2020
Teksi, Mvulana wa Shule, na Jibu la Sala
Aprili 2020


Teksi, Mvulana wa Shule, na Jibu la Sala

Mwandishi anaishi Jimbo la Rivers, Nigeria.

Tulikuwa na msukumo kwamba tungempata, kwa hivyo ni kwa nini hilo halikufanikiwa?

Picha
A Taxi, a Schoolboy, and an Answer to Prayer. Missionaries in Ghana with a schoolboy in a taxi outside.

Siku moja mimi na mwenza wangu mmisionari tulipewa jina kwa ajili ya kumfundisha mwanaume ambaye aliishi katika kijiji kinachoitwa Tema, karibu na jiji zuri la Accra, Ghana. Nambari za nyumba katika kijiji hicho hazikuwa sahihi, kwa hivyo tulipewa maelezo yaliyokuwa yameandikwa kwenye karatasi kutusaidia kuipata nyumba hiyo.

Wakati tulipowasili katika kijiji, tulifuata maelezo yote lakini hatukuweza kumpata mwanaume huyo kwa sababu ilionekana kwamba kulikuwa na nyumba nyingi ambazo zililingana na maelezo hayo. Tukiwa tunahisi kukanganyikiwa, tuliamua kubisha milango katika ujirani ili kuuliza, lakini hakuna aliyeonekana kumfahamu mwanaume ambaye tulikuwa tunamtafuta. Nilipata msukumo wa kusali kumwomba Baba wa Mbinguni msaada.

Baada ya kusali, nilipata hisia kwamba tungempata mwanaume ambaye tulikuwa tunamtafuta, kwa hivyo tuliongeza juhudi zetu. Bado, hatukumpata. Tulichoka na kuamua kurudi katika eneo letu la kuhubiri kwa sababu tulikuwa na miadi mingine. Wakati tulipofika kwenye uwanja wa teksi, dereva wa teksi ambaye alikuwa ametuleta katika kijiji aliona nyuso zetu za masikitiko na kutuuliza kama tulimpata yule ambaye tulikuwa tunamtafuta. Jibu letu lilikuwa, bila shaka, la!

Alipendekeza kwamba twende ndani ya shule iliyokuwa pembeni na tuulizie hapo. Tulimwelezea kwamba hayo si maelezo ambayo tulikuwa tumepewa, lakini alisisitiza. Tulishuka kutoka ndani ya teksi na kuelekea shuleni—sio kwa sababu tulidhani kwamba tungempata mtu yeyote, lakini kumfurahisha tu rafiki yetu aliyekuwa na wasiwasi.

Wakati tulipoanza kutembea kuelekea katika jengo la utawala la shule, mvulana mdogo alikuja akikimbia upande wetu. Alitabasamu na kutuambia kwamba yeye na kaka yake ndio waumini pekee wa Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho wanaoishi katika eneo hilo na kwamba angeweza kutusaidia.

Mimi na mwenza wangu tuliangaliana kwa mshangao. Ilikuwa ni muujiza. Mvulana huyo alitusaidia kumpata mwanaume ambaye tulikuwa tunamtafuta, na mwishowe alikubali injili na kubatizwa.

Tukio hili lilinifundisha kwamba Baba wa Mbinguni hujibu sala kwa muda Wake na kwa njia Yake mwenyewe. Wakati tunapokosa kupata majibu ya sala zetu mara moja, tunaweza kuwa na imani Kwake na kuwa wavumilivu.

Kielelezo na Corey Egbert