Vitabu vya Maelekezo na Miito
1. Mpango wa Mungu na Wajibu Wako katika Kazi ya Wokovu na Kuinuliwa


“1. Mpango wa Mungu na Wajibu Wako katika Kazi ya Wokovu na Kuinuliwa,” Kurasa Zilizochaguliwa kutoka kwenye Kitabu cha Maelezo ya Jumla (2013).

“1. Kazi ya Wokovu na Kuinuliwa,” Kurasa Zilizochaguliwa kutoka kwenye Kitabu cha Maelezo ya Jumla

Picha
wanaume wakijenga nyumba

1.

Mpango wa Mungu na Wajibu Wako katika Kazi ya Wokovu na Kuinuliwa

1.0

Utangulizi

Umeitwa kuhudumu katika Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho. Asante kwa huduma yako. Utabariki maisha ya watu na utapata furaha unapohudumu kwa imani.

Kitabu hiki cha maelezo ya jumla kitakusaidia ujifunze kanuni za huduma kama ya Kristo na uelewe majukumu yako. Utakuwa mwenye ufanisi zaidi wakati utakapofunganisha huduma yako katika Kanisa na kazi ya Mungu Baba na Mwanaye, Yesu Kristo.

1.1

Mpango wa Mungu wa Furaha

Baba wa Mbinguni alitoa mpango wa furaha ili kutuwezesha sisi kufurahia baraka zake zote. Kazi Yake na utukufu wake ni “kuleta kutokufa na uzima wa milele wa mwanadamu” (Musa 1:39).

Yesu Kristo ni kiini cha mpango wa Mungu. Kwa sababu ya upendo usio na mwisho wa Baba wa Mbinguni kwetu, Alimtuma Mwanaye ili kutukomboa sisi kutokana na dhambi na kifo kupitia dhabihu Yake ya upatanisho (ona Yohana 3:16). Kupitia Upatanisho Wake, Yesu Kristo anahakikisha kwamba kila mmoja wetu aliyezaliwa duniani atafufuliwa na kupata kutokufa. Upatanisho wake pia unawezesha sisi kusafishwa kutokana na dhambi na kufanya mioyo yetu ibadilishwe ili tuweze kupokea uzima wa milele na utimilifu wa furaha.

Ili kupokea uzima wa milele, ni lazima sisi “tuje kwa Kristo, na kukamilishwa ndani Yake” (Moroni 10:32).

1.2

Kazi ya Wokovu na Kuinuliwa

Tunapokuja kwa Kristo na kuwasaidia wengine kufanya vivyo hivyo, tunashiriki katika kazi ya Mungu ya wokovu na kuinuliwa. Kazi hii inaongozwa na amri kuu mbili kumpenda Mungu na kuwapenda majirani zetu (ona Mathayo 22:37–39).

Kazi ya Wokovu na kuinuliwa inalenga kwenye majukumu manne ya kiungu yaliyoteuliwa.

Kitabu hiki cha maelezo ya jumla kitakusaidia uelewe vipengele hivi vinne vya kazi ya Mungu. Roho Mtakatifu atakuongoza unapofanya sehemu yako katika kuyatimiza hayo (ona 2 Nefi 32:5).

1.2.1

Kuishi Injili ya Yesu Kristo

Kuishi injili ya Yesu Kristo kunajumuisha:

  • Kuonesha imani katika Kristo, kutubu kila siku, kufanya maagano na Mungu tunapopokea ibada za wokovu na kuinuliwa, na kuvumilia hadi mwisho kwa kuyashika maagano hayo (ona 3.5.1).

  • Kujifunza na kufundisha injili ya Yesu Kristo nyumbani na Kanisani.

  • Kuwa wenye kujitegemea katika kujikimu kwa ajili yetu wenyewe na familia zetu, kiroho na kimwili.

1.2.2

Kuwajali Wale Wenye Mahitaji

Kuwajali wale wenye shida kunajumuisha:

  • Kuwahudumia na kuwatumikia watu binafsi, familia, na jumuiya.

  • Kushiriki rasilimali, pamoja na msaada wa Kanisa, kwa wale wenye mahitaji.

  • Kuwasaidia wengine wawe wenye kujitegemea.

1.2.3

Kuwaalika Wote Waipokee Injili

Kuwaalika wote waipokee injili kunajumuisha:

  • Kushiriki katika kazi ya umisionari na kuhudumu kama wamisionari.

  • Kuwasaidia waumini wa Kanisa wapya na wanaorudi kuendelea kusonga kwenye njia ya agano.

1.2.4

Kuziunganisha Familia Milele

Kuziunganisha familia milele kunajumuisha:

  • Kufanya maagano tunapopokea ibada zetu wenyewe za hekaluni.

  • Kuwagundua mababu zetu waliofariki na kufanya ibada kwa niaba yao katika hekalu ili nao waweze kufanya maagano na Mungu.

  • Kwenda hekaluni mara kwa mara, pale inapowezekana, ili kumwabudu Mungu na kufanya ibada kwa ajili ya watoto Wake.

1.3

Lengo la Kanisa

Yesu Kristo alianzisha Kanisa Lake ili kuwawezesha watu binafsi na familia wafanye kazi ya wokovu na kuinuliwa (ona Waefeso 4:11–13; ona pia sehemu ya 2.2 katika kitabu hiki cha maelezo). Ili kusaidia kukamilisha lengo hili takatifu, Kanisa na viongozi wake wanatoa:

  • Mamlaka na funguo za ukuhani.

  • Maagano na ibada.

  • Maelekezo ya Kinabii.

  • Maandiko Matakatifu.

  • Msaada wa kujifunza na kufundisha injili.

  • Fursa za huduma na uongozi.

  • Jumuiya ya Watakatifu.

1.3.1

Mamlaka na Funguo za Ukuhani

Kupitia ukuhani, Mungu anakamilisha kazi ya wokovu na kuinuliwa. Mamlaka na funguo za ukuhani zinazohitajika kuelekeza kazi ya Mungu duniani zilirejeshwa kwa Nabii Joseph Smith (ona Mafundisho na Maagano 110:11–16; 112:30). Funguo hizi zinashikiliwa na viongozi wa Kanisa leo. Wanawaita na kuwapa mamlaka wengine ili kusaidia katika kazi ya Mungu (ona Mafundisho na Maagano 107:8, 65–67).

1.3.2

Maagano na Ibada

Katika mpango wa Baba wa Mbinguni, tunafanya maagano tunapopokea ibada za wokovu na kuinuliwa, kama vile ubatizo (ona Yohana 3:5; ona pia sura ya 18 katika kitabu hiki cha maelezo). Maagano haya na ibada ni muhimu kwa ajili yetu sisi ili kuwa zaidi kama Mungu na kurudi kuishi katika uwepo Wake (ona Mafundisho na Maagano 84:19–22)).

1.3.3

Maelekezo ya Kinabii

Kupitia manabii Wake wateule, Mungu anafunua ukweli na kutoa mwongozo wa kiungu na maonyo (ona Amosi 3:7; Mafundisho na Maagano 1:4). Mwongozo huu unatusaidia sisi tuingie na tubaki kwenye njia inayoongoza kwenye uzima wa milele.

1.3.4

Maandiko Matakatifu

Chini ya maelekezo ya manabii na mitume wa Bwana, Kanisa linatoa na kuhifadhi neno la Mungu kama linavyopatikana katika maandiko matakatifu. Maandiko hushuhudia juu ya Kristo, hufundisha injili Yake, na kutusaidia sisi kuonesha imani Kwake (ona Yakobo 7:10–11; Helamani 15:7).

1.3.5

Msaada wa Kujifunza na Kufundisha Injili

Kanisa linawasaidia watu binafsi na familia katika wajibu wao wa kujifunza kweli za injili na kufundisha kweli hizi kwa wanafamilia na watu wengine (ona Mafundisho na Maagano 88:77–78,118; ona pia 2.2.3 katika kitabu hiki cha maelezo).

1.3.6

Fursa za Huduma na Uongozi

Kupitia miito na upangaji wa majukumu katika Kanisa, Mungu anatoa fursa kwa waumini kuhudumu na kuongoza. Kanisa linatoa mpangilio ili kusaidia kuwajali waumini wenye mahitaji na kutoa msaada wa kibinadamu kwa wengine (ona Mosia 18:27–29).

1.3.7

Jumuiya ya Watakatifu

Kama jumuiya ya Watakatifu, waumini wa Kanisa hukusanyika mara kwa mara ili kumwabudu Mungu na kumkumbuka Mwokozi kwa kushiriki sakramenti (ona Moroni 6:4–6; Mafundisho na Maagano 20:77). Waumini pia wanajaliana na kuhudumiana (ona Waefeso 2:19).

1.4

Wajibu Wako katika Kazi ya Mungu

Kama kiongozi katika Kanisa, umeitwa kufundisha na kuwasaidia wale unaowahudumia pale wanaposhiriki katika kazi ya Wokovu na kuinuliwa (ona 1.2). Wewe unawajibika katika kutimiza wito wako na “kufundisha … neno la Mungu kwa bidii zote” (Yakobo 1:19). Kufanya kazi na Bwana katika shamba Lake la mizabibu kutakuletea furaha kubwa (ona Yakobo 5:70–72).

Kuwa na uelewa dhahiri wa kazi ya Mungu, wa kile Anachokualika ufanye, na kuhusu lengo la Kanisa Lake kutakusaidia kufokasi juhudi zako katika kuzileta nafsi kwa Kristo.

Rejelea mara kwa mara kwenye kanuni zilizoko katika sura hii. Kwa sala tafuta kujua jinsi unavyoweza kusaidia kufikisha malengo ya Mungu katika maisha ya hao unaowatumikia. Mungu atakuelekeza kupitia ushawishi wa Roho Mtakatifu.