Maandiko Matakatifu
Etheri 7


Mlango wa 7

Oriha anatawala kwa haki—Katika hali ya mapinduzi na mzozo, falme za upinzani za Shule na Kohori zinaanzishwa—Manabii wanalaani uovu na kuabudu kwa sanamu kwa watu, ambao kisha wanatubu.

1 Na ikawa kwamba Oriha alitoa hukumu kwenye nchi kwa haki siku zake zote, ambaye siku zake zilikuwa nyingi sana.

2 Na alizaa wana na mabinti; ndiyo, alizaa thelathini na mmoja, miongoni mwao walikuwa wana ishirini na watatu.

3 Na ikawa kwamba pia alimzaa Kibu katika umri wake wa uzee. Na ikawa kwamba Kibu alitawala badala yake; na Kibu akamzaa Korihori.

4 Na wakati Korihori alipokuwa na miaka thelathini na miwili aliasi dhidi ya baba yake, na akaenda kuishi katika nchi ya Nehori; na alizaa wana na mabinti, na wakawa warembo sana; kwa hivyo Korihori aliwavutia wengi kumfuata.

5 Na baada ya kukusanya pamoja jeshi alikuja kwenye nchi ya Moroni ambapo mfalme aliishi, na kumchukua mateka, ambako kulileta kutimia amsemo wa kaka wa Yaredi kwamba watawekwa kwenye utumwa.

6 Sasa nchi ya Moroni, ambako mfalme aliishi, ilikuwa karibu na nchi inayoitwa Ukiwa na Wanefi.

7 Na ikawa kwamba Kibu aliishi utumwani, na watu wake chini ya Korihori mwana wake, mpaka alipokuwa mzee sana; walakini Kibu alimzaa Shule katika umri wake wa uzee, wakati alipokuwa bado utumwani.

8 Na ikawa kwamba Shule alimkasirikia kaka yake; na Shule akaongezeka nguvu, na akawa mwenye nguvu kulingana na nguvu ya mwanaume; na pia alikuwa mkuu kwa kuhukumu.

9 Kwa hivyo, alienda kwenye kilima cha Efraimu, na akayeyusha chuma kutoka kwa kile kilima, na kutengeneza mapanga kutoka kwa chuma cha pua kwa wale ambao alikuwa amekuja nao; na baada ya kuwahami kwa panga alirejea kwenye mji wa Nehori, na kupigana vita na kaka yake Korihori, kwa njia ambayo alijipatia ufalme na kuurudisha kwa baba yake Kibu.

10 Na sasa kwa sababu ya kitu ambacho Shule alifanya, baba yake alimpa ufalme; kwa hivyo alianza kutawala badala ya baba yake.

11 Na ikawa kwamba alitoa hukumu kwa haki; na alisambaza ufalme wake juu ya nchi yote, kwani watu walikuwa wameongezeka sana.

12 Na ikawa kwamba Shule pia alizaa wana na mabinti wengi.

13 Na Korihori alitubu kutoka kwa maovu mengi ambayo alikuwa ameyafanya; kwa hivyo Shule alimpatia uwezo katika ufalme wake.

14 Na ikawa kwamba Korihori alikuwa na wana wengi na mabinti wengi. Na miongoni mwa wana wa Korihori kulikuwa na mmoja ambaye jina lake lilikuwa Nuhu.

15 Na ikawa kwamba Nuhu aliasi dhidi ya Shule, mfalme, na pia baba yake Korihori, na kumvuta kaka yake Kohori kumfuata, na pia ndugu zake wote na wengi wa watu wengine.

16 Na alifanya vita na Shule, mfalme, ambamo kwake alipata nchi ya urithi wa kwanza; na akawa mfalme juu ya sehemu hiyo ya nchi.

17 Na ikawa kwamba alifanya vita tena na Shule, mfalme; na akamshika Shule, mfalme, na kumchukua mbali hadi Moroni kama mateka.

18 Na ikawa wakati alipokuwa karibu kumuua, wana wa Shule walienda polepole hadi kwenye nyumba ya Nuhu usiku na kumuua, na walivunja mlango wa gereza na kumtoa nje baba yao, na kumweka kwenye kiti cha enzi cha ufalme wake.

19 Kwa hivyo, mwana wa Nuhu aliimarisha ufalme wake badala yake; walakini hawakupata uwezo tena juu ya Shule, mfalme, na watu waliokuwa chini ya utawala wa Shule, mfalme, walifanikiwa sana na walikuwa na nguvu.

20 Na nchi iligawanywa; na kukawa na falme mbili, falme ya Shule, na falme ya Kohori, mwana wa Nuhu.

21 Na Kohori, mwana wa Nuhu, alisababisha kwamba watu wake wapigane na Shule, ambapo Shule aliwashinda na kumuua Kohori.

22 Na sasa Kohori alikuwa na mwana aliyeitwa Nimrodi; na Nimrodi alisalimisha ufalme wa Kohori kwa Shule, na alipata fadhila za Shule; kwa hivyo Shule alimpatia mapendeleo mengi, na alifanya chochote kulingana na kutaka kwake katika ufalme wa Shule.

23 Na pia katika utawala wa Shule kulikuwa na manabii miongoni mwa watu, ambao walitumwa kutoka kwa Bwana, wakitabiri kwamba uovu na kuabudu asanamu kwa watu kulikuwa kumeleta laana juu ya nchi, na wangeangamizwa kama hawangetubu.

24 Na ikawa kwamba watu walitoa matusi dhidi ya manabii, na kuwafanyia mzaha. Na ikawa kwamba mfalme Shule aliwaadhibu wale wote waliotoa matusi dhidi ya manabii.

25 Na aliweka sheria kote nchini, ambayo iliwapatia manabii uwezo kwamba wangeenda popote walipotaka; na katika njia hii watu waliletwa kwenye toba.

26 Na kwa sababu watu walitubu kutoka kwa uovu wao na kuabudu sanamu kwao Bwana aliwasamehe, na wakaanza kufanikiwa tena nchini. Na ikawa kwamba Shule alizaa wana na mabinti katika umri wake wa uzee.

27 Na hapakuwepo na vita tena katika siku za Shule; na alikumbuka vitu vikubwa ambavyo Bwana alikuwa amewafanyia babu zake katika kuwaleta akuvuka kilindi kikubwa hadi kwenye nchi ya ahadi; kwa hivyo alitoa hukumu katika haki siku zake zote.