Mkutano Mkuu
Jinsi Ukuhani Unavyobariki Vijana
Mkutano mkuu wa Aprili 2020


Jinsi Ukuhani Unavyobariki Vijana

Tumepewa nafasi ya kuhudumu kama malaika, kuhubiri injili katika mabara yote ya dunia, na kusaidia roho kuja kwa Kristo.

Akina kaka na akina dada, ninashukuru sana kuzungumza nanyi jioni hii ya kihistoria juu ya zawadi takatifu ya ukuhani na nguvu ya ajabu ulio nao kuwabariki vijana katika wakati huu. Ninaomba kwamba licha ya udhaifu wangu, Roho atanisaidia katika kufundisha ukweli.

Urais wa Kwanza umewakumbusha walio na ukuhani wa Haruni kwamba “unaishi katika siku yenye fursa na changamoto kuu—siku ambayo ukuhani umerejeshwa. Una mamlaka ya kusimamia ibada za Ukuhani wa Haruni. Unapotumia mamlaka hayo kwa kustahili na kwa dhati, utabariki sana maisha ya wale walio karibu nawe.”1 Kama vijana wa Kanisa, tunakumbushwa pia kuwa sisi ni “wana [wapendwa] wa Mungu, na Yeye ana kazi kwa ajili yetu [sisi] kufanya”2 na tunasaidia katika kazi Yake ya “kuleta kutokufa na uzima wa milele wa mwanadamu” (Musa 1:39).

Ukuhani ni mamlaka ya kusimamia ibada na maagano ya injili ya Mwokozi kwa wale wanaostahili kuzipokea. Kupitia kwa ibada hizi za ukuhani na maagano matakatifu huja baraka kamili za Upatanisho wa Mwokozi, ambazo hutusaidia kufikia majaliwa yetu ya Kiungu.

Joseph Smith alikuwa kijana ambaye aliitwa na Mungu ili kurejesha injili ya Yesu Kristo na, kwa kusudi hilo, alipewa ukuhani, ambao alitumia kubariki wanadamu wote. Mafundisho na Maagano 135 inaelezea baraka nyingi ambazo Joseph amewapa vijana wa wakati huu. Tunasoma: “Joseph Smith … amefanya zaidi, isipokuwa Yesu tu, kwa wokovu wa wanadamu katika ulimwengu huu, kuliko mtu mwingine yeyote ambaye amewahi kuishi ndani yake. … Ameleta Kitabu cha Mormoni…; ametuma utimilifu wa injili ya milele…kwenye sehemu nne za dunia; ameleta ufunuo na amri ambazo zinaunda Mafundisho na Maagano …; amewakusanya maelfu mengi ya Watakatifu wa Siku za Mwisho, … na kuacha umaarufu na jina ambalo haliwezi kuuawa ” (Mafundisho na Maagano 135:3).

Ili kutumikia vizuri kama vile Joseph alivyofanya, ni lazima tustahili kutumia nguvu ya ukuhani wa Bwana. Wakati wakitafsiri Kitabu cha Mormoni, Joseph na Oliver Cowdery walitaka kubatizwa, lakini walikosa mamlaka sahihi. Mnamo Mei 15, 1829, walipiga magoti katika maombi na walitembelewa na Yohana Mbatizaji, ambaye aliwapa funguo na mamlaka ya Ukuhani wa Haruni, akisema, “Juu yenu ninyi watumishi wenzangu, katika jina la Masiya, ninawatunukia Ukuhani wa Haruni, ambao hushikilia funguo za huduma ya malaika, na za injili ya toba, na za ubatizo kwa uzamisho kwa ajili ya ondoleo la dhambi” (Mafundisho na Maagano 13:1).

Tumepewa nafasi ya kuhudumu kama malaika, kuhubiri injili katika mabara yote ya dunia, na kusaidia roho kuja kwa Kristo. Huduma hii inatuweka katika kazi ya pamoja na Yohana Mbatizaji, Moroni, Joseph Smith, Rais Russell M. Nelson, na watumishi wengine wenye bidii wa Bwana.

Huduma yetu katika na pamoja na ukuhani Wake inakusanya pamoja wale ambao wamejitolea kufuata na kuishi mafundisho ya Bwana kwa usahihi, ambayo mimi binafsi najua kuwa inaweza kuwa ngumu tunapokabiliana na changamoto za ujana. Lakini kuungana na watumishi hawa wa Bwana katika kutimiza kazi Yake kutasaidia kututia nguvu dhidi ya majaribu na udanganyifu wa mwovu. Unaweza kuwa nuru ya kuashiria kwa wale wote ambao hawajiamini. Nuru iliyo ndani yako itaangaza sana kwamba kila mtu unayekutana naye atabarikiwa kwa kuwa tu na kampani yako. Inaweza kuwa ngumu wakati mwingine kukiri kuwapo kwa wenzi wetu wa kiroho, lakini nashukuru kujua kwamba mimi ni mshiriki wa akidi ya wenye ukuhani waaminifu ambao pamoja nao ninaweza kujitahidi kuwa karibu na Kristo.

Pamoja na marafiki na familia zetu, Roho Mtakatifu ni mmoja wa wenzi wetu waaminifu sana na wa kutegemewa. Lakini ili kualika wenza Wake wa kila wakati, ni lazima tujiweke katika hali na mahali ambapo atataka kuwepo. Hii inaweza kuanzia nyumbani mwetu wenyewe wakati tunapofanya kazi kupafanya pawe mahali patakatifu kwa kushiriki katika kusoma maandiko kila siku na kusali kama familia na, muhimu zaidi, tunapojifunza binafsi maandiko na kusali peke yetu.

Picha
Enzo na dada yake
Picha
Enzo na familia yake

Mapema mwaka huu, nilipewa nafasi ya kusisimua lakini yenye kunyenyekeza ya kumsaidia dada yangu mdogo, Oceane, kuendelea kwenye njia ya agano kwa kukubali mwaliko wa kubatizwa na kutimiza moja ya mahitaji yaliyowekwa ya kuingia ufalme wa selestia. Aliahirisha ubatizo wake kwa mwezi mmoja, hadi nilipotawazwa kuwa kuhani, ili kunipa fursa ya kutekeleza ibada hiyo, wakati dada zetu wengine pia walikuwa na fursa ya kufanya kazi chini ya uteuzi wa ukuhani na kusimama kama mashahidi. Tulipokuwa tumesimama mkabala na kisima cha ubatizo na tukijiandaa kuingia ndani ya maji, niligundua msisimko wake, na ulifanana na wangu. Na nilihisi nimeunganishwa naye, kwa kuona kwamba alikuwa akifanya uamuzi sahihi. Fursa hii ya kutumia ukuhani ilinihitaji kuwa mwangalifu zaidi kutokuwa wa kawaida katika maisha yangu ya kuishi injili. Ili kujiandaa, nilienda hekaluni kila siku juma hilo, nikisaidiwa na mama yangu, bibi, na dada yangu, kufanya ubatizo wa ajili ya wafu.

Uzoefu huu ulinifundisha mengi juu ya ukuhani na jinsi ambavyo ningeweza kuutumia kwa kustahili. Ninajua kuwa wenye ukuhani wote wanaweza kuhisi mambo yale niliyohisi ikiwa tutafuata mfano wa Nefi wa “kwenda na kutenda.” (ona 1 Nefi 3:7). Hatuwezi kukaa bila kufanya kazi na kutarajia Bwana atutumie katika kazi Yake kubwa. Hatupaswi kungojea wale ambao wanahitaji msaada wetu watutafute; ni jukumu letu kama wenye ukuhani kutoa mfano na kusimama kama mashahidi wa Mungu. Ikiwa tunafanya maamuzi ambayo yanatuzuia kwenye ukuaji wetu wa milele, ni lazima tubadilike sasa. Shetani atajaribu kwa bidii yake tote kutuweka katika hali ya mwili ya kutafuta raha za muda. Lakini ninajua kuwa ikiwa tutaweka bidii, kutafuta wale ambao watatuunga mkono, na kutubu kila siku, baraka zitakazokuja zitakuwa za ajabu na maisha yetu yatabadilishwa milele tunapoendelea kusonga mbele kwenye njia ya agano.

Ninajua kwamba hili ni Kanisa la Kweli la Yesu Kristo, ambaye ni Mwokozi wetu na ametoa funguo za ukuhani kwa Mitume Wake, ambao wanazitumia kutuongoza, hasa katika siku hizi za changamoto, na kuuandaa ulimwengu kwa ujio Wake.

Ninajua kwamba Joseph Smith alikuwa nabii wa Urejesho na kwamba Rais Nelson ni nabii wetu anayeishi leo. Ninawaalika sote tujifunze maisha ya hawa wenye ukuhani wakuu na kutafuta kujiboresha sisi wenyewe kila siku ili tuwe tayari kukutana na Muumbaji wetu. Katika jina la Yesu Kristo, amina.

Muhtasari

  1. Urais wa Kwanza, katika Fulfilling My Duty to God (booklet, 2010), 5.

  2. Dhima ya Akidi za Ukuhani wa Haruni, katika General Handbook: Serving in The Church of Jesus Christ of Latter-day Saints, 10.1.2, ChurchofJesusChrist.org.