katika mikutano mikuu ya kanda, baraza la uongozi wa misheni, na mahojiano. Fanya hivyo hivyo wakati unapofundisha pamoja nao.

  • Wasaidie wamisionari wayaelewe maandiko na wakuze upendo kwa ajili ya maandiko. Mzee Jeffrey R. Holland aliwashauri viongozi wa misheni:

    “Fanyeni upendo kwa ajili ya neno la Mungu uwe kiini cha utamaduni wa misheni yenu. … Kuweni na uelewa wa ufunuo na matumizi ya kila wakati ya vitabu vikuu vya Kanisa viwe mojawapo ya sifa muhimu za wamisionari wenu kwa maisha yao yote.

    “Wakati mnapowafundisha wamisionari wenu—na hiyo ni wakati wote—wafundisheni kutoka kenye maandiko. Waruhusuni waone mahali ambapo mnapata nguvu yenu na mwongozo wenu. Wafundisheni wapende na wategemee ufunuo huo uliokusanywa.

    “Rais [wangu] wa misheni alifundisha kutoka kwenye Kitabu cha Mormoni na maandiko [mengine] kila mara tulipokuwa katika uwepo wake, au ndivyo ilivyoonekana. Mahojiano binafsi yalipambwa kwa maandiko. Mihutasari kwa ajili ya … mikutano ilitafutwa kutoka kwenye vitabu vikuu vya Kanisa. …

    “Hatukujua wakati huo, lakini rais wetu alikuwa anatukinga kwenye mkono wa kulia na wa kushoto, akituhimiza kwa nguvu zote za moyo wake na kwa akili zake zote alizokuwa nazo tushikilie kwa nguvu fimbo ya chuma ili kamwe tusiangamie [ona 1 Nefi 15:23–25]” (“The Power of the Scriptures” seminar for new mission leaders, June 25, 2022).