Agano la Kale 2022
Mawazo ya Kuboresha Kujifunza Maandiko Kwako Binafsi


“Mawazo ya Kuboresha Kujifunza Maandiko Kwako Binafsi,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: Agano Jipya 2022 (2021)

“Mawazo ya Kuboresha Kujifunza Maandiko Kwako Binafsi,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: 2022

Picha
mwanamke akisoma maandiko nyumbani

Mawazo ya Kuboresha Kujifunza Maandiko Kwako Binafsi

Hizi ni baadhi ya njia rahisi za kuboresha kujifunza kwako neno la Mungu katika maandiko.

Tafuta Ukweli kuhusu Yesu Kristo

Maandiko hutufundisha kwamba vitu vyote humshuhudia Kristo (ona 2 Nefi 11:4; Musa 6:63), kwa hivyo weka kumbukumbu au alama mistari ambayo inafundisha kuhusu Mwokozi na jinsi ya kumfuata Yeye.

Tafuta Maneno na Vifungu vya Kutia Moyo

Unaweza kukuta kwamba maneno na vifungu fulani katika maandiko vinakugusa wewe, kana kwamba viliandikwa mahususi kwa ajili yako. Vinaweza kuwa na maana kwako binafsi na kukutia moyo na kukuhamasisha. Unaweza kuviwekea alama katika maandiko yako au kuviandika katika shajara ya kujifunzia.

Tafuta Kweli za Injili

Wakati mwingine kweli za injili (mara nyingi zikiitwa mafundisho au kanuni) zinasemwa wazi, na wakati mwingine zinatolewa kupitia mfano au hadithi. Jiulize, “Ni kweli zipi za milele zinafundishwa katika mistari hii?”

Msikilize Roho

Kuwa makini na mawazo na hisia zako, hata kama havihusiani na kile unachokisoma. Misukumo hiyo inaweza kuwa ni mambo hasa ambayo Baba wa Mbinguni anakutaka ujifunze.

Yafananishe Maandiko na Maisha Yako

Fikiria jinsi hadithi na mafundisho unayoyasoma yanavyohusiana na maisha yako. Kwa mfano, ungeweza kujiuliza, “Je ni uzoefu gani nilioupata ambao unafanana na kile ninachokisoma?” au “Ni kwa jinsi gani ninaweza kufuata mfano wa mtu huyu katika maandiko?”

Uliza Maswali Unapojifunza

Unapojifunza maandiko, maswali yanaweza kuja akilini. Maswali haya yanaweza kuhusiana na kile unachokisoma au maisha yako kwa ujumla. Tafakari maswali haya na tafuta majibu kadiri unavyoendelea kujifunza maandiko.

Picha
vijana wakijifunza maandiko nyumbani

Tumia Misaada ya Kujifunza Maandiko

Ili kupata umaizi wa ziada katika mistari unayoisoma, tumia tanbihi, Mwongozo wa Mada, Kamusi ya Biblia, Mwongozo wa Maandiko (scriptures.ChurchofJesusChrist.org), na misaada mingine ya kujifunza.

Zingatia Muktadha wa Maandiko

Unaweza kupata umaizi wa maana kuhusu maandiko kama utazingatia muktadha wake—hali au mazingira katika maandiko. Kwa mfano, kufahamu chimbuko na imani ya watu ambao nabii alizungumza nao kunaweza kukusaidia kuelewa dhamira ya maneno yake.

Andika Mawazo na Hisia zako

Kuna njia tofauti za kuandika misukumo ambayo hukujia unapojifunza. Kwa mfano, ungeweza kuwekea alama neno lenye maana au kifungu na kuandika mawazo yako kama neno la kukumbuka katika maandiko yako. Unaweza pia kutunza shajara ya umaizi, hisia, na misukumo unayoipata.

Jifunze Maneno ya Manabii na Mitume wa Siku za Mwisho

Soma kile ambacho manabii na mitume wa siku za mwisho wamefundisha kuhusu kanuni unazozipata ndani ya maandiko (kwa mfano, ona conference.ChurchofJesusChrist.org na majarida ya Kanisa).

Shiriki Umaizi

Kujadili umaizi kutokana na kujifunza kwako kibinafsi sio tu ni njia nzuri ya kuwafundisha wengine, bali pia husaidia kuimarisha uelewa wako katika kile ambacho umesoma.

Ishi kwa Kile Unachojifunza

Kujifunza maandiko hakupaswi tu kututia moyo lakini pia kunapaswa kutuongoza kwenye kubadilisha jinsi tunavyoishi. Sikiliza kile ambacho Roho anakushawishi kufanya unaposoma, na kisha diriki kuitendea kazi misukumo hiyo.

Mzee David A. Bednar alisema: “Hatupaswi kutegemea Kanisa kama taasisi kutufundisha au kutuambia kila kitu tunachohitaji kujua na kufanya ili kuwa wafuasi tulioongoka na kuvumilia kishujaa mpaka mwisho [ona Mafundisho na Maagano 121:29]. Badala yake, wajibu wetu binafsi ni kujifunza kile tunachopaswa kujifunza, kuishi kama tunavyojua tunapaswa kuishi, na kuwa yule ambaye Bwana angetaka tuwe. Na nyumba zetu ni mpangilio wa mwisho kwa ajili ya kujifunza, kuishi, na kuwa” (“Kujiandaa Kupata Kila kitu Kinachohitajika,” Ensign au Liahona, Mei 2019,102).