Mkutano Mkuu
Jamii Endelevu
Mkutano Mkuu wa Oktoba 2020


Jamii Endelevu

Kama sisi na majirani zetu kwa kiwango cha kutosha tutajitahidi kuongoza maisha yetu kwa ukweli wa Mungu, maadili mema yanayohitajika katika kila jamii yatakuwepo.

Ni uimbaji mzuri ulioje wa kwaya wa wimbo Mwokozi mzuri.

Mwaka 2015 Marekani ilikubali kile kilichoitwa “Ajenda ya Maendeleo Endelevu kwa Mwaka 2030.” Ilielezewa kama “mpango shirikishi kwa ajili ya amani na ustawi wa watu na dunia, sasa na katika siku zijazo.” Ajenda kwa ajili ya Maendeleo Endelevu inajumuisha malengo 17 ya kufikiwa ifikapo mwaka 2030, kama vile hakuna ufukara, hakuna njaa, elimu bora, usawa wa kijinsia, maji safi na uondoaji maji machafu na takataka, na kazi nzuri. 1

Dhana ya maendeleo endelevu inapendeza na ni muhimu. Muhimu zaidi, hata hivyo, ni swali pana la jamii endelevu. Je, ni ipi misingi ambayo inaendeleza jamii inayochanua, ile inayohamasisha furaha, maendeleo, amani, na ustawi miongoni mwa watu wake? Tunazo kumbukumbu za kimaandiko za angalau jamii mbili za aina hiyo. Tunaweza kujifunza nini kutoka kwao?

Hapo kale, patriaki mkuu na nabii Henoko alihubiri haki na “akajenga mji ambao uliitwa Mji wa Utakatifu, Sayuni.” 2 Inaripotiwa kwamba “Bwana aliwaita watu wake Sayuni, kwa sababu walikuwa wa moyo mmoja na wazo moja, na waliishi katika haki; na hakukuwa na maskini miongoni mwao.” 3

“Naye Bwana akaibariki nchi, nao walibarikiwa juu ya milima, na juu ya mahali palipoinuka, na wakastawi.” 4

Watu wa karne ya kwanza na ya pili katika nusu ya Magharibi waliojulikana kama Wanefi na Walamani wanatoa mfano mwingine wa wazi wa jamii zilizostawi. Kufuatia huduma iliyotukuka ya Mwokozi mfufuka miongoni mwao, “walitembea kulingana na amri ambazo walipokea kutoka kwa Bwana wao na Mungu wao, wakiendelea katika kufunga na sala, na kwa kukutana pamoja mara kwa mara ili kuomba na kusikia neno la Bwana. …

“Na hakukuwa na wivu, wala ubishi, wala misukosuko, wala ukahaba, wala uwongo, wala mauaji, wala uzinifu wa aina yoyote; na kweli hakujakuwa na watu ambao wangekuwa na furaha zaidi miongoni mwa watu wote ambao waliumbwa na mkono wa Mungu.” 5

Jamii katika mifano hii miwili zilisaidiwa na baraka za mbinguni zilizoongezeka kutokana na mfano wao wa kujitoa kwenye amri kuu mbili: “Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili yako yote,” na “Mpende jirani yako kama nafsi yako.” 6 Walikuwa watiifu kwa Mungu katika maisha yao binafsi, na walijali ustawi wa kimwili na kiroho wa kila mmoja wao. Katika maneno ya Mafundisho na Maagano, hizi zilikuwa jamii ambazo “kila mtu alitafuta ustawi wa jirani yake, na kufanya mambo yote kwa ajili ya utukufu wa Mungu.” 7

Kwa bahati mbaya, kama Mzee Quentin L. Cook alivyokumbusha asubuhi ya leo, jamii kamilifu iliyoelezewa katika 4 Nefi katika Kitabu cha Mormoni haikustahimili zaidi ya karne yake ya pili. Uendelevu hauna garantii, na jamii inayojitahidi inaweza kuanguka baada ya muda fulani kama itaacha maadili makuu ambayo yanashikilia amani na ustawi wake. Katika suala hili, wakikubali majaribu ya ibilisi, watu “wakaanza kugawanyika katika madaraja; na wakaanza kujijengea makanisa yao wenyewe ili kupata faida, na wakaanza kukataa kanisa la kweli la Kristo.” 8

“Na ikawa kwamba wakati miaka mia tatu ilipokwisha, watu wa Nefi na Walamani walikuwa waovu sana mmoja sawa na mwingine.” 9

Kufikia mwisho wa karne nyingine, mamilioni walikuwa wamekufa katika vita vya wenyewe kwa wenyewe na taifa lao lililokuwa lenye maelewano likashushwa kuwa makabila yanayopigana.

Tukitafakari juu ya hili na mifano mingine ya jamii zilizowahi kustawi ambazo baadae zilizama, nafikiri ni salama kusema kwamba wakati watu wanapogeuka kutoka kwenye kuwajibika kwa Mungu na badala yake kuanza kutegemea “mkono wa mwanadamu,” majanga yanaingia. Kutegemea mkono wa mwanadamu ni kumpuuza Mwanzilishi mtakatifu wa haki za binadamu na utu wa binadamu na kutoa kipaumbele cha juu kabisa kwenye utajiri, madaraka, na sifa za ulimwengu (wakati mara nyingi ukiwafanyia mzaha na kuwatesa wale wanaofuata kiwango tofauti). Wakati huo huo, wale walio katika jamii endelevu hutafuta, kama Mfalme Benyamini alivyosema, “kuendelea wakiwa katika ufahamu wa utukufu wa yule [aliyewaumba], au katika ufahamu wa yale yaliyo ya haki na kweli.” 10

Taasisi za familia na dini zimekuwa muhimu katika kuwapa watu binafsi na jumuiya maadili ambayo yanasaidia jamii endelevu. Maadili haya, yakiwa na mizizi katika injili, yanajumuisha uadilifu, majukumu na uwajibikaji, huruma, ndoa, na uaminifu katika ndoa, heshima kwa wengine na mali za wengine, huduma, na umuhimu na heshima ya kazi, miongoni mwa mengine.

Mhariri kwenye Large Gerard Baker aliandika makala mwanzoni mwa mwaka huu katika Wall Street Journal akitoa heshima kwa baba yake, Frederick Baker, katika tukio la kumbukumbu ya miaka 100 ya kuzaliwa kwake. Baker alikisia kuhusu sababu za maisha marefu ya baba yake lakini kisha akaongeza mawazo haya:

“Wakati pengine sote tungetaka kujua siri ya maisha marefu, mara nyingi mimi huhisi ingekuwa bora zaidi kama tungeutoa muda wetu katika kufikiria ni kitu gani kinafanya maisha yawe mazuri, bila kujali tumepewa muda kiasi gani wa kuishi. Hapa, nina hakika ninajua siri ya baba yangu.

“Yeye anatoka enzi zile wakati maisha kimsingi yalikuwa yakifafanuliwa kwa kazi, siyo kwa kuwa na kitu; kwa wajibu katika jamii, siyo marupurupu binafsi. Kanuni ya msingi iliyokuwa inachangamsha katika karne yake yote imekuwa ni dhana ya wajibu—kwa familia, Mungu, nchi.

“Katika enzi iliyotawaliwa na mabaki ya familia zilizovunjika, baba yangu alikuwa mume mwaminifu kwa mke wake wa miaka 46, baba mwenye kuwajibika wa watoto sita. Hakuwahi kuwepo mara nyingi zaidi na kuwa wa muhimu zaidi kuliko wakati wazazi wangu walipoteseka kwa janga lisilofikirika la kupoteza mtoto. …

“Na katika enzi ambapo dini inazidi kuwa udadisi unaoongezeka, baba yangu ameishi kama Mkatoliki wa kweli, mwaminifu, mwenye imani isiyotingishika katika ahadi za Kristo. Ndiyo, wakati mwingine ninafikiri yeye ameishi miaka mingi kwa sababu amejitayarisha vyema zaidi kuliko mtu yeyote niliyemwona akikaribia kufariki.

“Nimekuwa mtu mwenye bahati—niliyebarikiwa kwa elimu nzuri, familia yangu mwenyewe nzuri, baadhi ya mafanikio ya kiulimwengu ambayo sikuyastahili. Lakini bila kujali fahari na shukrani niliyonayo, imetiwa giza na fahari na shukrani niliyo nayo kwa ajili ya mtu ambaye, pasipo kelele au mbwembwe, pasipo matarajio ya thawabu au hata kutambulika, ameendelea—kwa karne sasa—na kazi za kawaida, wajibu na hatimaye, shangwe ya kuishi maisha mema.” 11

Mtazamo wa umuhimu wa dini na imani ya kidini umeshuka katika mataifa mengi katika miaka ya hivi karibuni. Ongezeko la idadi ya watu wanafikiri kwamba imani katika, na utiifu kwa Mungu havihitajiki ili kuwa na maadili safi kwa watu binafsi au jamii katika ulimwengu wa leo. 12 Nafikiri sote tungekubali kwamba wale ambao hawatamki imani ya dini wanaweza kuwa, na mara nyingi, ni wema, watu wenye maadili. Tusingekubali, hata hivyo, kwamba hii inatokea pasipo ushawishi wa kiungu. Ninamaanisha ile nuru ya Kristo. Mwokozi alitamka, “Mimi ni nuru ya kweli imwangazayo kila mtu ajaye ulimwenguni.” 13 Iwe unatambua hili au la, kila mwanamume, mwanamke, na mtoto wa kila imani, mahali, na wakati ametiwa moyoni Nuru ya Kristo na kwa hiyo anayo akili ya kujua jema na baya ambayo mara nyingi tunaiita dhamiri. 14

Hata hivyo, wakati elimu dunia inapotenganisha maadili binafsi na ya kiraia kutoka kwenye dhana ya uwajibikaji kwa Mungu, inaukata mmea kutoka kwenye mizizi yake. Utegemezi kwenye mila na desturi pekee haitatosha kudumisha maadili katika jamii. Wakati mtu anapokuwa hana mungu wa juu zaidi yake yeye mwenyewe na hatafuti wema wa juu zaidi ya kuridhisha matamanio na mapendeleo yake mwenyewe, madhara yatajitokeza katika wakati wake.

Jamii, kwa mfano, ambamo ridhaa ya mtu ndiyo kipingamizi pekee kwenye shughuli ya kingono ni jamii iliyooza. Uzinzi, uasherati, uzaaji nje ya ndoa, 15 na uchaguzi wa kutoa mimba ni baadhi tu ya matunda machungu ambayo hukua kutokana na mageuzi yanayoendelea ya kujamiiana. Matokeo yanayofuatia ambayo hufanya kazi dhidi ya uendelevu wa jamii yenye ustawi yanajumuisha idadi kubwa ya watoto wanaolelewa katika umasikini na pasipo ushawishi chanya wa akina baba, wakati mwingine kwa vizazi vingi; wanawake wakibeba peke yao kile ambacho kilipaswa kuwa majukumu ya kushirikiana; na upungufu mkubwa wa elimu pale ambapo shule, kama taasisi zingine, zinabebeshwa mzigo kufidia kushindwa kulikotokea nyumbani. 16 Yaliyoongezwa kwenye magonjwa haya ya kijamii ni matukio yasiyopangilika ya kuvunjika moyo na kukata tamaa kwa mtu binafsi—maangamizo ya kiakili na kihisia yakiwaadhibu wote mwenye hatia na asiye na hatia.

Nefi anatangaza:

“Ole kwa yule anayetii mawaidha ya wanadamu, na kukana nguvu za Mungu na kipawa cha Roho Mtakatifu! …

“… Ole kwa wale wote wanaotetemeka, na wanakasirika kwa sababu ya ukweli wa Mungu!” 17

Kinyume chake, ujumbe wetu wa shangwe kwa watoto wetu na kwa wanadamu wote ni kwamba “ukweli wa Mungu” unaonyesha njia bora, au kama Paulo alivyosema, “njia iliyo bora zaidi,” 18 njia ielekeayo kwenye furaha binafsi na ustawi wa jumuiya sasa na kwenye amani isiyo na mwisho na shangwe baada ya hapa.

Ukweli wa Mungu unarejelea kwenye kiini cha kweli ambazo ni msingi wa mpango Wake wa furaha kwa ajili ya watoto Wake. Kweli hizi ni kwamba Mungu yu hai; kwamba Yeye ni Baba wa Mbinguni wa roho zetu; kwamba kama dhihirisho la upendo Wake, Yeye ametupatia amri ambazo zinatuongoza kwenye utimilifu wa furaha pamoja Naye; kwamba Yesu kristo ni Mwana wa Mungu na ni Mkombozi wetu; kwamba Yeye aliteseka na kufa ili kulipia dhambi zetu kwa masharti ya toba yetu; kwamba alifufuka kutoka wafu, akileta Ufufuko wa wanadamu wote; na kwamba sisi sote tutasimama mbele yake ili kuhukumiwa, ambako ni, kutoa hesabu ya maisha yetu. 19

Miaka tisa katika kile kilichoitwa “utawala wa waamuzi,” katika Kitabu cha Mormoni, nabii Alma alijiuzulu nafasi yake kama mwamuzi mkuu ili kutoa muda wake wote kwenye uongozi wa Kanisa. Madhumuni yake yalikuwa kuelezea kiburi, mateso, na ulafi ambavyo vilikuwa vikiongezeka miongoni mwa watu na hususani miongoni mwa waumini wa Kanisa. 20 Kama Mzee Stephen D. Nadauld wakati mmoja alivyosema, uamuzi wa “[Alma] wenye msukumo wa kiungu haukuwa kutumia muda zaidi ili kujaribu kutengeneza na kutunga sheria zaidi ili kurekebisha tabia za watu wake, bali kuzungumza nao kuhusu neno la Mungu, kufundisha mafundisho na kufanya uelewa wao juu ya mpango wa ukombozi uwaongoze kubadili tabia zao.” 21

Kuna mengi tunayoweza kufanya kama majirani na raia wenza ili kuchangia kwenye uendelevu na mafanikio ya jamii ambamo ndani yake tunaishi, na hakika huduma yetu ya msingi kabisa na ya kudumu itakuwa ni kufundisha na kuishi kulingana na kweli hizi za asili zilizo katika mpango mkuu wa Mungu wa ukombozi. Kama ilivyoelezwa katika maneno ya wimbo wa kanisa:

Imani ya baba zetu, tutawapenda

Wote rafiki na adui katika migongano yetu yote,

Na kukuhubiri wewe, pia, kadiri upendo ujuavyo,

Kwa maneno ya ukarimu na maisha mema. 22

Kama sisi na majirani zetu kwa kiwango cha kutosha tutajitahidi kufanya maamuzi na kuongoza maisha yetu kwa ukweli wa Mungu, maadili mema yanayohitajika katika kila jamii yatakuwepo.

Kwa upendo Wake, Baba yetu wa Mbinguni Alimtoa Mwanawe wa Pekee, Yesu Kristo, ili tupate uzima wa milele. 23

“[Yesu Kristo] hafanyi chochote ila tu kwa manufaa ya ulimwengu; kwani anaupenda ulimwengu, hata kwamba anatoa maisha yake ili awavute wanadamu wote kwake. Kwa hivyo, hamwamuru yeyote asipokee wokovu wake.

“Tazama, je yeye hulilia yeyote, na kusema: Niondokeeni? Tazama, ninawaambia, Hapana; lakini husema: Njooni kwangu nyote kutoka pande zote za mwisho wa ulimwengu, nunueni maziwa na asali bila pesa na bila bei.” 24

Hili tunatamka “kwa taadhima moyoni, kwa roho ya unyenyekevu,” 25 na katika jina la Yesu Kristo, amina.

Muhtasari

  1. Ona “The 17 Goals,” United Nations Department of Economic and Social Affairs website, sdgs.un.org/goals.

  2. Musa 7:19.

  3. Musa 7:18.

  4. Musa 7:17.

  5. 4 Nefi 1:12, 16.

  6. Mathayo 22:37, 39.

  7. Mafundisho na Maagano 82:19.

  8. 4 Nefi 1:26.

  9. 4 Nefi 1:45.

  10. Mosia 4:12.

  11. Gerard Baker, “A Man for All Seasons at 100,” The Wall Street Journal, Feb. 21, 2020, wsj.com.

  12. Ona Ronald F. Inglehart, “Giving Up on God: The Global Decline of Religion,” Foreign Affairs, Sept./Oct. 2020, foreignaffairs.com; see also Christine Tamir, Aidan Connaughton, and Ariana Monique Salazar, “The Global God Divide,” Pew Research Center, July 20, 2020, especially infographic “Majorities in Emerging Economies Connect Belief in God and Morality,” pewresearch.org.

  13. Mafundisho na Maagano 93:2; ona pia Moroni 7:16, 19.

  14. ona Boyd K. Packer, “Nuru ya Kristo,” Liahona, Apr. 2005, 10; ona pia D. Todd Christofferson, “Truth Endures,” Religious Educator, vol. 19, no. 3 (2018), 6.

  15. Katika kutoa mfano huu, ninazungumzia juu ya matokeo muhimu yasiyofaa kwa watoto kama “matunda machungu” na si watoto wenyewe. Kila mtoto wa Mungu ana thamani, na kila uhai una thamani isiyopimika licha ya mazingira ya kuzaliwa.

  16. Ona, kwa mfano, Pew Research Center, “The Changing Profile of Unmarried Parents,” Apr. 25, 2018, pewsocialtrends.org; Mindy E. Scott and others, “5 Ways Fathers Matter,” June 15, 2016, childtrends.org; and Robert Crosnoe and Elizabeth Wildsmith, “Nonmarital Fertility, Family Structure, and the Early School Achievement of Young Children from Different Race/Ethnic and Immigration Groups,” Applied Developmental Science, vol. 15, no. 3 (July–Sept. 2011), 156–70.

  17. 2 Nefi 28:26, 28.

  18. 1 Wakorintho 12:31.

  19. Ona Alma 33:22.

  20. Ona Alma 4:6–19.

  21. Stephen D. Nadauld, Principles of Priesthood Leadership (1999), 13; ona pia Alma 31:5.

  22. “Faith of Our Fathers,” Nyimbo za Kanisa, na. 84.

  23. Ona Yohana 3:16.

  24. 2 Nefi 26:24–25; ona pia 2 Nefi 26:33.

  25. Mafundisho na Maagano 100:7.