2010–2019
Baba
Oktoba 2018


Baba

Kila mmoja wetu ana nafasi ya kuwa kama Baba. Kufanya hivyo, lazima tumwabudu Baba katika jina la Mwana.

Katika maisha yake yote, mke wangu, Melinda, amekuwa akijaribu kwa moyo wake wote kuwa mfuasi mwaminifu wa Yesu Kristo. Lakini, kuanzia ujana wake, alihisi kutostahili upendo na baraka za Baba wa Mbinguni kwa sababu hakuelewa uhalisia Wake. Kwa bahati nzuri, Melinda aliendelea kutii amri licha ya huzuni aliyoihisi. Miaka michache iliyopita, alikuwa na mfuatano wa uzoefu ambao ulimsaidia kuelewa vizuri zaidi uhalisia wa Mungu, ikijumuisha upendo Wake kwa watoto Wake na shukrani Zake hata kwa juhudi zetu zisizo kamilifu za kufanya kazi Yake.

Alielezea jinsi gani hili limeathiri maisha yake: “Sasa ninahisi uhakika kwamba mpango wa Baba unafanya kazi, kwamba Yeye mwenyewe amewekeza katika mafanikio yetu, na kwamba Yeye hutupatia masomo na uzoefu tunaouhitaji ili kurudi katika uwepo Wake. Ninajiona mwenyewe na kuwaona wengine kama vile Mungu anavyotuona. Nina uwezo wa kulea, kufundisha, na kutumikia kwa upendo zaidi na woga kidogo. Ninahisi amani na ujasiri kuliko wasiwasi na woga. Badala ya kuhisi kushutumiwa, ninahisi kusaidiwa. Imani yangu ni dhahiri zaidi. Ninahisi upendo wa Baba yangu mara nyingi zaidi na kwa kina zaidi.”1

Kuwa na wazo sahihi la sifa ya [Baba wa Mbinguni], ukamilifu, na tabia” ni muhimu katika kutumia imani ya kutosha kupata kuinuliwa.2 Uelewa sahihi wa sifa ya Baba wa Mbinguni unaweza kubadili jinsi tunavyojiona na kuwaona wengine na hutusaidia kuelewa upendo wa Mungu usio kifani kwa watoto Wake na hamu Yake kuu ya kutusaidia kuwa kama Yeye. Mtazamo usio sahihi wa uhalisia Wake unaweza kutuacha tukihisi kama vile kamwe hatuna uwezo wa kurudi katika uwepo Wake.

Dhumuni langu leo ni kufundisha dondoo za fundisho kuu kuhusu Baba ambalo litaruhusu kila mmoja wetu, lakini hasa wale ambao wanajiuliza kama Mungu anawapenda, ili kuelewa vizuri tabia Yake ya kweli na kutumia imani kubwa zaidi Kwake, kwa Mwanaye na kwenye mpango Wake kwetu.

Maisha Kabla ya kuja Duniani

Katika maisha kabla ya kuja duniani, tulizaliwa kama roho kwa Wazazi wa Mbinguni na kuishi Nao kama familia.3 Walitujua, walitufundisha, na kutupenda.4 Tulitaka sana kuwa kama Baba yetu wa Mbinguni. Hata hivyo, ili kuwa hivyo, tulitambua kwamba tulitakiwa:

  1. Kupata miili ya nyama na mifupa, iliyotukuka, isiyokufa;5

  2. Kuwa na ndoa na kutengeneza familia kupitia nguvu za kuunganisha za ukuhani;6 na

  3. Kupata ujuzi wote, nguvu, na sifa za kiungu.7

Kama matokeo, Baba alitengeneza mpango ambao ungeturuhusu, kwa masharti fulani,8 kupata miili ya nyama na mifupa ambayo ingekuwa si ya kufa na mitukufu katika Ufufuko; kuwa na ndoa na kutengeneza familia katika maisha ya duniani au, kwa waaminifu ambao hawakupata fursa hii, baada ya maisha ya duniani;9 kuendelea kuelekea ukamilifu; na hatimaye kurudi kwa wazazi Wetu wa Mbinguni na kuishi Nao pamoja na familia zetu katika hali ya kuinuliwa na furaha ya milele.10

Maandiko huita huu mpango wa wokovu.11 Tulishukuru sana kwa mpango huu kwamba wakati ulipoletwa kwetu, tulishangilia kwa furaha.12 Kila mmoja wetu alikubali masharti ya mpango, ikijumuisha uzoefu na changamoto za maisha ya duniani ambazo zingetusaidia kukuza sifa za kiungu.13

Maisha ya Duniani

Katika maisha ya duniani, Baba wa Mbinguni hutupatia masharti yanayotakiwa ili tuendelee katika mpango Wake. Baba alimzaa Yesu Kristo katika mwili14 na akampa Yeye msaada kutoka mbinguni kutimiza kazi Yake duniani. Baba wa Mbinguni vile vile humsaidia kila mmoja wetu kama tutajitahidi kutimiza amri zake.15 Baba hutupatia uhuru wa kuchagua.16 Maisha yetu yako mikononi Mwake, na “siku zetu zinafahamika” na hazitahesabika kuwa chache.”17 Na Anahakikisha kwamba hatimaye mambo yote yatakuwa kwa faida ya wale Wampendao.18

Ni Baba wa Mbinguni ambaye hutupatia mkate wetu wa kila siku,19 ambao hujumuisha vyote chakula tunachokula na nguvu tunazohitaji kutii amri zake.20 Baba hutoa zawadi nzuri.21 Anasikia na kujibu sala zetu.22 Baba wa Mbinguni hutuokoa kutoka kwenye maovu pale tunapomruhusu.23 analia kwa ajili yetu pale tunaposumbuka.24 Hatimaye, baraka zetu zote hutoka kwa Baba.25

Baba wa Mbinguni hutuongoza na kutupatia uzoefu tunaohitaji kulingana na nguvu zetu, udhaifu wetu, na chaguzi zetu ili kwamba tungeweza kuzaa matunda mema.26 Baba huturudi inapohitajika kwa sababu Anatupenda.27 Yeye ni “Mtu wa Ushauri,”28 ambaye atashauriana nasi kama tutamuomba.29

Ni Baba wa mbinguni ambaye hutuma vyote ushawishi na kipawa cha Roho Mtakatifu katika maisha yetu.30 Kupitia kipawa cha Roho Mtakatifu, utukufu—au uelewa, nuru, na nguvu—za Baba vinaweza kukaa ndani yetu.31 Kama tutajitahidi kuongezeka katika nuru na kweli mpaka macho yetu yakawa kwenye utukufu wa Mungu, Baba wa Mbinguni atamtuma Roho Mtakatifu wa Ahadi kututia mhuri katika maisha ya milele na kufunua uso Wake kwetu—iwe katika maisha haya au yajayo.32

Maisha Baada ya Maisha ya Duniani

Katika maisha kwenye ulimwengu wa roho, Baba wa Mbinguni huendelea kumimina Roho Mtakatifu na kutuma wamisionari kwa wale wanaohitaji injili. Anajibu sala na kuwasaidia wale wanaozikosa kupokea ibada okozi kwa niaba yao.33

Baba alimwinua Yesu Kristo na kumpa Yeye nguvu za kuleta Ufufuko,34 ambao ni njia ambayo kwayo tunapokea miili isiyokufa. Ukombozi wa Mwokozi na Ufufuko huturejesha katika uwepo wa Baba, ambapo tutahukumiwa na Yesu Kristo.35

Wale wanaotegemea “fadhili, na rehema, na neema za Masiya Mtakatifu”36 watapokea miili iliyotukuka kama Baba37 na kukaa Naye katika “hali ya furaha isiyo na mwisho.”38 Hapo, Baba atatufuta machozi yetu yote39 na kutusaidia kuendelea mbele katika safari yetu ya kuwa kama Yeye.

Kama unavyoweza kuona, Baba wa Mbinguni mara zote yuko kwa ajili yetu.40

Sifa ya Baba

Ili kuwa kama Baba, lazima tujenge tabia yenye sifa Zake. Ukamilifu na sifa za Baba wa Mbinguni hujumuisha yafuatayo:

  • Baba “Hana Mwisho na ni wa Milele.”41

  • Yeye ni mwenye haki kamili, mwenye rehema, mkarimu, mvumilivu, na hutaka kile kilicho kizuri kwa ajili yetu.42

  • Baba wa Mbinguni ni upendo.43

  • Anatimiza maagano Yake.44

  • Habadiliki.45

  • Hawezi kudanganya.46

  • Baba hampendelei mtu.47

  • Anajua vitu vyote—vilivyopita, vilivyopo, na vijavyo—tangu mwanzo.48

  • Baba wa Mbinguni ana uelewa49 zaidi yetu wote.50

  • Baba ana nguvu zote51 na hufanya vitu vyote ambavyo amenuia moyoni Mwake kufanya.52

Akina kaka na akina dada, tunaweza kumwamini na kumtegemea Baba. Kwa sababu ana mtazamo wa milele, Baba wa Mbinguni anaweza kuona vitu tusivyoweza kuona. Shangwe yake, kazi, na utukufu ni kutuletea kutokufa na kuinuliwa.53 Kila kitu anachofanya ni kwa manufaa yetu. “Anataka furaha [yetu] ya milele hata zaidi ya [sisi] tunavyotaka.”54 Na “hangetuhitaji [sisi] kupitia wakati wa magumu zaidi ya vile inavyohitajika kwa manufaa [yetu] au ya wale [tunao] wapenda.”55 Kama matokeo, Yeye hufokasi katika kutusaidia kuendelea, si katika kutushutumu na kutulaumu.56

Kuwa Kama Baba Yetu

Kama wana na mabinti wa kiroho wa Mungu, kila mmoja wetu ana nafasi ya kuwa kama Baba. Kufanya hivyo, lazima tumwabudu Baba katika jina la Mwana.57 Tunafanya hivi kwa kujitahidi kuwa watiifu kwa mapenzi ya Baba, kama Mwokozi alivyokuwa,58 na kwa kuendelea kutubu.59 Tunapofanya vitu hivi, “tunapokea rehema kwa rehema” mpaka tutakapopokea ukamilifu wa Baba60 na kupata zawadi ya “tabia yake, ukamilifu, na sifa.”61

Umbali uliopo kati ya jinsi tulivyo kama wanadamu wenye kufa na jinsi Baba wa Mbinguni amekuwa, haishangazi kwamba baadhi wanahisi kuwa kama Baba hakuwezekani. Hata hivyo, maandiko yako wazi. Kama tutashikilia imani katika Kristo, kutubu, na kutafuta rehema ya Mungu kupitia utiifu, hatimaye tutakuwa kama Baba. Ninapata faraja kubwa kutokana na ukweli kwamba wale wanaojitahidi kuwa watiifu, “watapokea rehema kwa rehema” na hatimaye “kupokea utimilifu wake.”62 Kwa maneno mengine, hatutakuwa kama Baba kwa kupitia sisi wenyewe.63 Badala yake, itafanyika kupitia zawadi ya rehema, ikiwa kubwa lakini mara nyingi ikiwa ndogo, ambayo hujenga juu ya nyenzake mpaka tuwe na utimilifu. Lakini, akina kaka na akina dada itakuja!

Ninawaalika kuamini kwamba Baba wa Mbinguni anajua jinsi ya kuwainua; tafuta kila siku, msaada Wake; na songa mbele kwa imani katika Kristo hata pale unapoweza kutohisi upendo wa Mungu.

Kuna vingi hatuvielewi kuhusu kuwa kama Baba.64 Lakini ninashuhudia dhahiri kwamba kujitahidi kuwa kama Baba kunastahili kila dhabihu.65 Dhabihu tunazozitoa katika maisha haya ya duniani, hata ziwe kubwa kiasi gani, haziwezi kulinganishwa na shangwe isiyo na kipimo, furaha na upendo tutakaouhisi katika uwepo wa Baba.66 Kama una shaka kuamini kwamba inalingana na dhabihu ambazo unaombwa kutoa, Mwokozi anatoa wito kwako, akisema, “Nanyi bado hamjaelewa jinsi baraka kuu Baba alizo nazo … amezitayarisha kwa ajili yenu; … Na hamwezi kustahimili mambo yote kwa sasa; hata hivyo, changamkeni, kwa kuwa nitawaongoza.”67

Ninashuhudia kwamba Baba yako wa Mbinguni anakupenda na anakutaka wewe uishi Naye tena. Katika jina la Yesu Kristo, amina.