Maandiko Matakatifu
Ushuhuda wa Mashahidi Watatu


Ushuhuda wa Mashahidi Watatu

Ijulikane kwa mataifa yote, makabila, lugha, na watu, ambao kwao kazi hii itawajia: Kwamba sisi, kwa neema ya Mungu Baba, na Bwana wetu Yesu Kristo, tumeyaona mabamba ambayo yana kumbukumbu hiyo, ambayo ni historia ya watu wa Nefi, na pia ya Walamani, ndugu zao, na pia ya watu wa Yaredi, ambao walitoka kwenye ule mnara ambao tayari umezungumziwa. Na pia sisi tunajua kwamba yametafsiriwa kwa karama na nguvu ya Mungu, kwani sauti yake imetutangazia hayo; kwa hivyo tunajua kwa uhakika kwamba kazi hii ni ya kweli. Na pia tunashuhudia kwamba tumeona michoro ambayo iko juu ya mabamba hayo; na tumeonyeshwa haya kwa uwezo wa Mungu, wala sio wa binadamu. Na tunatangaza kwa maneno ya kiasi, kwamba malaika wa Mungu aliteremka kutoka mbinguni, na akaleta na kulaza mbele ya macho yetu, na tukatazama na kuona mabamba hayo, na michoro yake; na tunajua kwamba ni kwa neema ya Mungu Baba, na ya Bwana wetu Yesu Kristo, kwamba tuliona na tunashuhudia kwamba vitu hivi ni vya kweli. Na ni ya kustaajabisha machoni mwetu. Walakini, sauti ya Bwana ilituamuru kwamba tuishuhudie; kwa hivyo, kwa kutii amri za Mungu, tunatoa ushuhuda wa mambo haya. Na tunajua kuwa kama tutakuwa waaminifu katika Kristo, tutatakasa mavazi yetu kutokana na damu ya watu wote, ili tusipatikane na doa mbele ya kiti cha hukumu cha Kristo, na tutaishi na yeye milele mbinguni. Na utukufu uwe kwa Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu, ambao ni Mungu mmoja. Amina.

Oliver Cowdery

David Whitmer

Martin Harris