Vitabu vya Maelekezo na Miito
32. Toba na Mabaraza ya Kanisa ya Uumini


“32. Toba na Mabaraza ya Kanisa ya Uumini,” Kurasa Zilizochaguliwa kutoka Kitabu cha Maelezo ya Jumla (2023).

“32. Toba na Mabaraza ya Kanisa ya Uumini,” Kurasa Zilizochaguliwa kutoka Kitabu cha Maelezo ya Jumla

Picha
wanaume wakizungumza

32.

32. Toba na Mabaraza ya Kanisa ya Uumini

32.0

Utangulizi

Toba nyingi zinafanyika kati ya mtu binafsi, Mungu na wale ambao wamedhurika na dhambi za mtu huyo. Hata hivyo, wakati mwingine askofu au rais wa kigingi anahitaji kusaidia waumini wa Kanisa katika juhudi zao za kutubu.

Wakati wakiwasaidia waumini kwa toba, maaskofu na marais wa vigingi ni wenye upendo na kujali. Wanafuata mfano wa Mwokozi, ambaye aliwainua watu binafsi na aliwasaidia wageuke kutoka katika dhambi na wageuke kumwelekea Mungu (ona Mathayo 9:10–13; Yohana 8:3–11).

32.1

Toba na Msamaha

Ili kuleta mpango wake wa huruma, Baba wa Mbinguni alimtuma Mwanaye wa Pekee, Yesu Kristo, kufanya upatanisho kwa ajili ya dhambi zetu (ona Alma 42:15.). Yesu aliteseka adhabu ambayo sheria ya haki inahitaji kwa ajili ya dhambi zetu (ona Mafundisho na Maagano 19:15–19; ona pia Alma 42:24–25). Kupitia dhabihu hii, wote wawili Baba na Mwana walionesha upendo wao usio na mwisho kwa ajili yetu (ona Yohana 3:16).

Wakati tunapoonesha “imani iongozayo kwenye toba” Baba wa Mbinguni anatusamehe, akitupatia neema kupitia upatanisho wa Yesu Kristo (Alma 34:15; ona pia Alma 42:13). Wakati tunapokuwa tumesafishwa na kusamehewa, hatimaye tunaweza kurithi ufalme wa Mungu (ona Isaya 1:18; Mafundisho na Maagano 58:42).

Toba ni zaidi ya kubadilisha tabia. Ni kugeuka kutoka kwenye dhambi na kuelekea kwa Baba wa Mbinguni na Yesu Kristo. Inaongoza kwenye mabadiliko ya moyo na akili (ona Mosia 5:2; Alma 5:12–14; Helamani 15:7). Kupitia toba, tunakuwa watu wapya, tuliopatanishwa na Mungu (ona 2 Wakorintho 5:17–18; Mosia 27:25–26).

Fursa ya kutubu ni moja ya baraka kuu ambazo Baba wa Mbinguni ametupatia kupitia zawadi ya Mwanaye.

32.2

Madhumuni ya Vizuizi vya Uumini wa Kanisa au Kujiondoa

Kama muumini anafanya dhambi kubwa, askofu au rais wa kigingi anamsaidia atubu. Kama sehemu ya mchakato huu, anaweza kuhitaji kuzuia baadhi ya fursa za uumini wa Kanisa kwa muda. Katika baadhi ya hali, anaweza kuhitaji kuondoa uumini wa mtu kwa muda.

Kuzuia au kuondoa uumini wa mtu haikusudiwi kuwa adhabu. Badala yake, vitendo hivi wakati mwingine ni muhimu kumsaidia mtu kutubu na apate uzoefu wa mabadiliko ya moyo. Pia wanampa mtu muda kujitayarisha kiroho kufanya upya na kushika maagano yake tena.

Makusudi matatu ya vizuizi vya uumini au kuondolewa kwa uumini ni kama ifuatavyo.

32.2.1

Husaidia Kuwalinda Wengine

Kusudi la kwanza ni kusaidia kuwalinda Wengine. Wakati mwingine mtu anakuwa ni tishio kimwili au kiroho. Tabia za unyang’anyi, madhara ya kimwili, unyanyasaji wa kijinsia, matumizi ya madawa ya kulevya, udanganyifu na ukengeufu ni baadhi ya njia ambazo zinaweza kupelekea hili kutokea. Kwa mwongozo wa kiungu, askofu au rais wa kigingi anachukua hatua kuwalinda wengine wakati mtu fulani anapotoa tishio katika njia hizi na zingine ambazo ni hatari (ona Alma 5:59–60).

32.2.2

Humsaidia mtu Kupata Nguvu ya Ukombozi ya Yesu Kristo kupitia Toba

Kusudi la pili ni kumsaidia mtu kupata nguvu ya ukombozi ya Yesu Kristo kupitia toba. Kupitia mchakato huu, anaweza tena kuwa msafi na mwenye kustahili kupokea baraka zote za Mungu.

32.2.3

Hulinda Uadilifu wa Kanisa

Kusudi la tatu ni kulinda uadilifu wa Kanisa. Kuzuia au kuondoa uumini wa Kanisa wa mtu kunaweza kuwa kwa lazima kama tabia yake ina madhara kwa Kanisa (ona Alma 39:11). Uadilifu wa Kanisa haulindwi kwa kuficha au kupunguza dhambi nzito—bali kwa kuzishughulikia.

32.3

Majukumu ya Waamuzi katika Israeli

Maaskofu na marais wa vigingi wanaitwa na kusimikwa kuwa waamuzi katika Israeli (ona Mafundisho na Maagano 107:72–74). Wanashikilia funguo za ukuhani za kumwakilisha Bwana katika kuwasaidia waumini wa Kanisa watubu (ona Mafundisho na Maagano 13:1; 107:16–18).

Mara nyingi maaskofu na marais wa kigingi wanasaidia katika toba kupitia ushauri binafsi. Usaidizi huu unaweza kujumuisha kuzuia kusiko rasmi baadhi ya fursa za uumini wa Kanisa kwa muda.

Kwa baadhi ya dhambi kubwa, viongozi wanawasaidia kwa toba kwa kuitisha baraza la uumini (ona 32.6). Usaidizi huu unaweza kujumuisha kuzuia rasmi baadhi ya fursa za uumini wa Kanisa au kuondoa uumini wa mtu kwa muda.

Maaskofu na marais wa vigingi ni wenye upendo na wanaojali wakati wanapowasaidia waumini watubu. Kuingilia kwa Mwokozi kwenye tukio la mwanamke aliyechukuliwa katika uzinzi ni mwongozo (ona Yohana 8:3–11 Ingawa hakusema dhambi zake zilisamehewa, hakumtia hatiani. Badala yake, Alimwambia “usifanye dhambi tena”—kutubu na kubadili maisha yake.

Viongozi hawa wanafundisha kwamba kuna “furaha … mbinguni juu ya mwenye dhambi mmoja ambaye anatubu” (Luka 15:7). Wana subira, ni wenye msaada na wako chanya. Wanatoa msukumo kwenye tumaini. Wanafundisha na kushuhudia kwamba kwa sababu ya dhabihu ya upatanisho ya Mwokozi, wote wanaweza kutubu na kuwa wasafi.

Maaskofu na marais wa vigingi wanatafuta mwongozo kutoka kwa Roho kujua jinsi ya kumsaidia kila mtu atubu. Ni kwa dhambi kubwa kuliko kiwango ndizo ambazo kwazo Kanisa limeweka viwango vya hatua ambazo viongozi wake wanapaswa kuchukua (ona 32.6). Hakuna hali mbili ambazo ni sawa. Ushauri ambao viongozi wanatoa na njia ya toba wanayoipendekeza lazima iwe na msukumo na yaweza kuwa tofauti kwa kila mtu.

32.4

Kuungama, Usiri, na Kuripoti kwa Mamlaka za Serikali

32.4.1

Kuungama

Toba inahitaji kwamba dhambi iungamwe kwa Baba wa Mbinguni. Yesu Kristo alisema, “Kwa hili mnaweza kujua kama mtu ametubu dhambi zake—tazama, ataungama na kuziacha” (Mafundisho na Mafundisho na Maagano 58:43.; ona pia Mosia 26:29).

Wakati waumini wa Kanisa wanapofanya dhambi kubwa, toba zao pia hujumuisha kuungama kwa askofu wao au rais wa kigingi. Kisha anaweza kutumia funguo za injili ya toba kwa niaba yao (ona Mafundisho na Maagano 13:1; 84:26–27; 107:18, 20). Hii inawasaidia wapone na kurudi kwenye njia ya injili kupitia nguvu za Upatanisho za Mwokozi.

Kusudi la kuungama ni kuwatia moyo waumini wajitue mzigo wao wenyewe ili waweze kikamilifu kutafuta msaada wa Bwana katika kubadilika na kupona. Kukuza “moyo uliovunjika na roho iliyopondeka” kunasaidiwa na kuungama (2 Nefi 2:7). Kuungama kwa hiari kunaonesha kwamba mtu huyo anatamani kutubu.

Wakati mtu anaungama, askofu au rais wa kigingi anafuata maelekezo kwa ajili ya ushauri katika 32.8. Kwa sala anatafuta mwongozo kuhusu mazingira yanayofaa kwa ajili ya kumsaidia muumini atubu. Anazingatia ikiwa baraza la uumini litakuwa na msaada. Kama sera za Kanisa zinahitaji baraza la uumini, anaelezea hili (ona 32.6).

Wakati mwingine muumini anakuwa amemkosea mwenza au mtu mzima mwingine. Kama sehemu ya toba, mtu huyo anapaswa kwa kawaida akiri kwa mtu yule na kuomba msamaha. Kijana anayefanya dhambi kubwa kwa kawaida anahimizwa kushauriana na wazazi wake.

32.4.4

Usiri

Maaskofu, marais wa vigingi na washauri wengine wana kazi takatifu ya kulinda taarifa zote za siri walizoshirikishwa. Taarifa hii inaweza kutokana na usaili, ushauri na kuungama. jukumu sawa na hilo la usiri linahusika kwa wote wanaoshiriki katika mabaraza ya uumini. Usiri ni muhimu kwa sababu waumini wanaweza wasikiri dhambi au kutafuta mwongozo ikiwa kile wanachokishiriki hakitakuwa na usiri. Kuvunja ujasiri kunasaliti imani ya waumini na kuwasababishia kupoteza ujasiri kwa viongozi wao.

wakidumu katika jukumu lao la usiri, askofu, rais wa kigingi au washauri wao wanaweza tu kushiriki taarifa kama hizo kama ifuatavyo:

  • Wanahitaji kujadiliana na rais wake wa kigingi, rais wa misheni au askofu kuhusu kuendesha baraza la uumini au mada zinazohusiana na hizo.

  • Mtu huyo kahamia kata mpya (au kiongozi wa ukuhani amepumzishwa) wakati hatua kwa muumini au mambo mengine mazito yakiwa hayajatatuliwa.

  • Askofu au rais wa kigingi amegundua kwamba muumini wa Kanisa anayeishi nje ya kata au kigingi anaweza kuwa amehusika na dhambi kubwa.

  • Ni muhimu kutoa taarifa wakati wa baraza la uumini.

  • Muumini anachagua kutoa ruhusa kwa ajili ya kiongozi kushiriki taarifa na watu maalumu.

  • Inaweza kuwa ni lazima kushiriki taarifa kidogo kuhusu maamuzi ya baraza la uumini.

Ili kuwasaidia viongozi katika kuwalinda wengine na kufuata sheria, Kanisa linatoa msaada kutoka kwa wataalamu wenye weledi. Ili kupokea mwongozo huu, viongozi bila kuchelewa wanatafuta kituo cha msaada cha unyanyasaji cha Kanisa pale kinapopatikana (ona 38.6.2.1). Pale ambapo hakipo, rais wa kigingi anawasiliana na mshauri wa kisheria wa eneo kwenye ofisi ya eneo.

Ni katika hali moja tu askofu au rais wa kigingi anapaswa kutoa taarifa za siri bila kwanza kutafuta mwongozo kama huo. Huo ni wakati ambapo utoaji siri ni lazima ili kuzuia madhara yanayotishia maisha au majeraha makubwa na hakuna muda wa kutafuta mwongozo. Katika hali kama hizo, jukumu la kuwalinda wengine ni muhimu zaidi kuliko jukumu la usiri. Viongozi wanapaswa kuwasiliana na mamlaka ya serikali mara moja.

32.6

Uzito wa Dhambi na Sera za Kanisa

Uzito wa dhambi ni kigezo muhimu katika kuamua mazingira ambayo (1) yatasaidia kuwalinda wengine na (2) kumsaidia mtu atubu. Bwana amesema kwamba Yeye “hawezi kuiangalia dhambi na kuivumilia hata kidogo” (Mafundisho na Maagano 1:31; ona pia Mosia26:29). Watumishi wake hawapaswi kudharau ushahidi wa dhambi kubwa.

Dhambi kubwa ni chukizo la dhahiri na kubwa dhidi ya sheria za Mungu. Aina za dhambi kubwa zimeorodheshwa hapa chini.

  • Vitendo vya fujo na unyanyasaji

  • Uasherati/uzinzi

  • Vitendo vya udanganyifu

  • Kuvunja uaminifu

  • Baadhi ya vitendo vingine

Wakati Baraza la Uumini Linapohitajika au Linaweza Kuwa la Muhimu

Aina ya Dhambi

Baraza la Uumini Linahitajika

Baraza la Uumini Linaweza Kuwa la Muhimu

Aina ya Dhambi

Vitendo vya Fujo na Unyanyasaji

Baraza la Uumini Linahitajika

  • Mauaji

  • Ubakaji

  • Hatia ya shambulio la kijinsia

  • Unyanyasaji wa mtoto au kijana

  • Tabia ya unyang’anyi wa nguvu

Baraza la Uumini Linaweza Kuwa la Muhimu

  • Jaribio la kujiua

  • Unyanyasaji wa kijinsia, ukijumuisha shambulio la kimwili na unyanyasaji (ona 38.6.18 ili kujua wakati baraza linapohitajika)

  • Unyanyasaji wa mwenza au mtu mzima mwingine (ona 38.6.2.4 ili kujua wakati baraza linapohitajika)

Aina ya Dhambi

Uasherati/Uzinzi

Baraza la Uumini Linahitajika

  • Kujamiiana kwa maharimu

  • Ponografia ya watoto

  • Ndoa ya mitala

  • Tabia ya unyang’anyi wa kijinsia

Baraza la Uumini Linaweza Kuwa la Muhimu

  • Zinaa, uasherati, mahusiano ya jinsia moja na mahusiano yote ya kijinsia nje ya ndoa ya kisheria kati ya mwanamume na mwanamke, ikijumuisha maongezi ya kingono mtandaoni au kwa simu.

  • Kuishi pamoja bila ndoa, kukubaliana kukaa pamoja kimila na ndoa ya jinsia moja

  • Matumizi makubwa ya ponografia au ya kulazimisha ambayo yamesababisha madhara makubwa kwa ndoa ya muumini au familia ya muumini

Aina ya Dhambi

Vitendo vya Udanganyifu

Baraza la Uumini Linahitajika

  • Tabia ya udanganyifu wa fedha, kama vile ulaghai na shughuli zifananazo na hizo (ona 32.6.3.3 kama muumini alihusika katika ubadhirifu wa pesa au mali za Kanisa)

Baraza la Uumini Linaweza Kuwa la Muhimu

  • Unyang’anyi, wizi wa kuvunja, wizi au ubadhirifu (ona 32.6.3.3 kama muumini alihusika katika ubadhirifu wa pesa au mali za Kanisa)

  • Kosa la Kusema Uongo

Aina ya Dhambi

Ukiukaji wa Uaminifu

Baraza la Uumini Linahitajika

  • Dhambi kubwa wakati unashikilia nafasi kubwa Kanisani

Baraza la Uumini Linaweza Kuwa la Muhimu

  • Dhambi kubwa wakati unashikilia nafasi ya mamlaka au kuaminika katika Kanisa au jamii (ona 32.6.3.3 kama muumini alihusika katika ubadhirifu wa pesa au mali za Kanisa)

  • Dhambi kubwa ambayo inajulikana kote

Aina ya Dhambi

Baadhi ya Vitendo Vingine

Baraza la Uumini Linahitajika

  • Kupatikana na hatia mara nyingi

Baraza la Uumini Linaweza Kuwa la Muhimu

  • Utoaji mimba (isipokuwa upekee katika 38.6.1 unatumika)

  • Mpangilio wa dhambi kubwa

  • Utelekezaji kwa makusudi wajibu wa familia, ikijumuisha kutotoa msaada wa matunzo kwa mtoto na masurufu baada ya mume kumwacha mke

  • Uuzaji wa dawa za kulevya

  • Matendo mengine makubwa ya jinai

32.6.3

Wakati Rais wa Kigingi Anaposhauriana na Urais wa Eneo kuhusu Ikiwa Baraza la Uumini au Hatua Nyingine ni Muhimu

Baadhi ya mada zinahitaji umakini zaidi na mwongozo. Ili kujua jinsi nzuri ya kusaidia, rais wa kigingi lazima ashauriane na Urais wa Eneo kuhusu hali husika katika sehemu hii.

32.6.3.2

Ukengeufu

Maswala ya ukengeufu mara nyingi yana athari inayoenda zaidi ya mipaka ya kata au kigingi. Yanahitaji kushughulikiwa kwa haraka ili kuwalinda wengine.

Askofu anashauriana na rais wa kigingi kama anahisi kwamba kitendo cha muumini kinaweza kupelekea ukengeufu.

Kama lilivyotumika hapa, ukengeufu humaanisha kwamba muumini anajihusisha na chochote kati ya vifuatavyo:

  • Upinzani wa kujirudia na wa makusudi wa hadharani dhidi ya Kanisa, mafundisho yake, sera zake au viongozi wake

  • Kuendelea kufundisha kama mafundisho ya Kanisa kile ambacho siyo mafundisho ya Kanisa baada ya kusahihishwa na askofu au rais wa kigingi

  • Kuonesha mwenendo wa makusudi wa kufanya kazi ili kudhoofisha imani na shughuli za waumini wa Kanisa

  • Kuendelea kufuata mafundisho ya madhehebu yaliyokengeuka baada ya kusahihishwa na askofu au rais wa kigingi

  • Kujiunga rasmi na kanisa jingine na kueneza mafundisho yake

32.6.3.3

Ubadhirifu wa Pesa za Kanisa

Kama muumini anafanya ubadhirifu wa pesa za Kanisa au anaiba mali za thamani za Kanisa, rais wa kigingi anashauriana na Urais wa Eneo kuhusu ikiwa baraza la uumini au hatua nyingine inaweza kuwa muhimu.