Maandiko Matakatifu
Mawazo ya Kuboresha Kujifunza Maandiko Kwako Binafsi


“Mawazo ya Kuboresha Kujifunza Maandiko Kwako Binafsi,” Mawazo ya Kujifunza Maandiko (2021)

“Mawazo ya Kuboresha Kujifunza Maandiko Kwako Binafsi,” Mawazo ya Kujifunza Maandiko

Picha
mwanamke akisoma maandiko

Mawazo ya Kuboresha Kujifunza Maandiko Kwako Binafsi

Hizi ni baadhi ya njia rahisi za kuboresha kujifunza kwako neno la Mungu katika maandiko.

Sali kwa Ajili ya Mwongozo

Maandiko yana neno la Mungu. Wakati ukiyasoma, mwombe Baba yako wa Mbinguni mwongozo Wake na mpokee Roho Wake ili akusaidie kuyaelewa.

Tafuta Kweli zihusianazo na Yesu Kristo

Maandiko hutufundisha kwamba vitu vyote humshuhudia Kristo (ona 2 Nefi 11:4; Musa 6:63), kwa hivyo mtafute Yeye katika matukio, hadithi, na mafundisho ya maandiko. Fikiria kuandika au kuwekea alama mistari inayofundisha kuhusu Mwokozi na jinsi ya kumfuata.

Tafuta Maneno na Vifungu vya Kutia Moyo

Unaweza kukuta kwamba maneno na vifungu fulani katika maandiko vinakugusa wewe, kana kwamba viliandikwa mahususi kwa ajili yako. Vinaweza kuwa na maana kwako binafsi na kukutia moyo na kukuhamasisha. Fikiria kuviwekea alama katika maandiko yako au kuviandika katika shajara ya kujifunzia.

Tafuta Kweli za Injili

Wakati mwingine kweli za injili (mara nyingi zikiitwa mafundisho au kanuni) zinasemwa wazi, na wakati mwingine zinatolewa kupitia mfano au hadithi. Jiulize, “Ni kweli zipi za injili zinafundishwa katika mistari hii?”

Msikilize Roho Mtakatifu

Kuwa makini na mawazo na hisia zako, hata kama zinaonekana hazihusiani na kile unachokisoma. Misukumo hiyo inaweza kuwa ni mambo hasa ambayo Baba wa Mbinguni anakutaka ujifunze na uhisi.

Picha
mwanamke akisoma maandiko 2

Yafananishe Maandiko na Maisha Yako

Fikiria jinsi hadithi na mafundisho unayoyasoma yanavyohusiana na maisha yako. Kwa mfano, ungeweza kujiuliza, “Je ni uzoefu gani nilioupata ambao unafanana na kile ninachokisoma?” au “Ni kwa jinsi gani ninaweza kufuata mfano wa mtu huyu katika maandiko?”

Uliza Maswali

Kuuliza maswali kuhusu injili kunaweza kukusaidia kuamua ni nini cha kujifunza. Unapojifunza maandiko, maswali pia yanaweza kuja akilini. Maswali haya yanaweza kuhusiana na kile unachokisoma au maisha yako kwa ujumla. Tafakari maswali haya na tafuta majibu kadiri unavyoendelea kujifunza maandiko. Baada ya kujifunza kwako, uliza ni nini zaidi Mungu angependa ujifunze, na subiri majibu wakati wa masaa yajayo na siku zijazo.

Tumia Misaada ya Kujifunza Maandiko

Ili kupata umaizi wa ziada katika mistari unayoisoma, tumia tanbihi, Mwongozo wa Mada, Kamusi ya Biblia, Mwongozo wa Maandiko (scriptures.ChurchofJesusChrist.org), na misaada mingine ya kujifunza.

Zingatia Muktadha wa Maandiko

Unaweza kupata umaizi wa maana kuhusu maandiko kama utazingatia muktadha wake—hali au mazingira ya maandiko. Kwa mfano, kufahamu chimbuko na imani ya watu ambao nabii alizungumza nao kunaweza kukusaidia kuelewa dhamira ya jumbe zake.

Picha
mwanamume akisoma maandiko

Andika Mawazo na Hisia zako

Kuna njia nyingi za kuandika misukumo ambayo hukujia wakati unapojifunza. Kwa mfano, unaweza kuwekea alama neno au kifungu chenye maana na kuandika mawazo yako kama neno la kukumbuka katika maandiko yako. Unaweza pia kutunza shajara ya umaizi, hisia, na misukumo unayoipata. Au unaweza kurekodi swali ambalo uliuliza kabla ya kuanza kujifunza kwako, ikifuatiwa na majibu uliyoelekezwa kwayo.

Jifunze Maneno ya Manabii na Mitume wa Siku za Mwisho

Soma kile ambacho manabii na mitume wa siku za mwisho wamefundisha kuhusu kanuni unazopata ndani ya maandiko. Jumbe zao zinapatikana katika “Magazeti ya Kanisa,” “Mkutano Mkuu wa Kanisa,” na makusanyo mengine katika Maktaba ya Injili.

Soma Hadithi

Soma hadithi katika maandiko, ukitafuta kuelewa muktadha wake (wakati, mahali, mzungumzaji, na hadhira). Hadithi za maandiko zilizo katika kielelezo ni nyenzo kubwa kwa hili, hasa kwa watoto na washiriki wasiojua sana maandiko.

Shiriki Umaizi

Kujadili umaizi kutokana na kujifunza kwako binafsi ni njia nzuri ya kuwafundisha wengine na husaidia kuimarisha uelewa wako katika kile ambacho umesoma.

Ishi kwa Kile Unachojifunza

Kujifunza maandiko kunaweza kutuhamasisha na kutuongoza kubadili jinsi tunayoishi. Sikiliza kile ambacho Roho anakushawishi kufanya wakati unaposoma, na kisha weka kusudio la kuitendea kazi misukumo hiyo.