Mkutano Mkuu
Omba, Tafuta, na Bisha
Mkutano Mkuu wa Oktoba 2020


Omba, Tafuta, na Bisha

Sehemu muhimu ya mpango wa Baba wa Mbinguni ni fursa ya kuwasiliana Naye wakati wowote tunapotaka.

Miezi minne iliyopita, katika masomo yangu ya maandiko, nilikuwa nikisoma juu ya misheni ya Alma huko Amoniha wakati nilipopata pendekezo hili kwenye Njoo, Unifuate: “Unaposoma juu ya baraka kuu ambazo Mungu aliwapa watu wa Nefi (ona Alma 9:19–23), tafakari baraka kubwa alizokupa.”1 Niliamua kufanya orodha ya baraka za Mungu kwangu na kuirekodi katika mwongozo wangu wa kidijiti. Katika muda wa dakika chache, nilikuwa nimeorodhesha baraka 16.

Za kwanza kati ya hizo zilikuwa baraka kubwa za rehema ya Mwokozi na dhabihu ya upatanisho kwa niaba yangu. Niliandika pia juu ya baraka niliyokuwa nayo kumwakilisha Mwokozi kama mmisionari kijana nchini Ureno na, baadaye, na mwenzi mpendwa wangu wa milele, Patricia, katika Misheni ya Brazil Porto Alegre Kusini, ambapo tulihudumu na wamisionari 522 wenye nguvu na wa ajabu. Nikizungumzia juu ya Patricia, baraka nyingi nilizoandika siku hiyo ni baraka ambazo tumefurahia pamoja katika kipindi chote cha miaka 40 ya ndoa—ikiwa ni pamoja na kufunganishwa katika Hekalu la São Paulo Brazil, watoto wetu watatu wazuri, wenzi wao wa ndoa, na wajukuu wetu 13.

Mawazo yangu yakawageukia pia wazazi wangu waadilifu, ambao walinilea katika kanuni za injili. Nilikumbushwa haswa wakati mama yangu mwenye upendo alipiga magoti pamoja nami kusali kando ya kitanda changu nilipokuwa na umri wa miaka 10. Lazima alihisi kuwa ikiwa maombi yangu yangeenda kumfikia Baba yangu wa Mbinguni, yangehitaji kuboreshwa. Kwa hivyo akasema, “Nitasali kwanza, na baada ya sala yangu, utasali.” Aliendelea na mtindo huu kwa usiku mwingi, hadi alipoamini kuwa nimejifunza kanuni na kwa mazoezi jinsi ya kuzungumza na Baba wa Mbinguni. Nitamshukuru milele kwa kunifundisha kusali, kwani nilijifunza kwamba Baba yangu wa Mbinguni husikia maombi yangu na kuyajibu.

Kwa hakika, hiyo ilikuwa baraka nyingine ambayo niliijumuisha katika orodha yangu—karama ya kuweza kusikia na kujifunza mapenzi ya Bwana. Sehemu muhimu ya mpango wa Baba wa Mbinguni ni fursa ya kuwasiliana Naye wakati wowote tunapotaka.

Mwaliko kutoka kwa Bwana

Wakati Mwokozi alipotembelea Amerika baada ya Ufufuo Wake, Alirudia mwaliko ambao alikuwa amewapa wanafunzi Wake kule Galilaya. Alisema:

“Ombeni, na mtapewa; tafuteni na mtapata, bisheni, na mtafunguliwa.

“Kwani kila mmoja ambaye huuliza, hupata; na yule anayetafuta, huvumbua; na yule ambaye hubisha, hufunguliwa.” (3 Nefi 14:7–8; ona pia Mathayo 7:7–8).

Nabii wetu, Rais Russell M. Nelson, ametoa mwaliko kama huo katika siku zetu. Alisema: “Omba katika jina la Yesu Kristo kuhusu matatizo yako, hofu zako, udhaifu wako—ndio, mahitaji ya moyo wako. Na kisha sikiliza! Andika mawazo ambayo yanakuja kwenye akili yako. Andika hisia zako na zifuatilie kwa vitendo ambavyo unashawishiwa kufanya. Unaporudia utaratibu huu siku baada ya siku, mwezi baada ya mwezi, mwaka baada ya mwaka, ‘utakua katika kanuni za ufunuo.’”2

Rais Nelson aliongeza, “Katika siku zijazo, haitawezekana kunusurika kiroho bila uzoefu wa kuongoza, kuelekeza, kufariji na ushawishi wa daima wa Roho Mtakatifu.”3

Kwa nini ufunuo ni muhimu sana kwa kunusurika kiroho? Kwa sababu ulimwengu unaweza kuwa wenye kuchanganya na wenye kelele, uliojaa udanganyifu na mahangaiko. Mawasiliano na Baba yetu wa Mbinguni hutuwezesha kupambanua yaliyo ya kweli na ya uwongo, ambayo yanafaa kwa mpango wa Bwana kwetu na ambayo hayafai. Ulimwengu pia unaweza kuwa wenye ukali na wa kuvunja moyo. Lakini tunapofungua mioyo yetu katika maombi, tutahisi faraja ambayo hutoka kwa Baba yetu wa Mbinguni na uhakikisho kwamba Yeye anatupenda na anatuthamini sisi.

Uliza:

Bwana alisema kwamba “Kwani kila mmoja ambaye huuliza, hupata.” Kuuliza kunaonekana rahisi, lakini ni kitu chenye nguvu kwa sababu kinadhihirisha hamu zetu na imani yetu. Walakini, inachukua muda na uvumilivu kujifunza kuelewa sauti ya Bwana. Tunatilia maanani mawazo na hisia zinazokuja akilini na mioyoni mwetu, na tunaziandika, kama vile nabii wetu alivyotushauri kufanya. Kurekodi maoni yetu ni sehemu muhimu ya kupokea. Inatusaidia kukumbuka, kurejelea, na kuhisi tena kile Bwana anatufundisha.

Hivi karibuni mpendwa mmoja aliniambia, “Ninaamini ufunuo binafsi kuwa ni wa kweli. Nimaamini Roho Mtakatifu atanionyesha mambo yote ninayopaswa kufanya.4 Ni rahisi kuamini ninapohisi mwako kifuani mwangu bila kuwa na dhamira ya shaka.5 Lakini ninawezaje kuwa na Roho Mtakatifu akinena nami kila wakati katika kiwango hiki? ”

Kwa mpendwa wangu na kwenu nyote, ningesema kwamba mimi pia ningependa kuhisi kila mara hisia hizo za nguvu kutoka kwa Roho na daima kuona vyema njia ya kufuata. Lakini sivyo. Hatahivyo, kile tunachoweza kuhisi mara nyingi zaidi ni sauti ndogo, tulivu ya Bwana ikinong’ona akilini na mioyoni mwetu, “mimi niko hapa. Ninawapenda. Songa mbele; fanya kwa uwezo wako wote. Nitawasaidia.” Hatuhitaji kila wakati kujua kila kitu au kuona kila kitu.

Ile sauti ndogo, tulivu inathibitisha, inatia moyo, na inafariji—na mara nyingi hiyo ndiyo tu tunayohitaji kwa siku hiyo. Roho Mtakatifu ni halisi na misukumo Yake ni halisi—yote mikubwa na midogo.

Tafuta

Bwana aliendelea kuahidi, “yule anayetafuta, huvumbua.” Kutafuta kunamaanisha juhudi za kiakili na kiroho—kutafakari, kujipima, kujaribu, na kujifunza. Tunatafuta kwa sababu tunaamini ahadi za Bwana. “Kwa maana kila mtu anayemwendea Mungu ni lazima aamini kwamba Mungu yuko, na kwamba huwatunza wale wanaomtafuta.” (Waebrania 11:6). Tunapotafuta, tunakubali kwa unyenyekevu kwamba bado tuna mengi ya kujifunza, na Bwana atapanua uelewa wetu, akituandaa kupokea zaidi. “Kwani tazama, hivyo ndivyo asemavyo Bwana Mungu: Nitawapatia watoto wa watu mstari juu ya mstari, amri juu ya amri, hapa kidogo na pale kidogo; … kwani kwa yule ambaye hupokea nitampatia zaidi” (2 Nefi 28:30).

Bisha

Hatimaye, Bwana alisema, “yule ambaye hubisha, hufunguliwa.” Kubisha ni kutenda kwa imani. Tunapomfuata Yeye kikamilifu, Bwana anafungua njia mbele yetu. Kuna wimbo mzuri ambao unatufundisha “kuamka na kufanya kitu zaidi ya kuota kuhusu nyumba [yetu] iliyo juu. Kufanya mema ni raha, furaha isiyo na kipimo, baraka ya wajibu na upendo.”6 Mzee Gerrit W. Gong wa Akidi ya wale Kumi na Wawili hivi majuzi alielezea kwamba ufunuo mara nyingi huja tunapokuwa katika tendo la kutenda mema. Alisema, “Tunapojaribu kuwafikia kwa huduma wale wanaotuzunguka, nadhani Bwana anatupatia kipimo cha ziada cha upendo Wake kwao na kwa hivyo kwetu. Nadhani tunasikia sauti Yake, tunamhisi kwa njia tofauti—tunapoomba kuwasaidia wale wanaotuzunguka kwa sababu hayo ni mojawapo ya maombi ambayo Anataka kuyajibu zaidi.”7

Mfano wa Alma

Pendekezo hilo rahisi kwenye Njoo Unifuate la kufikiria juu ya baraka zangu lilileta roho nzuri na ufahamu wa kiroho uliokuwa haujatarajiwa. Nilipoendelea kusoma juu ya Alma na huduma yake huko Amoniha, niligundua kwamba Alma anatoa mfano mzuri wa maana ya kuomba, kutafuta, na kubisha. Tunasoma kuwa “Alma alitia bidii sana katika roho, akipambana na Mungu katika sala kuu, ili awateremshie watu Roho wake.” Sala hiyo, hata hivyo, haikujibiwa jinsi alivyotarajia, na Alma alitupwa nje ya mji. “Akizidiwa sana na huzuni,” Alma alikuwa tayari kukata tamaa, wakati malaika alipomfikishia ujumbe huu: “Heri wewe, Alma; kwa hivyo, inua kichwa chako na ufurahi, kwani una sababu kubwa ya kufurahi.” Malaika kisha akamwambia arudi Amoniha na kujaribu tena, na Alma “alirejea upesi.”8

Je, tunajifunza nini kutoka kwa Alma juu ya kuomba, kutafuta, na kubisha? Tunajifunza kuwa sala inahitaji kazi ya kiroho, na si kila wakati itapelekea kwenye matokeo tunayotarajia. Lakini tunapohisi kuvunjika moyo au kulemewa na huzuni, Bwana hutupa faraja na nguvu kwa njia tofauti. Huenda asijibu yote ya maswali yetu au kutatua matatizo yetu mara moja, ila anatutia moyo tuendelee kujaribu. Ikiwa basi kwa haraka tutaoanisha mpango wetu na mpango Wake, Atatufungulia njia, kama alivyofanya kwa Alma.

Ni ushuhuda wangu kwamba huu ni wakati wa utimilifu wa injili. Tunaweza kufurahia baraka za Upatanisho wa Yesu Kristo katika maisha yetu. Tunayo maandiko yanayopatikana kwa wingi kwetu. Tunaongozwa na manabii ambao hutufundisha mapenzi ya Bwana kwa nyakati ngumu tunazoishi. Kwa kuongezea, tuna msaada wa moja kwa moja wa ufunuo wetu wenyewe ili Bwana aweze kutufariji na kutuongoza sisi binafsi. Kama vile malaika alivyomwambia Alma tuna “sababu kubwa ya kufurahi.”(Alma 8:15). Katika Jina la Yesu Kristo, amina.