2019
Walipanda Mbegu katika Moyo Wangu
Oktoba 2019


Sauti za Watakatifu wa Siku za Mwisho

Walipanda Mbegu katika Moyo Wangu

Marta Algarve

Santa Catarina, Brazil

Picha
heart-shaped wreath of leaves with seed in middle

Kielelezo na Rafael López

Nilitoka wapi? Ninafanya nini hapa? Nitaenda wapi baada ya maisha haya?

Wakati nikiwa na umri wa miaka 29, maswali haya yaliendelea kujirudia kwangu. Wazazi wangu walikuwa wamefariki. Niliomboleza kwa kumpoteza mwana wangu wa kwanza mchanga. Nilikuwa na watoto wengine watatu wa kulea na maisha yalijaa changamoto.

Bwana alianza kujibu maswali yangu wakati alipowaongoza wamisionari wawili vijana nyumbani kwangu. Nilipowakaribisha ndani, waliniuliza ikiwa kulikuwa na chochote nilichohisi kilikosekana katika maisha yangu. Niliwaambia kuhusu wazazi wangu na mwanangu. Niliwaambia nilidhani isingekuwa sawa kuwa na watoto na kuunda familia ikiwa kila kitu kilihitimishwa na kifo. Niliuliza ikiwa ningeweza kuwaona tena wazazi wangu na mwanangu.

“Marta,” walisema, “unaweza kuwa na familia yako milele.”

Shangwe ilijaza nafsi yangu. Nilitaka kujua zaidi. Kwenye matembezi yao yaliyofuata, walinifundisha zaidi kuhusu injili ya Yesu Kristo. Walinipa Kitabu cha Mormoni na kunipa changamoto ya kukisoma na kumuuliza Mungu ikiwa ni neno Lake. Nilikubali changamoto yao. Niliposali, jibu la Mungu lilikuja wazi kama mng’aro wa jua. Nilijua moyoni mwangu kilikuwa cha kweli.

Kwa bahati mbaya, nilipopata kazi mpya, nilipoteza mawasiliano na wamisionari. Katika miezi iliyofuata, ndoa yangu ilifika kikomo na nilijaribu kuanza maisha mapya pamoja na watoto.

Hatimaye, niliolewa tena. Siku moja mume wangu alisema alikuwa amemkosa sana Mungu katika maisha yake. Tuliamua kuhudhuria kanisa alilokuwa akihudhuria. Tulipoingia ndani ya jengo, niliona Kitabu cha Mormoni juu ya meza ukumbini. Hili lilikuwa kanisa sawa na lile nililotambulishwa kwalo kabla. Nilipenda Roho niliyemhisi pale. Tulipoondoka, nilimuuliza mume wangu ni kwa jinsi gani ningeweza kubatizwa.

“Unahitaji kufundishwa na wamisionari,” alisema.

“Nilifundishwa miaka mitano iliyopita!” Nilijibu.

Mimi na watoto wangu tulifundishwa masomo. Siku yetu ya ubatizo ilikuwa siku yetu ya furaha kuliko siku zote za maisha yetu.

Miaka kadhaa baadaye, nilihisi kwamba nilipaswa kuwaambia akina dada ambao walinifundisha mwanzo kwamba nilikuwa nimejuinga na Kanisa. Kwenye Facebook, nilipata kundi la wamisionari waliorudi kutoka Misheni ya Brazil Santa Maria. Lilimjumuisha mmoja wa akina dada aliyenifundisha. Nilimuomba urafiki na kumwambia nilikuwa nani, jinsi nilivyokuwa muumini wa Kanisa, kwamba familia yetu ilikuwa imeunganishwa hekaluni, na kwamba kijana wangu alikuwa akitumikia misheni kwa muda wote. Nilimwambia haya yote yaliwezekana kwa sababu yeye na mmisionari mwenzake walikuwa wamepanda mbegu ya injili ya urejesho ndani ya moyo wangu.